To Chat with me click here

Monday, February 4, 2013

HOJA YA MBUNGE MWINGINE KUTIKISA BUNGE TENA LEO



Mkutano wa 10 wa Bunge unaendelea leo mjini Dodoma baada ya mapumziko ya mwisho wa wiki na leo itakuwa zamu ya Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, kuwasilisha hoja binafsi kuhusu hatua za uboreshaji wa upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es Salaam.

Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya vikao vya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinaeleza kwamba hoja ya Mnyika itakabiliwa na upinzani mkubwa kutoka kwa wabunge hao kwa madai kwamba siyo Jiji la Dar es Salaam pekee lenye tatizo la maji.

Taarifa zaidi zinaeleza kwamba wabunge hao wamejipanga kuizuia hoja hiyo kama walivyofanya hoja ya Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia, ambayo ilikuwa ikizungumzia udhaifu ulipo katika sekta ya elimu hasa kutokuwapo kwa mitaala rasmi ya shule za msingi na sekondari.

Wabunge hao wamejipanga kuilazimisha serikali iangalie kwanza tatizo la maji vijijini badala ya Jiji la Dar es Salaam kama Mnyika anavyopendekeza.

Akizungumza na NIPASHE jana, Mnyika alisema Ijumaa aliwasilisha kwa Katibu wa Bunge mapendekezo ya kuboresha na kupanua wigo wa hoja yake pamoja na hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji jijini Dar es Salaam.

Alisema katika mapendekezo hayo, hoja yake imejielekeza katika  kuboresha utekelezaji wa miradi ya maji nchi nzima kwa kuingiza masuala muhimu kuhusu Programu ya Maji Safi na Mazingira Vijijini (RWSSP) maarufu kama mradi wa vijiji kumi ambao unatekelezwa katika Halmashauri za Dar es Salaam na wilaya zote nchini.

“Nimeeleza kuwa Programu ya Maji Safi na Mazingira Vijijini ikiwamo katika Manispaa za Jiji la Dar es Salaam ilipaswa kutekelezwa kuanzia mwaka 2005/2006 na kukamilika mwaka 2010/2011 kwa kugharimu dola za Marekani milioni 292 (zaidi ya Sh. bilioni 438).  Hata hivyo, tathmini ya miaka miwili na nusu ya utekelezaji imebainisha kasoro nyingi katika utekelezaji,” alisema.

Alisema: “Nitawasilisha bungeni hatua zipi za haraka ambazo napendekeza zichukuliwe ikiwamo kuhusu ufisadi katika sekta ya maji kwenye Jiji la Dar es Salaam na nchini kwa ujumla.”

Alisema mabadiliko aliyofanya yanalenga pamoja na mambo mengine, kuifanya iguse matukio ya karibuni kuhusu tatizo la maji nchini.

Kabla ya Mnyika kuwasilisha hoja yake, wabunge wataendelea na mjadala wa hoja ya Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Hamis Kigwangalla, ya kuitaka serikali ianzishe mfuko maalum wa kukuza ajira kwa vijana kwa kuanzisha mfuko wa mikopo wa vyama vinavyowekeza katika kilimo na viwanda vyenye uhusiano wa moja kwa moja na kilimo.

Hoja ya Kigwangalla iliwasilishwa bungeni Ijumaa iliyopita na kujadiliwa na baadhi ya wabunge, lakini leo wengine zaidi watapata nafasi ya kuchangia kabla ya mbunge huyo kupewa nafasi ya kuhitimisha.

Hoja ya Mnyika ambayo itafuatiwa na ya Mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari, ambaye kesho atawasilisha hoja binafsi kuhusu mwenendo wa Baraza la Mitihani la Taifa unavyoathiri elimu nchini.

Mbali ya hoja hizo, Bunge pia litajadili maazimio ya mikataba mbalimbali ya Kimataifa pamoja na miswada ya sheria itakayowasilishwa na serikali.

Hoja ya Mnyika huenda ikageuzwa kama ilivyofanywa na Mbatia baada ya wabunge wa CCM kutoiunga mkono. Hatari ya hoja kutoungwa mkono na wabunge wa CCM ni kura za ndiyo na siyo ambazo zinakwamisha hoja hata kama zina nguvu.

Katika hoja yake, Mbatia aliliomba Bunge liunde Kamati Teule kuchunguza udhaifu uliopo kwenye sekta ya elimu hasa kutokuwepo kwa mitaala rasmi.

Hoja hiyo ilipingwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, ambaye alipinga kamati akieleza kwamba tayari serikali imechukua hatua nyingi za kuitekeleza elimu kwa kujenga madarasa mengi na idadi ya wanafunzi wanaojiunga elimu ya msingi na sekondari imekuwa ikiongezeka kila mwaka.
Waziri Kawambwa aliahidi kwamba atawasilisha miswada hiyo bungeni Februari 6, kabla Mkutano huu haujamalizika.

Baadhi ya wabunge waliochangia hoja ya Dk. Kigwangalla wameonyesha wasiwasi wa zitakakopatikana fedha za kuweka kwenye mfuko wa kukopesha vijana na badala yake wamependekeza mfumo mzima wa elimu uboreshwe ili nchi izalishe wahitimu wanaoweza kujiajiri na kushindana kwenye soko la ajira.
Kwa mujibu wa ratiba, Mkutano wa Kumi wa Bunge unatarajiwa kuahirishwa Februari 8, mwaka huu.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment