To Chat with me click here

Monday, May 20, 2013

CCM INAGAWA USHINDI KWA CHADEMA!



Kitendo cha CCM yangu kukamata, kushikilia na kuachia viongozi waandamizi na hata Wabunge wa CHADEMA au kuwafunga midomo wahusika hao, ni kugawa bure Majimbo na ushindi mwingine hata kabla ya 2015 kwa chama hicho kikuu cha upinzani nchini. Kiukweli, mbinu ya kutumia Jeshi la Polisi kutekeleza maagizo ya chama na Serikali hata bila ya kufikiri vyema ni kukiangamiza chama chetu cha Mapinduzi.

Amini nawaambia, viongozi wote waandamizi wa CHADEMA pamojana Wabunge wao waliowahi na wanaoendelea kupata kashkash za Polisi au Dola, wameshakabidhiwa majimbo na ushindi mwingine. Wananchi kwasasa ni wapole mno. Hawana nguvu yoyote kama silaha yao. Lakini,itakapofika 2015, mambo yatakuwa tofauti. Wananchi watakuwa wafalme kupitia kura zao. Na hawa wa kizazi hiki, hawataibiwa kura zao. 2015 ni mwaka tofauti, na uchaguzi tofauti. Dalili za kuzidi ugonjwa zitaanza 2014 kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Nakishauri chama changu kuachana na siasa chafu za kutumiaJeshi la Polisi na vyombo vingine vya Dola. Kwakuwa CCM ni chama cha siasa, ni muda sasa wa kufanya siasa. Kadiri ya uelewa wangu, siasa ni hoja za ubunifu na utekelezaji ili kupeleka mambo ya kimaendeleo mbele. Siasa si mabavu, kejeli, matusi, vitisho wala vita!

Kama chama tawala, CCM kina mambo mengi ya kufanya: kuitekeleza Ilani ya mwaka 2010-2015. Sehemu kubwa ya Ilani bado haikutekelezwa. Ilani itatekelezwaje kwa kila siku kukamata, kupiga mabomu, kushtaki na kutisha viongozi wa kisiasa NA WANANCHI KWA UJUMLA nchini? Haiwezekani, lazima CCM ibadilike. Ikinipuuza, italia na kusaga meno 2015.

Mzee Tupatupa wa Lumumba, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment