To Chat with me click here

Friday, September 28, 2012

UONGOZI MPYA WA CCM SASA NDANI YA BAHASHA

MIGIRO MAKAMU MWENYEKITI, NAPE KATIBU MKUU, NGELEJA KATIBU MWENEZI. 

 
UONGOZI mpya wa CCM sasa uko ndani ya bahasha. Kilichobaki ni uamuzi wa kura za wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ( NEC ) kufungua bahasha hiyo na kuweka siri hiyo wazi.

Kumalizika kwa vikao vikuu vya chama kunatoa taswira ya uongozi mpya wa CCM, hasa kuzingatia kilio cha muda mrefu kutoka kwa wanachama kuisihi CCM irejee kwenye uasilia wake.

Sasa ni sura mpya na taswira mpya. Kauli ya Mwenyekiti Taifa, Rais Kikwete kuwa “Hatuwezi kuwa na Chama cha wazee tu, hapana, tumeona tuwape nafasi vijana wengi, tena wasomi waweze kugombea…Ni muhimu kupata sura mpya ya chama na taswira mpya kwa kuingiza wasomi”, ni kauli inayoashiria mabadiliko makubwa katika CCM yanayotarajiwa.

Anaendelea kusisitiza akiwaeleza wajumbe wa NEC, kuwa “lengo ni kuunda timu ya ushindi ya Chama kwa mwaka 2014 katika uchaguzi wa Serikali za mitaa, na mwaka 2015 katika Uchaguzi Mkuu.”

Nasaha kwa wale “wenye ndimimbili” anasema kuwa “isiwe nongwa ukiwa basi ni kulalamikia chama hiki kimefanya nini, ukishafikia hivyo wewe haukuwa na moyo na chama ila moyo wako ulikuwa na shida ya uongozi.”

Wakati hali ikijiri hivyo, hali ndani ya chama inaripotiwa kuwa ni tulivu hata mara baada ya kupita panga la kung’oa visiki, hii ikiashiria kuwa sasa chama kinajivua ‘gamba’, na hii imepokewa kwa shangwe na furaha na wana-CCM wengi.

UCHAGUZI WA MAMEYA NYAMAGANA NA ILEMELA MWANZA LEO


Uchaguzi wa mameya wa wilaya mbili za Nyamagana na Ilemela jijini Mwanza, unatarajiwa kufanyika leo huku mnyukano mkali ukiwa katika halmashauri ya Nyamagana kutokana na CCM na CHADEMA kuwa na idadi sawa ya viti vya madiwani na hivyo kutegemea kura za CUF ziamue mshindi.

Katika Halmashauri ya Ilemela, CHADEMA ina uhakika wa asilimia mia moja kutokana na kuwa na madiwani wengi kuzidi wenzao wa CCM huku mikakati yao ikilenga kuwashirikisha CUF ili waitwae pia Nyamagana.

Uchaguzi huo unafanyika baada ya Halmashauri ya Jiji la Mwanza kugawanywa na hivyo kuzaa halmashauri hizo mbili. Lakini pia Halmashauri ya Jiji la Mwanza kwa sasa muda kadhaa haikuwa na Meya baada ya Baraza la Madiwani kumvua wadhifa huo, Jackson Manyerere (CHADEMA).

Baada ya meya kuenguliwa, kulizuka mtafaruku ndani ya CHADEMA jijini hapa ambao ulisababisha madiwani wawili kutimuliwa uanachama kwa kile kilichodaiwa ni usaliti wa kuanzisha hoja ya kumtosa kiongozi huyo.

Hivyo kutokana na CHADEMA kutokuwa na madiwani hao, inaingia kwenye uchaguzi wa leo ikiwa na madiwani sita na mbunge Ezekiel Wenje katika wilaya ya Nyamagana wakati wenzao CCM wana madiwani saba na CUF wawili.

Kwa mnyukano huo ni dhahiri kuwa CHADEMA na CCM watakuwa wamefungana kwa kura na hivyo kuhitaji huruma ya madiwani wa CUF ili upande mmoja uibuke kidedea.

Taarifa za uhakika kutoka jijini hapa ni kwamba CHADEMA wamefanya mazungumzo ya kushirikiana na CUF kwa kuwaachia nafasi ya Naibu Meya ambayo itagombewa na diwani wao wa kata ya Mirongo, Daud Mukama.

Kwa halmashauri ya Ilemela CHADEMA wana uhakika wa kuibuka kidedea kutokana na kuwa na madiwani wanane na mbunge Highness Kiwia huku wenzao wa CCM wakiwa na madiwani sita na CUF ina mbunge wa Viti Maalum, Mkiwa Kimwanga.

Kamati za utendaji za CHADEMA katika wilaya hizo zimefanya vikao tofauti kwa kushirikiana na kamati za madiwani na kukamilisha mchakato wa kupata wagombea wao.

Kwa mujibu wa ofisa habari wa CHADEMA, Tumaini Makene, kamati ya utendaji ya wilaya pamoja na madiwani wa Nyamagana walimteua aliyekuwa Naibu Meya kabla, Diwani wa Kata ya Maina, Charles Chibara, kuwa mgombea wa umeya wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Kwa upande wa Ilemela, kikao cha kamati ya utendaji pamoja na madiwani walimteua Diwani wa Kata ya Nyamanoro, Abubakar Kapera, kuwa mgombea wa umeya Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela.

Kikao hicho cha Ilemela, pia kilimteua Diwani wa Kirumba, Danny Kahungu, kuwa mgombea wa nafasi ya Naibu Meya halmashauri hiyo wakati kamati ya utendaji ya Nyamagana imekubali kumwachia kugombea nafasi ya Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Diwani wa Mirongo, Daudi Mkama (CUF).

Wao CCM wamemteua Diwani ya Kata ya Mkolani, Stanslaus Mabula, kugombea nafasi ya umeya katika halmashauri ya jiji la Mwanza huku diwani wa kata ya Igogo, John Minja, akigombea unaibu meya na Ilemela wagombea ni Renatus Kalunga na naibu wake Sarah Ng’hwanu.

DK. SLAA: JK AMEIZIKA CCM


ADAI NI KWA KUWAPITISHA WATUHUMIWA WA UFISADI KUGOMBEA

Katibu Mkuu Chadema, Dr. Willibroad Slaa
KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibroad Slaa, amemvaa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, akisema amekitengenezea kaburi la kukizika rasmi chama chake kwa kuruhusu watuhumiwa wakubwa wa ufisadi kugombea nyadhifa mbalimbali.

Dk. Slaa alisema uteuzi wa wagombea ndani ya CCM uliomalizika juzi umeonyesha wazi kwamba sasa chama hicho kinatumbukia kwenye dimbwi kubwa na pana lisiloweza kukitoa tena.

Akizungumza na vyanzo vya habari hizi toka jijini Mwanza, alikojichimbia kuhakikisha mchakato wa uchaguzi wa mameya wa jiji hilo unakwenda vizuri leo, Dk. Slaa alisema dhamira ya kweli dhidi ya CCM katika kuwaweka vijana kwenye uongozi ili kukinusuru chama hicho imezimika baada ya Kikwete kuruhusu watuhumiwa wa ufisadi na wakongwe kugombea uongozi.

“Katika hili la uteuzi wa CCM, nangojea taratibu zao zikamilike. Tulitegemea CCM muda huu ni wa kujisafisha, lakini imeshindwa kufanya hivyo. Mimi simung’unyi maneno kuhusu watuhumiwa wa ufisadi.

Mfano (anataja) ni fisadi wa fedha za rada. Mimi hapa nilishapeleka ushahidi hadi wa akaunti namba ya benki yake kwa DPP (Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini), alisema.

