To Chat with me click here

Wednesday, January 2, 2013

GONGO LA MBOTO WAMKABA KOO JERRY SILAA


WANACHAMA wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kata ya Gongo la Mboto Dar es Salaam, wamemtaka diwani wa kata hiyo ambaye pia ni Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa, kutoa ufafanuzi kuhusu kiasi cha sh milioni 100 kilichotengwa kwa ajili ya matengezo ya barabara katika bajeti ya 2011/2012.

Akizungumza juzi kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na wanachama hao, Katibu wa Jimbo la Ukonga, Juma Mwaipopo, alieleza kuwa fedha hizo zilitengwa na Halmashauri ya Ilala katika kipindi hicho ambazo hadi sasa hazijafahamika zilikokwenda.

Alifafanua kuwa katika bajeti hiyo halmashauri ilitenga sh bilioni 93 kwa matumizi ya jimbo hilo, zikiwemo sh milioni 100 kwa kata sita zilizo Gongo la Mboto ambazo zingetumika kwa ajili ya upanuzi na matengenezo ya barabara pamoja na kusambaza huduma ya maji kwa wananchi, jambo ambalo hadi sasa ni kitendawili.

Alisema bado tatizo la huduma ya maji safi katika kata hiyo ni kitendawili ambacho kimeshindikana kupatiwa ufumbuzi na serikali.

“Tunahitaji kuwa na maamuzi ya pamoja juu ya Silaa, kwa sababu hatujui tumetoka wala tunaelekea wapi hadi sasa? Inawezekana hajui kazi yake kwa sababu hatuna maendeleo wala mabadiliko katika kata yetu, Watanzania tudai haki ambazo serikali ilituahidi itazitekeleza bure,” alisema Mwaipopo.

Naye Mbunge wa Jimbo la Nyamagana (CHADEMA), Ezekia Wenje, alitumia fursa hiyo kueleza kuwa diwani huyo ameshindwa kutekeleza majukumu yake hasa kwa kushindwa kukutana na wananchi wake walau kwa mwaka mara moja ili kutoa ufafanuzi juu ya mapato na matumizi ya fedha yanavyotumika.

Alipopigiwa simu kujibu tuhuma hizo diwani huyo alikata na kutuma ujumbe mfupi wa maneno: “Niko sehemu tata; naomba unitumie ujumbe wa maneno (sms).”

No comments:

Post a Comment