To Chat with me click here

Wednesday, January 2, 2013

IDADI YA WATANZANIA YAONGEZEKA KWA ZAIDI YA MILIONI 10 KWA MUONGO MMOJA


Idadi ya Watanzania imechupa kutoka milioni 34.4 mwaka 2002 hadi takriban milioni 45 mwaka 2012, alitangaza Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete hapo Jumatatu (tarehe 31 Disemba).

Matokeo ya sensa ya watu na makaazi ya mwaka 2012, iliyoanza mwezi Agosti, yalionesha kwamba kuna watu 44,929,002 nchini Tanzania, alisema Kikwete kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja mjini Dar es Salaam.

Baada ya kutangaza matokeo hayo, Rais Kikwete aliwatolea wito Watanzania kuzingatia uzazi wa mpango kwani kasi ya ukuwaji wa idadi ya watu ni kubwa mno kwa uchumi wa nchi kuweza kuikimu.

“Kiwango cha uzazi ni 2.6, lakini ndani ya miaka kumi tu idadi ya watu imeongezeka kwa milioni 10.5,” alisema Kikwete. “Tunapaswa kuzingatia uzazi wa mpango, vyenginevyo naweza kuona hatari inayolinyemelea taifa letu.”

Alisema utabiri unaonesha kwamba mwaka 2016 Tanzania itakuwa na watu milioni 51. Serikali inapaswa kuirekebisha mipango yake na kutenga fedha, alisema, kwa sababu asilimia 63 ya watu wako chini ya miaka 30, jambo linalomaanisha kwamba kutahitajika shule zaidi, hospitali zaidi na huduma ziada nyengine kwa kizazi kijaacho.

Waziri wa Fedha William Mgimwa alisema kwamba matokeo hayo ya sensa yatachapishwa kitaifa na kutumwa kwenye mitandao ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Kiuchumi ya Kusini mwa Afrika na Kitengo cha Takwimu cha Umoja wa Mataifa.

Serikali ilitumia jumla ya shilingi bilioni 140 (dola milioni 88.5) kufanya sensa hiyo, ambayo ni ya tano tangu uhuru mwaka 1961. Sensa nyengine itafanyika mwaka 2022.

No comments:

Post a Comment