To Chat with me click here

Wednesday, January 9, 2013

MAPATO YAPANDA KATIKA BANDARI YA DAR ES SALAAM KUFUATIA KUSIMAMISHWA KWA MUDA



Meli zinapakua makontena katika bandari ya Dar es Salaam tarehe 29 Disemba, 2012.
Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imeongeza ukusanyaji wa mapato katika bandari ya Dar es Salaam kutoka shilingi bilioni 28 mwezi Novemba hadi shilingi bilioni 50 (dola milioni 18 hadi dola milioni 31) katika mwezi wa Disemba, kufuatia kusimamishwa kwa muda maofisa 16 wa bandari wanaotuhumiwa kwa mwenendo usiofaa.

Maofisa hao wa bandari, wakiwemo wakurugenzi wa ngazi za juu, walisimamishwa kwa muda mwezi Disemba baada ya Wizara ya Usafirishaji kuanzisha uchunguzi wa ndani kwa lengo la kutoa mwitikio wa malalamiko ya wateja kuhusu kucheleweshwa katika bandari hiyo, kwa mujibu wa Waziri wa Usafirishaji Harrison Mwakyembe.

Maofisa wa bandari wengine wasiopungua sita walisimamishwa mwezi Agosti. Uchunguzi huo, ambao bado unaendelea, uligundua kuwa waajiriwa wa bandari walibadilisha mwelekeo wa biashara kutoka katika bandari kwenda kwa kampuni ndogo za usafirishaji na utoaji mizigo wanazomiliki, ukiukaji wa moja kwa moja wa mkataba wao wa ajira.

"Wateja wanakimbia bandari yetu kwa sababu ya ucheleshaji wa kukusudia unaofanywa na waajiriwa wasio na maadili ambao wanaongeza gharama za kufanya biashara," Mwakyembe aliiambia Sabahi. "Hii ni kinyume na mikataba yao ya ajira na wana mgongano wa maslahi na mwajiri wao [serikali]."

Miongoni mwa viongozi wa bandari wa ngazi ya juu waliosimamishwa ni Mkurugenzi Mkuu wa TPA Ephraim Mgawe, Mkurugenzi wa Mipango Florence Nkya, Mkurugenzi wa Uhandisi Bakari Kilo, Mkurugenzi wa Mifumo ya Utawala Maimuna Mrisho, Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Ayub Kamili, Kaimu Mkurugenzi Mkuu Hamad Koshyuma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu Julius Fuko, na Meneja wa Bandari Cassian Ng'amilo.

Mashtaka rasmi bado hayajatolewa dhidi ya viongozi waliosimamishwa na bado hawajajibu tuhuma zozote hadharani. Mwakyembe alisema Bodi ya Wakurugenzi ya TPA itakutana hivi karibuni kutoa uamuzi wa mwisho kuhusiana na ajira yao.

Kwa kawaida, makampuni ya kupokea na kusafirisha mizigo hutoza shilingi 640,000 (dola 400) kuondoa kontena lenye futi 20 hadi 40 kutoka bandarini ndani ya siku saba. Makontena ambayo hayajalipiwa ndani ya muda huo uliyotengwa hutozwa fedha za ziada. 

Mwakyembe alisema wateja wanalalamika kwamba kulipia na kutoa kontena katika bandari ya Dar es Salaam kumekuwa kukichukua hadi wiki nane, wakati inachukua siku saba tu katika bandari ya Mombasa nchini Kenya.

Wateja wanataka bidhaa kuondolewa bandarini katika kipindi kifupi kadri iwezekanavyo, Mwakyembe alisema, na pale ambapo kuna ucheleweshaji bandari ya Dar es Salaam, wanahamishia mizigo yao katika bandari nyingine, ambako kunasababisha serikali ya Tanzania kupoteza mapato.

Mwakyembe alisema makampuni binafsi yanayomilikiwa na viongozi tangu wakati huo yamesimamishwa na biashara imerejea bandarini, na kuchangia ongezeko la mapato ya Disemba.

Makampuni ya kuagiza na kusafirisha bidhaa nje yakaribisha marekebisho

Vincent Nyerere, anayemiliki kampuni ya kuagiza bidhaa, alikubaliana na kusimamishwa kwa viongozi wa bandari, lakini alisema bado jitihada zaidi zinatakiwa ili kuboresha biashara bandarini, kwa kuwa bado inaenda taratibu.
Alisema aliagiza makontena manne kutoka China mwezi Novemba -- mawili yaliingizwa kupitia bandari ya Mombasa na mawili kupitia Dar es Salaam. Makontena yaliyopitia Mombasa yaliondolewa ndani ya siku tisa, wakati yale yaliyopitia Dar es Salaam yaliendelea kukwama katika bandari ya Dar es Salaam hadi tarehe 7 Januari.

"Lengo langu lilikuwa ni kuuza bidhaa katika wiki la kati ya Krismasi na mwaka mpya lakini sasa kama nikipata bidhaa hizo zote nitazifanyia nini?" aliiambia Sabahi. "Bandari [ya Dar es Salaam] imeua kabisa biashara yangu."

Nyerere alisema kama bandari ingekuwa na utaratibu mzuri na kufanya kazi kwa ufanisi, ingeweza kuzalisha hadi shilingi bilioni 100 (dola milioni 63) kwa mapato ya mwezi.

Haron Ishimwabula, ambaye kampuni yake ya usafirishaji nje na uingizaji wa bidhaa inahudumia Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Malawi na Zambia, alisema kwamba kwa sababu ya kutofanya kazi kwa ufanisi katika bandari ya Dar es Salaam, anatumia bandari ya Mombasa ili kuingizia bidhaa kwa haraka hata kama inaongeza gharama katika biashara yake.

Mchumi Benson Mahenya, mkurugenzi wa Andrew's Consulting Group, alisema serikali inapoteza mapato mengi sana kwa bandari shindani katika nchi za eneo hili. Kwa kuwa ni eneo la kimkakati, bandari inaweza kuzalisha hadi asilimia 60 katika bajeti ya taifa, aliiambia Sabahi, lakini kwa sababu ya kutokuweko kwa ufanisi mapato yanayotarajiwa kupatikana hayafikiwi.

Mahenya alipongeza jitihada za Mwakyembe kuboresha utendaji wa bandari na kuwaomba kila mmoja kuunga mkono mabadiliko yanayokusudia kuondoa ufisadi.

Hata hivyo, alisema mfumo wa uchukuzi katika bandari pia unahitaji maboresho. Kwa mfano, badala ya kutumia magari makubwa ya mizigo, mfumo wa reli unapaswa kuhuishwa kwa ajili ya shehena kubwa na usafirishaji wa haraka wa bidhaa kutoka bandarini, alisema Mahenya.

Mwakyembe alisema maboresho ya utendaji bandarini ni endelevu na wizara yake itaendelea kukagua njia za kuboresha ufanisi. Alisema wizara hiyo inazingatia kufanya kazi katika bandari kwa saa 24 ili kuondoa shehena ya kontena ambazo zinatakiwa kutolewa.

No comments:

Post a Comment