To Chat with me click here

Thursday, January 31, 2013

MAKINDA AMPONGEZA LEMA


SPIKA wa Bunge Anna Makinda, amempongeza Mbunge wa Arusha Mjini, Goodbless Lema (CHADEMA) kwa kurejea bungeni.

Spika alitoa pongezi hizo jana ndani ya Ukumbi wa Bunge baada ya kumuona mbunge huyo akiingia ukumbini na kuketi kwenye kiti chake.
“Naona Mheshimiwa Lema anaingia. Nachukua nafasi kukupongeza kwa kurudi bungeni. Karibu sana,” alisema spika huku wabunge wengine wakishangilia kwa kupiga makofi.

Lema, mmoja wa wabunge machachari wa CHADEMA, alikuwa nje ya Bunge kwa takribani miezi kumi baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha kumvua ubunge.

Kesi dhidi yake ilifunguliwa na wanachama sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambao pamoja na mambo mengine walidai Lema alimkashifu mgombea wao, DkBatilda Burian.

Hata hivyo, Lema alikata rufaa na kurejeshewa ubunge wake Desemba mwaka jana.

Tayari Lema ameahidi kufufua hoja zote alizoziacha bungeni, ikiwemo hoja kwamba Waziri Mkuu alilidanganya Bunge.

TUME YA KATIBA YAKAMILISHA KUPOKEA MAONI MAKUNDI MAALUM


Tume ya Mabadiliko ya Katiba imefunga rasmi kupokea maoni ya uundwaji wa katiba mpya kutoka kwa makundi, taasisi na watu wenye hadhi ya kitaasisi.

Mwenyekiti wa Tume hiyo, Waziri Mkuu mstaafu Jaji Joseph Warioba, alipozungumza na NIPASHE.

“Upokeaji wa maoni kwa njia nyingine bado unaendelea, isipokuwa tumefunga kupokea maoni kutoka kwa watu,” alisema Jaji Warioba.

Tume hiyo iliapishwa na Rais Jakaya Kikwete Aprili 13, mwaka jana na kuanza kazi ya kukusanya maoni  Julai 2, mwaka jana, baada ya kujigawa katika makundi saba.

Tume hiyo Ilipewa muda wa miezi 18 kufanya kazi hiyo hadi Aprili 26, mwaka 2014.

Tume ilijipangia kufanya kazi yake kwa awamu mbili tofauti; awamu ya kwanza ikiwa ni kukusanya na kuratibu maoni ya wananchi na awamu ya pili itakuwa ni kuandaa taarifa, mapendekezo na rasimu ya Katiba Mpya.

Baadaye Tume itakutana na Mabaraza ya Katiba,  na mwishowe rasimu ya katiba itafikishwa kwenye Bunge Maalum litakalowakilishwa na makundi mbalimbali katika jamii.

Baada ya hapo itaitishwa kura ya maoni, ambayo itatoa fursa kwa wananchi kuamua kama wanairidhia rasimu ya katiba hiyo au la.

Tume hiyo ina wajumbe 32 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, wakiongozwa na Jaji Warioba (Mwenyekiti) na Jaji Mkuu mstaafu, Augustino Ramadhani (Makamu Mwenyekiti).

CHANZO: NIPASHE

ZITTO: CCM INATUCHONGANISHA



NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Zitto Kabwe, amekishutumu Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba kinachonganisha viongozi wa chama chake kwa lengo la kukidhoofisha wakati huu kinapoelekea kushika dola mwaka 2015.

Zitto alisema hayo jana alipokuwa anazungumza na viongozi wa CHADEMA wa matawi na kata zote kutoka Jimbo la Kigoma Kaskazini ukiwa ni mkakati wake wa kuendelea kukijenga chama na kujua matatizo ya kisiasa na kijamii yanayowakabili wananchi wake.

Mbunge huyo ambaye ameamua kupiga kambi jimboni humo kwa lengo la kuwazuia CCM wasipotoshe wananchi wake wakati huu wanapoadhimisha miaka 36 ya kuzaliwa chama chao, alisema kuwa licha ya maneno na uvumi kuzagaa kwamba CHADEMA Taifa inakabiliwa na mgogoro baina ya viongozi, jambo hilo si kweli.