Alisema inashangaza kuona katika utetezi wa CCM, mtuhumiwa huyo amepatiwa nafasi licha ya kushindwa kueleza wazi fedha nyingi kwenye akaunti hiyo ya Uswisi alizipataje.

“Mtuhumiwa mkubwa kama huyu wa ufisadi eti leo CCM inampitisha awe mgombea. Kweli? Sioni dhamira ya CCM kupambana na vitendo vya kifisadi. Na hata dhamira ya vijana haipo bali imejitumbukiza kwenye dimbwi ambalo kamwe hakitatoka humo,” alisisitiza.

Kuhusu Lowassa na tuhuma zake za ufisadi wa kampuni ya kufua umeme wa dharura wa Richmond zilizosababisha kujiuzulu uwaziri mkuu mwaka 2008, Dk. Slaa alisema kiongozi huyo alilazimika kujiuzulu kama sehemu ya kuwajibika, lakini ameshindwa hadi leo kumtaja mhusika hasa wa kampuni hiyo.

Alisema kama kweli Lowassa alisingiziwa katika tuhuma hizo, alipaswa kuwaeleza Watanzania nani anayehusika na ufisadi huo wa Richmond ambayo ilishindwa kuzalisha umeme licha ya kutumia mamilioni ya fedha za umma.

Kuhusu wanachama wa CCM ambao majina yao yamekatwa na NEC, Dk. Slaa alisema milango iko wazi CHADEMA kwa wale wasio mafisadi kujiunga ili kukielekeza chama hicho kushika dola mwaka 2015.

Alisema CHADEMA ni chama makini huenda kuliko vyama vingine, hivyo hakiwezi kupokea wanachama kutoka CCM wanaotuhumiwa kwa ufisadi, vinginevyo kitafunga milango na mapazia yake.

“Unajua, kuna watu wanaojulikana kwa ufisadi. Pia wapo wasafi wanaoomba kujiunga na CHADEMA, hivyo watu safi hawana tatizo kujiunga na CHADEMA kwa ajili ya kuunganisha nguvu kwenda kuongoza dola mwaka 2015,” alisema Dk. Slaa.

TUUNGANE KUMCHANGIA FEDHA ZA MATIBABU MTOTO JULIANA



Mtoto Juliana Mwinuka mkazi wa kijiji Cha Mavanga wilaya ya Ludewa mkoani Njombe aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya CCBRT wodi la wagonjwa wa Macho, sasa amehamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.

Tunaendelea kuwashukuru wote wanaoendelea kutoa michango yao kunusuru uhai wa mtoto Juliana ambaye ni yatima pia tunawaomba muendelee kumchangia mtoto Juliana kwa kupitia namba za Francis Godwin kwa Tigo-Pesa 0712 750199 na M-Pesa 0754 026 299.

HIVI NDIVYO MWANANCHI WA KIJIJI CHA WENDA ALIVYOCHUNWA NGOZI


Hivi ndivyo  mkazi  wa Wenda  alivyochunwa  ngozi na  watu  wasiojulikana (Tunaomba Radhi kwa  picha hizi )
Eneo la tukio

Hivi karibuni vyombo vya habari viliripoti tukio la kusikitisha linalohusisha mauaji ya kinyama ya dereva wa bodaboda Sadiki Mbelwa (26) katika kijiji cha wenda, Tanangozi Iringa ambapo mwili wa marehemu ulikutwa ukiwa na majeraha sehemu za kichwani huku ikisadikiwa kupigwa na kitu chenye ncha kali.

JK: AFUNGUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA AFRICAN GREEN REVOLUTION MJINI ARUSHA


Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza naMwenyekiti wa Alliance for a Green Revolution in Africa Dkt.Kofi Annan(kushoto) pamoja na Mkurugenzi wa Bill and Melinda Gates, Bibi Melinda Gates wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa” Africa  Green Revolution Forum 2012,” uliofanyika katika ukumbi wa Ngurdoto mountain Lodge mjini Arusha.
Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa Kimataifa wa”African Green Revoultionmjni Arusha.