To Chat with me click here

Wednesday, December 19, 2012

MAONI YA NDUGU MAXMILLIAN KATTIKIRO KUCHANGIA UTENGENEZWAJI WA KATIBA MPYA:



Ndg. Kattikiro katika moja ya harakati zake za kisiasa
Maxmillian Kattikiro Blog inapenda kuchukua nafasi hii kuwakumbusha wananchi wote kuwa, mwisho wa kutoa maoni juu ya katiba mpya umekaribia (20th December 2012), hivyo kila mtu anaalikwa kuendelea kutoa maoni yake juu ya katiba mpya, kwani ni haki ya kila mwananchi kushiriki/kushirikishwa katika mchakato mzima wa kuundwa kwa katiba mpya. 

Kama haukupata nafasi ya kutoa maoni juu ya katiba mpya wakati kamati ya kukusanya maoni ilipopita katika maeneo yako, Maxmillian Kattikiro Blog, tunakukumbusha kuwa bado unaweza kuendelea kutoa maoni kwa njia zifuatazo;- 

1. Kwa njia ya barua pepe (e-mail): katibu@katiba.go.tz 

2. Kwa barua za posta, kwa anuani ifuatayo: 
    S. L. P. 1681, Dar-Es-Salaam, Tanzania. 

3. Maoni katika tovuti ya kamati ya katiba mpya. Fuata link hii hapa ili kutoa maoni yako; 

Hakikisha unashiriki, ni haki ya kila mwananchi (wale waishio  nnchi/hata nchi za nje). Pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli, na maendeleo katika nchi yetu kwa kutoa michango mihimu ambayo itakuwa ni mwongozo wa uwajibikaji kwa wote walio na dhamana ya kuwatumikia wananchi.

Haya ni maoni yangu ambayo pia niliyatoa kwa njia ya Mtandao siku chache zilizopita:- 

1.   Nimeshauri kuwa Katiba ijayo ijaribu kupunguza mamlaka aliyopewa Rais, pamoja na shughuli zake. Mfano: Rais kuwa ni mwenye dhamana na kauli ya mwisho juu ya Ardhi pamoja na mambo mengine ambayo yangeweza kufanywa hata watendaji wa ngazi nyingine mfano mawaziri n.k

2.     Nimeshauri kuwa Katiba ijayo, ni lazima ieleze au itoe mamlaka kwa wananchi juu ya kuwawajibisha viongozi wa umma hususani wale waliowachagua kuwaongoza mfano: Wabunge. Naamini wazi kuwa kama wananchi watakuwa na mamlaka hayo, basi utendaji na uwajibikaji wao kwa wananchi utakuwa ni wa tija kwakuwa watakuwa moja kwa moja wanawajibishwa na wananchi wenyewe. Hili litachochea kasi ya maendeleo na kupunguza mzigo wa watumishi wazembe ambao si watendaji wanosubiri posho ambazo ni pesa za walipa kodi wa Taifa hili.

3.     Nimeshauri pia, Katiba ijayo ihakikishe kuwa Kinga ya Rais kushitakiwa inaondolea. Kwa kumwekea Rais kinga ya kumshtaki hata baada ya kuondoka madarakani kumekuwa kunaliumiza Taifa letu, kwani tumeona jinsi baadhi ya marais wetu wastaafu jinsi walivyoweza kujilimbikizia na kujimilikisha mali za umma, tumeona pia jinsi walivyoliingizia taifa hasara kwa kubariki na kukubaliana na mikataba ya “KISANII” ambayo imeligharimu taifa letu mno. Na haya yote ni kwa sababu huamini kuwa hakuna madhara watakayoyapata baada ya kumaliza vipindi vyao vya utawala. Lakini kwa nchi change kama Tanzania tunapaswa kutokubaliana wala kuunga mkono swala hili la kinga kwani tumeona kwa baadhi ya nchi nyingine za kiafrika zilivyoweza kuwaburuza marais wao mahakamani kwa tuhuma za ufisadi, ubadhilifu, matumizi mabaya ya ofisi za umma n.k

