To Chat with me click here

Friday, July 26, 2013

UTAFITI: SERA YA UWEKEZAJI MADINI HAINUFAISHI JAMII



Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Uhasibu Arusha na Mchumi, Balozi Morwa alitoa mapendekezo hayo juzi, wakati akiwasilisha utafiti kuhusu wajibu wa kampuni kwa jamii(CSR),uliofanyika katika machimbo ya Tanzanite Mirerani, wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara.

ARUSHA, Tanzania: 

Serikali imeshauriwa kubadili sera ya uwekezaji nchini kwa kulazimisha kisheria kampuni za wawekezaji hasa wa Sekta ya Madini, kutekeleza miradi ya jamii inayozunguka maeneo yao ya uchimbaji badala ya suala hilo kuwa ni la hiari.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Uhasibu Arusha na Mchumi, Balozi Morwa alitoa mapendekezo hayo juzi, wakati akiwasilisha utafiti kuhusu wajibu wa kampuni kwa jamii(CSR),uliofanyika katika machimbo ya Tanzanite Mirerani, wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara.

Morwa akiwasilisha utafiti huo ,ambao uliratibiwa na Mtandao wa Mashirika yasiyo ya kiserikali ya Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Finnish NGO Platform, alisema wamebaini kuwa jamii zinazozunguka migodi ya Tanzanite hazinufaiki ipasavyo.

Morwa alisema utafiti huo, ulihoji watu 350 na nyaraka kukusanywa,wamebaini,wajibu wa kampuni ya wawekezaji kwa jamii ukiwa wa kisheria kama Ghana, utawanufaisha na ikishindika ifutwe na kampuni hizo zilipe kodi kubwa kama nchi nyingine.

CHADEMA YAIKOROGA POLISI!



UAMUZI wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukataa kuwasilisha ushahidi wa mauji ya mlipuko wa bomu uliotokea jijini Arusha, umeliweka njia panda Jeshi la Polisi na hivyo kushindwa kuchukua hatua.

Licha ya jeshi hilo kumhoji Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, na kumtaka awasilishe ushahidi huo, kiongozi huyo amekataa agizo hilo akisema kuwa wamekubaliana kuutoa ushahidi huo kwa tume huru ya majaji endapo Rais Jakaya Kikwete ataiunda kama walivyomuomba.

Chanzo chetu ndani ya jeshi hilo, kimedokeza kuwa msimamo huo wa CHADEMA umeliweka njia panda na hivyo kushindwa kuchukua hatua za kuwabaini watuhumiwa wa tukio hilo na kuwafungulia mashtaka kutokana na mkanganyiko wa taarifa zinazotolewa.

Jeshi hilo linadaiwa kuwa awali lilitaka kujiegemeza kwenye kauli za kisiasa za baadhi ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na serikali ili kuonyesha kuwa CHADEMA ilisababisha mlipuko huo yenyewe kwa ajili ya kuwahadaa wafuasi na kujitafutia umaarufu.

Hata hivyo, mbinu hiyo ya kutaka kuwasakama baadhi ya viongozi na wafuasi wa CHADEMA inadaiwa kufifishwa na tamko la Mbowe pamoja na mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, kwamba chama kina ushahidi unaoonyesha kuwa tukio hilo lilifanywa na polisi.

“Hapa kuna mkanganyiko hasa baada ya Mbowe kudai wanao ushahidi wa video ya tukio hilo. Wakubwa wetu wamegawanyika na kujikuta wakitoa kauli za kukinzana maana wanahofia wakiwafungulia kesi watu wengine mashtaka halafu CHADEMA ikaonyesha ushahidi tofauti itakuwa ni aibu,” kilisema chanzo chetu.

Kwa mujibu wa chanzo hicho, jeshi hilo mkoani Arusha lilikuwa limewakamata watu wawili raia wa kigeni likiwatuhumu kuhusika na mlipuko huo lakini baada ya Mbowe kugoma kupeleka ushahidi huo, watuhumiwa hao hawakuweza kufunguliwa mashtaka.

Pia katika hali ya kushangaza Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari kuwa makachero wa Taasisi ya Uchunguzi ya Marekani (FBI) wamefika mkoani Arusha kuchunguza jambo hilo.

Hata hivyo taarifa kutoka ubalozi wa Marekani zilikana FBI kuingia nchini kuchunguza jambo hilo hivyo kusababisha mkanganyiko wa tukio hilo lililovuta hisia kubwa ndani na nje ya nchi.

CHADEMA mara kwa mara imekuwa ikilituhumu jeshi la polisi na makada wa CCM kuendesha harakati za kukidhoofisha kwa kutumia matukio mbalimbali yanayofanywa na chama hicho cha upinzani.

Mmoja wa viongozi wa CHADEMA aliviambia vyanzo vyetu vya habari, kuwa polisi walikuwa wamepanga kuwatumia FBI kuuhabarisha umma kuwa CHADEMA ilihusika na ulipuaji huo bomu lakini kutokana na mazingira yaliyopo wameshindwa kutekeleza uovu huo.

“Unajua hila za polisi na CCM kila siku zinabadilika lakini kwa bahati mbaya hawajui kuwa wananchi wanajua kinachofanyika, kuna askari hawaridhiki na uovu unaofanywa na wenzao,” alisema kiongozi huyo.

JK: TUTAMNYUKA ATAKAYETUCHEZEA!



RAIS Jakaya Kikwete amesema Serikali ya Tanzania iko tayari kukabiliana na mtu yeyote atakayejaribu kuichezea au kuichokoza kwa namna yoyote ile, ikiwamo kumega ardhi yake, itamfundisha kama ilivyomfundisha aliyekuwa Rais wa Uganda, Idd Amin Dada, katika Vita ya Kagera.

Kikwete alisema serikali ilimshikisha adabu Amin alipojaribu kumega sehemu ya ardhi ya Tanzania, hivyo haitosita kufanya hivyo tena kwa asiye na nia njema na Tanzania.

Kiongozi huyo mkuu wa nchi alitoa onyo hilo jana wakati akizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Mashujaa yaliyofanyika kitaifa katika makaburi yaliyopo Kambi ya Kaboya, wilayani Muleba, mkoani Kagera.

Rais Kikwete alisema serikali iko tayari kukabiliana na kupambana kwa nguvu yoyote ile bila kuogopa mtu anayejaribu kuichezea nchi ya Tanzania kwa lengo la kukwaza amani na utulivu uliopo hivi sasa.

“Laleni usingizi salama. Msisikilize maneno ya mitaani, kwa sababu jeshi letu liko imara kabisa kulinda nchi yetu na mipaka yake. Yeyote atakayejaribu kuivamia ama kuichokoza nchi yetu atakiona cha mtema kuni. Nchi iko salama na jeshi liko imara kulinda nchi yetu.

“Ujumbe wetu mkubwa wa leo ni kwamba tuko tayari wakati wote na saa yoyote kuilinda nchi yetu na mipaka yake. Hatuna nchi nyingine. Hivyo, kamwe hatuwezi kumruhusu yeyote kuichezea nchi yetu, ama kuichezea ama kuimega nchi hii. Kama tulivyoshughulika na Amin naye tutashughulika naye vivyo hivyo,” alisema.

Rais Kikwete alisema shughuli ya kulinda amani ni ghali. “Na moja ya gharama hizo ni makaburi haya ya ndugu zetu ambao wamelala hapa baada ya kupoteza maisha yao katika vita dhidi ya nduli Idi Amin. Tutaendelea kuwaenzi kwa sababu hawa walijitolea maisha yao kulinda mipaka ya nchi yetu, kulinda amani ya nchi yetu na usalama wake na wetu sote,” alisema Kikwete.

Kiasi cha askari 619 waliopoteza maisha yao wamelazwa kwenye makaburi hayo ya Kaboya.

Rais Kikwete amesema kuwa serikali yake kwa ushauri wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania inaangalia jinsi gani ya kuwahudumia vizuri zaidi askari wa Tanzania ambao walipata vilema katika vita hiyo na bado wanaendelea kuishi.

“Nimesikia kuna malalamiko kuhusu ubora wa jinsi tunavyowahudumia, hivyo tutazungumza na Jeshi kuhusu njia bora zaidi ya jinsi ya kuwahudumia. Hawa ni mashujaa wetu, ni watu waliojitolea maisha yao kuweza kulinda uhuru wetu. Tunaendelea kuwashukuru na kuwaenzi. Hii ndiyo sababu sherehe za leo ni sherehe kubwa kwa nchi yetu,” alisema.

Rais Kikwete alishuhudia sherehe za kumbukumbu hizo ambapo miongoni mwa mambo mengine, ametembelea makaburi ya askari wa Tanzania waliopoteza maisha yao wakati wa kuikomboa nchi kutokana na uvamizi wa Amin wa Uganda na kuona silaha zilizotumika katika vita hiyo mwaka 1978/79.
Naye Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania ( JWTZ ), Davis Mwamunyange, alisema jeshi lake liko makini na lina uwezo mkubwa wa kupambana dhidi ya wale wanaotaka kuivunja amani iliyopo.

