To Chat with me click here

Saturday, December 1, 2012

CHADEMA YAMKOROGA JK


DK. SLAA ADAI JK ANAMLINDA IGP MWEMA


HOJA nzito zinazoendelea kuibuliwa na viongozi waandamizi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuhusu utendaji wa Rais Jakaya Kikwete, zinaonekana kuwa mwiba na kuikoroga serikali yake.

Wakati hoja ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, ya uteuzi wa baadhi ya majaji wasio na sifa ikiwa bado haijapatiwa majibu ya kuridhisha, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, naye amepigilia msumari mwingine akisema Rais Kikwete anamlinda Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Said Mwema.

Dk. Slaa aliibua hoja hiyo wakati akizungumzia mauaji mbalimbali yanayodaiwa kufanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya raia wema, akisema hali hiyo ni matokeo ya IGP Mwema, kulindwa na mkuu wake, na hivyo kushindwa kuwachukulia hatua wahusika.

Wakati hoja hizo zikiibuliwa, wasaidizi waandamizi wa Rais Kikwete wakiwemo mawaziri na watendaji wengine, wameonekana kupwaya, wakishindwa kuhimili mikiki ya kutoa majibu yenye kufafanua kile kinachohojiwa.

Akizungumza jana jijiji Dar es Salaam, wakati akifungua mkutano mkuu wa chama hicho Jimbo la Kinondoni, Dk. Slaa alisema kama IGP Mwema anashindwa kuchukua hatua juu ya matatizo yanayojitokeza, ikiwamo mauaji na kujeruhi wanayofanyiwa wananchi na polisi, rais anapaswa kuchukua hatua kwa lengo la kuiokoa nchi.

Huku akirejea matukio kadhaa ya mauaji na mateso mbalimbali yaliyofanyika katika mikoa ya Tabora, Morogoro, Iringa, Arusha, Mara, Mwanza, Mbeya, Dar es Salaam na maeneo mengine, Dk. Slaa alisema sheria zipo wazi juu ya suala hilo katika kuunda tume ya kimahakama katika kupata ukweli wa madhila hayo.

“Nyote mnajua kuwa haki katika nchi yetu imekuwa bidhaa adimu, matukio ya kutisha yanajitokeza kila siku, viongozi wenye dhamana na maisha yetu wanakaa kimya, katika hili kama rais hajui sheria si ana watu wanaomsaidia, hivi haoni hata haja ya kuunda tume huru ya kimahakama?” alihoji.

Alisema kuwa kutokana na ukimya wa rais, ikiwa ni pamoja na kushindwa kuwachukulia hatua Waziri wa Mambo ya Ndani, IGP Mwema, makamanda wa polisi wa mikoa ya Iringa na Morogoro, CHADEMA watakutana kabla ya Krismasi na kutoa msimamo wa nini kifanyike kutetea haki ya wananchi.

Dk. Slaa alisema madhumuni ya CHADEMA ni kukuza, kulinda na kutetea haki za binadamu, hivyo wanapaswa kuhakikisha wanafuatilia ukandamizaji wa watu katika misingi ya rangi jinsia, ukanda, rika na itikadi, jambo alilodai limewashinda CCM.

“CCM leo kila wanaposimama wanaomba waendelee kuungwa mkono ili watawale…wameacha yale yaliyo katika katiba ya nchi na kusahau maandiko yaliyo nyuma ya ilani ya chama,” alisema.

No comments:

Post a Comment