4.     Ardhi: Kwa mujibu wa katiba ardhi ni mali ya wananchi, na ndiyo maana hata ikitokea serikali au mwekezaji anahitaji sehemu ya ardhi ya wananchi Fulani huwapa fidia. Hivyo katiba mpya inapaswa kuonesha na kuzingatia hilo kuwa ardhi ni milki halali ya wananchi na ikiwa wananyang’anywa au kuondolewa katika ardhi hiyo basi wanapaswa kutendewa nini kama fidia. Hili litazuia unyanyaswaji wa wananchi ambao umekuwa ukiendelea nchini kwa baadhi ya matajiri kujiamuli kujitwalia ardhi ya wananchi huku wakikingiwa kifua na viongozi wa umma kwa dhana ya uwekezaji. Sheria ya ardhi lazima irekebishwe na itoe mamlaka na vipaumbele kwa wazawa na wageni kama ilivyo sasa.

5.     Matumizi mabaya ya ofisi za umma (Madaraka) pamoja na ubadhilifu ma rasilimali za Taifa: Katiba ijayo ni vyema ikaeleza wazi juu adhabu ya matumizi machafu ya ofisi za walipa kodi na rasilimali zetu tulizonazo. Tungependa kuona hawa wanaopewa mamlaka kuongoza au kusimamia rasilimali za taifa wanafanya hivyo tena kwa moyo wa uzalendo kwa manufaa ya Taifa zima na vizazi vyetu vijavyo na sisi wao na familia zao pekee. Rasilimali zetu zimekuwa zikimilikishwa kwa wageni wachache, na kuibwa huku watanzania tukiendelea kuwa maskini siku hadi siku, hii yote ni kwakuwa hakuna sheria iliyowazi na inayosimamia moja kwa moja rasilimali hizi na mamlaka ya watawala wetu.

6.     Umri wa kugombea nafasi ya Urais: Katiba ijayo ni vyema ikashusha kiwango cha umri unaoruhusiwa kwa mtu kugombea urais, nimependekeza iwe ni kuanzia miaka 35 na kuendelea. Kwani naamini kabisa kuwa vijana wa sasa wanauwezo na mitazamo chanya inayoendana zaidi na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia kuliko ilivyo kwa watu wa umri mkubwa zaidi. Naamini kuwa tunaweza kukwamuka toka kwenye umaskini huu uliokithiri kama tu, tutaweza kubadili mfumo wa uongozi uliopo madarakani na unoendesha nchi yetu kwa sasa. Hili limeonekana kushindikana na wazee waliowengi hususani walio madarakani, kwani wao pia wamekuwa ni sehemu ya huo mfumo kwa kipindi kirefu sasa.

7.     Muda wa utumishi wa Wabunge: nimependekeza kuwa kuwe na ukomo wa utumishi bungeni kama vile ilivyo kwa rais, lakini tofauti hapa ni hivi, wabunge wakae madarakani kwa muda wa miaka kumi tu kisha baada ya hapo wasiruhusiwe kugombea jimbo hilo hilo kwa mara nyingine. Wataruhusiwa kugombea ubunge kwa kupitia jimbo lingine tu. Kwanini hivi: ikiwa mbunge atakuwa amefanya mazuri kwa jimbo lake ndani ya miaka 10 basi yeye anaweza kukubalika kwingine kokote kwani atakuwa anaaminika kwa uchapa kazi wake. Lakini kama si mchapa kazi basi haina sababu ya kuendelea kuwa naye kwani ni mzigo na namna hii ya wabunge wamekuwa wakitumia pesa za walipa kodi pasipo manufaa yeyote kwa wananchi. Hivyo hawatastahili kurushwa bungeni baada ya miaka hiyo 10. 

Kumbuka, kila mmoja ana haki ya kutoa maoni yake binafsi bila kushinikizwa, hivyo haya ni maoni yangu binafsi ambayo nimeyatoa kwa utashi wangu timamu bila shinikizo toka kwa mtu, taasisi, wala kikundi fulani cha watu. Naamini yataheshimiwa na kuzingatiwa kama moja ya mochango muhimu ili kufikia malengo na mategemeo ya watanzania katika kupata katiba mpya.

No comments:

Post a Comment