Alisema uwepo wa amani na utulivu nchini umechangia watu washiriki kikamilifu kwenye shughuli za maendeleo pasipo kuhofia chochote, hivyo anayetaka kuivuruga JWTZ haitamuachia wala kumuonea huruma.

Mwamunyange alisema JWTZ wako mstari wa mbele kuwalinda na kuwatetea kwa hali na mali wananchi wa Tanzania ili kuhakikisha wanakuwa katika hali ya utulivu na amani.

Naye Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Mehtodius Kilaini, alisema ni wajibu wa viongozi wa dini na serikali kutambua wajibu wao katika kutenda haki na kutetea wananchi.

Askofu Kilaini alisema hayo wakati akiongoza sala ya kuwaombea mashujaa 619 waliouawa katika vita ya Kagera kati ya mwaka 1978 na 1979 wakitetea taifa lao.
Alisema ushindi wa nchi unatokana na umoja, mshikamano na uvumilivu baina ya viongozi na wananchi wanaoungana kutetea masilahi ya taifa lao kutoka kwa adui.

Aliongeza kuwa ili nchi iendelee pamoja na kustawi vizuri kwa jamii yake, amani ni msingi mkubwa unaopaswa kuzingatiwa.

Askofu Kilaini aliwataka viongozi wa dini na serikali kuhubiri amani pamoja na kutekeleza wajibu wa majukumu yao kwa wakati na kufuata utaratibu ulio sahihi kwa wananchi wake.

Wednesday, July 24, 2013

CHADEMA: HAKUNA KUSUBIRI MJADALA WA SERIKALI TATU


Makamu wa Rais,Dk Mohamed Bilal akizindua rasimu ya katiba mpya 

Dar es Salaam/Moshi. Chadema kimepinga kauli ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba kuhusu hatima ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 kikisema mchakato wa sasa wa Mabaraza ya Katiba, usiwe kikwazo cha mjadala wa muundo wa Serikali Tatu.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chadema, John Mnyika alisema Dar es Salaam jana kuwa hatima ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 utakaotokana na mchakato wa mabadiliko ya Katiba unaoendelea, siyo suala la kusubiri.

Akizungumza na mwandishi wetu juzi kuhusu kauli ya Waziri wa Katiba na Sheria Mathias Chikawe kwamba endapo mapendekezo ya Serikali Tatu yatapitishwa, kuna hatihati ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 kufanyika, Jaji Warioba alisema: “Tuachieni muda… hayo mengine ni hisia tu. Ni kweli tunayajua lakini acheni tumalize hili kwanza (la Mabaraza ya Katiba). Hii ndiyo hatua tuliyopo sasa.”

Lakini jana Mnyika alisema: “Hatuwezi kusubiri hadi Mabaraza ya Katiba yakamilishe mchakato kama alivyoeleza Jaji Warioba katika gazeti lenu la Mwananchi toleo la leo, (jana),” alisema Mnyika kwa simu.

Jaji Warioba alitaka suala la muundo wa Serikali Tatu utakavyokuwa lisiwe hoja kwa sasa kwa kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba inachokifanya ni kukusanya maoni kupitia Mabaraza ya Katiba na kisha kuandaa rasimu itakayopelekwa bungeni kwa ajili ya majadiliano na kwamba mjadala huo utawachanganya wananchi endapo utaingizwa katika hatua hii ya ukusanyaji maoni.

Lakini Mnyika alisema: “Mijadala hii haiwezi kusubiri mpaka hatua ya Mabaraza ya Katiba, inapaswa kuanza wakati huu kupitia mabaraza yanayosimamiwa na Tume na Mabaraza yanayoendeshwa na makundi ya kijamii. “Pia, masuala hayo ya mpito pamoja na marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, ni mambo ambayo yanapaswa  kutolewa ufafanuzi wa ziada na Serikali zaidi ya kauli ambayo Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe ameitoa kupitia gazeti la lenu la leo (jana).”

Alisema kimsingi bado kunahitajika mjadala wa masuala ya mpito kwa sababu kuna uwezekano kwamba Katiba Mpya, ya Muungano au ya Zanzibar na ya Tanganyika, isiwe tayari kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, endapo suala la Serikali tatu litapita.

Alisema kwa upande mwingine, rasimu ya Katiba iliyotolewa imeibua mjadala juu ya mkwamo wa kikatiba (constitutional stalemate), ambao ni muhimu upatiwe suluhisho akisema chama chake kinapendekeza mchakato wa Katiba Mpya ya Tanganyika uanze mara moja ili uende sambamba na huu wa Katiba Mpya ya Muungano. Alisema ilikuwa vyema yote yakajadiliwa katika Bunge la Agosti 27, mwaka huu.