Zitto alibainisha kuwa hali hiyo inakuzwa na watu waliopandikizwa na kutumiwa na CCM kwa ajili ya kuleta mpasuko na kukigawa chama ili kupunguza kasi yake ya kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

“CHADEMA hakuna mpasuko wala migogoro kama inavyotafsiriwa na wengi, badala yake kuna kakundi kanataka kutuhujumu kwa kutugawa kwa kutumia itikadi za kidini, kimaeneo, kimitazamo na hata kiitikadi kama walivyotumwa na hicho chama chao.

“Ninachoweza kusema ni kwamba ndani ya chama chetu kuna majungu, fitina, kuoneana wivu, usaliti na hata kumalizana kisiasa, haya tutahakikisha tunayamaliza kikatiba kwa sababu hiyo ndiyo sheria mama inayotuongoza ili tufikie malengo tuliyojiwekea,” aliongeza Zitto.

Alidai kuwa wajibu wake ni kupigania misingi ya uwajibikaji na demokrasia ndani ya CHADEMA ili kuondokana na vitendo vya uongozi wa kutumia mabavu kama ilivyo kwa CCM, ambayo imekuwa ikitumia nguvu katika kuendesha mambo yake, sambamba na serikali iliyopo madarakani.

Hata hivyo, aliwashutumu viongozi wa jimbo lake kwa kushindwa kuwajibika ipasavyo katika kujenga chama na badala yake kila kitu kumtegemea yeye kama mbunge ikiwa ni pamoja na vikao na mikutano ya hadhara.

“Ili tujenge chama chenye nguvu na heshima, ni lazima viongozi wote tushirikiane kuanzia ngazi ya matawi, kata na jimbo badala ya kila kitu kunitegemea mimi mbunge, lazima tuweke misingi imara ya chama ili mgombea ajaye wa CHADEMA asipate wakati mgumu wa kufanya kampeni,” alisisitiza.

Zitto aliongeza kuwa, wakazi wa Kigoma kwa miaka mingi wamekuwa hawana mtetezi katika ngazi za kitaifa, kiasi kwamba hoja za kuendeleza mkoa kwa kupatiwa miradi ya maendeleo zinapata upinzani mkubwa kwenye vikao vya uamuzi kama vile Baraza la Mawaziri na Bunge.

“Lazima sisi watu wa Kigoma tuwe na umoja kwa sababu tumekuwa wanyonge kwa miaka mingi, na daima nguvu ya wanyonge ni umoja baina yaoNa sisi tunapaswa kuwa na umoja kwa ajili ya maendeleo ya mkoa wetu na hata hii miradi inayoletwa Kigoma sasa ni kutokana na kelele tunazopiga,” alisema.

Aliongeza kuwa hata kama hatagombea nafasi yoyote ndani ya chama, bado ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu na ataitumikia CHADEMA kwa vile misingi aliyoshiriki kuitengeneza kwa ajili ya ustawi wa chama hicho bado haijakamilika na hawezi kuiacha ikiwa hivyo.

KANDA 10 ZA KIUTENDAJI ZA CHADEMA

1.             Kanda ya Ziwa Magharibi
Mwanza
Geita
Kagera

2.           Kanda ya Ziwa Mashariki
Mara
Simiyu
Shinyanga

3.           Kanda ya Ziwa Tanganyika
Kigoma
Tabora
Katavi
Rukwa

4.           Kanda ya Kati
Singida
Dodoma
Morogoro

5.           Nyanda za Juu Kusini
Mbeya
Ruvuma
Iringa
Njombe

6.           Kanda ya Kusini
Lindi
Mtwara

7.           Kanda ya Mashariki
Pwani
Dar es Salaam

8.           Kanda ya Kaskazini
Kilimanjaro
Manyara
Arusha
Tanga

9.           Kanda ya Pemba
(Mikoa yote ya Pemba)

10.    Kanda ya Unguja
(Mikoa yote ya Unguja)