To Chat with me click here

Wednesday, December 19, 2012

CHADEMA: 2013 NI MWAKA WA NGUVU YA UMMA



CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetangaza mkakati mzito kwamba mwaka 2013 utakuwa ni wa kuunganisha nguvu ya umma kitaifa, kuishinikiza serikali ya Rais Jakaya Kikwete kutoa tamko juu ya kuundwa tume huru ya kimahakama, itakayochunguza ya mauaji mbalimbali ya utatanishi yaliyotokea nchini katika kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja uliopita.

Mbali na kuunganisha nguvu ya umma, chama hicho pia kimeazimia kuitumia kambi rasmi ya upinzani bungeni kutumia njia za Kibunge kupitia hoja binafsi au muswada binafsi kuwasilisha bungeni mapendekezo ya marekebisho ya Katiba ya mpito kuhakikisha Tume Huru ya Uchaguzi na marekebisho ya sheria zinazosimamia uchaguzi, yanafanyika kabla ya Katiba Mpya.

Tamko la maazimio hayo yalitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe, wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya maazimio ya mkutano wa Kamati Kuu ya chama hicho, uliofanyika Desemba 15-16 mwaka huu, jijini Dar es Salaam.

Katika maazimio hayo yapatayo 10, Mbowe alisema baada ya chama hicho kumuandikia Rais Jakaya Kikwete barua ya kutaka tume huru ya kimahakama juu ya mauaji yenye utata, ikiwamo la kuuawa kwa mwandisahi wa habari wa Kituo cha Chanel Ten, Daudi Mwangosi, Ikulu haikutoa jibu lolote la kuwafahamisha wananchi nini kinaendelea.

“Mtakumbuka 9/9 mwaka huu tulimuandikia Rais Kikwete barua tukimtaka aunde tume huru ya kimahakama na hata tulipokutana naye, tulimuelezea umuhimu wa suala hili na akaahidi kushughulikia lakini hadi leo kimya sasa tutalirudisha suala hili kwa wananchi,” alisema Mbowe.

Alisema kuanzia Januari mwakani kutakuwa na mipango mipya ya kisiasa ambayo ni kuhamasisha umma kuishinikiza serikali kuchukua hatua katika masuala ya msingi.

Kuhusu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Mbowe alisema iliyopo haifanyi kazi kwa maslahi ya wananchi bali kwa ajili ya chama tawala huku akitolea mfano wa kushindwa kuitishwa kwa uchaguzi wa madiwani wa kata 13 kwa muda wa miaka miwili licha ya maeneo hayo kuwa wazi na sheria inaeleza kuwa siku 90 zikifika, lazima uchaguzi uitishwe katika maeneo yaliyokosa viongozi kwa sababu mbalimbali.
Aliongeza kuwa katika maeneo ambayo CCM ina kila sababu za kushindwa, NEC imekuwa ikibeba jukumu la kuokoa jahazi kwa kuacha kuitisha uchaguzi na kuwafanya wananchi kukosa wawakilishi.

Alisema kutokana na hali hiyo, CHADEMA haitaibembeleza serikali kuwajibika bali watawafahamisha wananchi umuhimu wa kuheshimiwa na kupewa uhuru wa kuchagua na kuchaguliwa bila kuingiliwa na Tume ya Uchaguzi.

“Tume itaarifiwa juu ya kucheleweshwa kwa chaguzi za marudio za udiwani, mitaa, vijiji na vitongoji katika maeneo mbali mbali, sisi CHADEMA tumeazimia kuunganisha nguvu ya umma kufanya shinikizo la kisiasa kwa mamlaka zinazohusika kutangaza nafasi kuwa wazi ili wananchi waweze kupata wawakilishi kwa wakati,” aliongeza Mbowe.