Waziri Chikawe alikaririwa na gazeti hili juzi akisema: “Uwepo wa Serikali tatu utafumua mfumo mzima wa utendaji ndani ya Serikali. Hatuwezi tena kufanya uchaguzi wa Rais na wabunge 2015, hatuwezi kufanya chochote nje ya Katiba ya Serikali Tatu kwa kuwa kinachofuata ni kuunda Katiba nyingine inayohusiana na Serikali tatu.

SHEREHE LONDON KWA KUZALIWA MWANAMFALME



William and Kate show off their son to the world - but they are still undecided about the name for the Prince of Cambridge.
Ujumbe wa heri njema umeendelea kutolewa kutoka kote duniani baada ya Kate na Prince William ambaye atakuwa wa tatu kwenye foleni katika kurithi ufalme wa Uingereza.

Mwanamfalme William na mkewe Kate ,wameamkia hospitalini asubuhi ya leo mjini London baada ya kupata mtoto wao wa kwanza Jumatatu jioni.
Mtoto huyo aliyezaliwa akiwa na takriban kilo tatu na nusu atafahamika kama mwanamfalme wa Cambridge, lakini hajapewa jina.

Katika taarifa fupi William,amesema wana furaha isiyo na kifani. Baadaye leo jeshi la Uingereza linatarajiwa kutoa heshima kwa kuzaliwa mwanamfalme huyo kwa kurusha mizinga 40 hewani huko London na kengele la kanisa la Westminster Abbey zitalia.
 
Kawaida saluti ambayo hutolewa kwa mwanamfalme huwa ni mizinga ishirini na moja lakini huongezeka hadi arobaini na moja ikiwa itarushwa kutoka katika makao ya kifalme

Taarifa kutoka katika Kasri la Buckingham, zinasema kuwa Malkia Elizabeth na mumewe walifurahishwa sana na habari za kuzaliwa kwa mtoto huyo. Naye babake William Prince Charles, alisema ana furaha isiyo kifani na ana raha sana kuwa babu kwa mara ya kwanza. 

Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron, alisifu sana kuzaliwa kwa mtoto huyo na kuitaja kuwa hatua muhimu sana kwa Uingereza.

Naye wawiri mkuu wa Australia, Kevin Rudd, alitaja sherehe za jana kama muhimu sana kwa nchi za juimuiya ya madola, huku akiongeza kuwa watu wa Australia wanampenda sana Prince William baada ya kuzuru nchi hiyo akiwa mtoto mwenyewe.

SUDAN KUSINI YAVUNJA BARAZA LA MAWAZIRI


Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini

Rais wa Sudan Kusini, Salva Kiir, amelivunja baraza lake la mawaziri pamoja na kumfuta kazi makamu wa rais Riak Machar katika mabadiliko makubwa zaidi kuwahi kutekelezwa katika historia ya miaka miwili ya taifa hilo. 

Aliyekuwa waziri wa habari, Barnaba Marial Benjamin, ameiambia BBC kuwa mawaziri wote kutoka kwa Makamu wa Rais Riek Machar wameondolewa.

Duru zinasema haijabainika iwapo kuna waziri yeyote miongoni mwa wale waliofutwa kazi atarejeshwa katika baraza jipya la mawaziri litakalobuniwa.

Pia hakuna sababu iliyotolewa kuhusiana na hatua ya rais kuwafuta kazi maafisa hao , lakini wadadisi wanasema kuwa Bwana Kiir na makamu wake Machar wamekuwa na mgogoro wa mamlaka kwa miezi kadhaa sasa.

Sudan Kusini imekumbwa na matatizo chungu nzima hasa ya kiuchumi tangu kujitenga na Sudan mwaka 2011.

Uthabiti wake umetatizwa na malumbano kati yake na Sudan kuhusu mipaka na swala la mafuta.

Hivi karibuni baadhi ya maafisa wa Bwana Kiir, wamekuwa wakizungumzia kuwepo minong'ono kuhusu uongozi wake.

Ripoti zinasema kuwa Kiir anajitahidi kusalia na ushawishi katikachama cha Sudan People's Liberation Movement (SPLM), ambacho kinathibiti serikali.

Kwa upande wake bwana Machar, ambaye mwezi Aprili alipunguziwa mamlaka, alisema huenda akagombea uongozi wa chama cha SPLM dhidi ya rais Kiir, kabla ya uchaguzi mkuu utakaofanyika mwaka 2015.