Kuhusu uboreshwaji wa daftari la wapiga kura, Mbowe alisema Kamati Kuu imezingatia hatua ya serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kukwepa wajibu wa kuboresha daftari hilo hivyo kuwanyima wananchi haki ya kuchagua na kuchaguliwa katika marudio ya uchaguzi zinazofanyika katika maeneo mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo Mbowe aliongeza kuwa Kamati Kuu (CC) imeazimia kambi rasmi ya upinzani bungeni inayoongozwa na CHADEMA ichukue hatua za kibunge kuhakikisha daftari hilo linaboreshwa mwaka 2013 kwa kile alichoeleza kuwa mwaka 2013 daftari hilo litatumika kwenye kura za maoni ya Katiba mpya.

Akizungumzia mchakato wa upatikanaji Katiba mpya mwaka 2014, Mbowe alisema Kamati Kuu imebaini upungufu katika mchakato mzima unaoendelea ya kukusanya maoni, hali aliyoelezea kuwa inaweza kukwamisha upatikanaji wa Katiba mpya bora mwaka 2014 kama ilivyotangazwa na serikali na tume husika.

Alisema wameazimia kwamba kamati ndogo ya Kamati Kuu ikutane haraka na kufanya tathmini zaidi na kutoa taarifa kwa umma na pia ipendekeze kwenye tume maoni ya CHADEMA ya kuzingatiwa katika Katiba mpya.

“Katika hili hatutanii mpaka sasa hakuna chama kinachojua kitaingia katika uchaguzi wa mwaka 2014 wa serikali ya mitaa na ule wa mwaka 2015 tukiwa katika mfumo gani; ni wakati muafaka wa kujadili mustakabali wa taifa na tusifungwe na hoja kuwa mambo hayo yasubiri katiba mpya,” alisema Mbowe.

Alisema ni wakati wa kuwa na muafaka wa kitaifa juu ya mfumo ambao hata Katiba mpya itakuwa imeufuata na kutolea mfano tatizo la kuzuiwa mijadala inayoendelea visiwani Zanzibar.

Alisisitiza kuwa wakati huu wa kuisubiria Katiba mpya ni vema taifa likaangalia masuala mbali mbali yanayogusa maisha ya Watanzania kila siku ambayo hayahitaji kusubiri mchakato wa Katiba mpya.

Kuhusu hali ya kisiasa, Mbowe alisema Kamati Kuu ilitaarifiwa kuhusu hoja binafsi zilizowasilishwa na wabunge wa (CHADEMA) Halima Mdee (Kawe) juu ya ugawaji holela wa ardhi na Zitto Kabwe (Kigoma Kaskazini), kuhusu fedha zilizofichwa nje ya nchi pamoja na kusudio lililotolewa na Tundu Lissu (Singida Vijijni), kuhusu hoja ya uteuzi wenye kasoro wa baadhi ya majaji na kwamba wameazimia kambi rasmi iifuatilie kwa karibu serikali kuhusu hoja hizo.

Akizungumzia kile kinachodaiwa kuna mgogoro wa CHADEMA wilayani Karatu, Mbowe alisema baada ya kupokea taarifa ya kamati waliyounda kufuatilia na kuchunguza hali hiyo, wameamua kuisimamisha kamati nzima ya utendaji ya chama hicho katika wilaya hiyo na kuiweka wilaya hiyo chini ya uangalizi wa Kamati Kuu Taifa mpaka hatua zingine zitakapochukuliwa.

Kuhusu serikali ya Chama cha Mapinduzi kutekeleza sera za CHADEMA, Mbowe alisema Kamati Kuu imezingatia kuwa hatua hiyo ni uthibitisho wa ziada kuwa CHADEMA ina sera nzuri na kwamba propaganda za CCM haziwezi kufanikiwa.

Alisema kutokana na hali hiyo ni wazi serikali ya CCM haiwezi kuzitekeleza kwa ufanisi sera hizo na kwamba kuna haja ya CHADEMA kuongeza nguvu kwa ajili ya kuzisimamia sera zake kwa umakini itakaposhika madaraka ya kuongoza serikali za mitaa mwaka 2014 na Serikali Kuu 2015

No comments:

Post a Comment