To Chat with me click here

Wednesday, December 24, 2014

M/KITI WA CCM, MKEWE WAUAWA KWA MAPANGA



MAJONZI na huzuni kubwa imetawala kwa wakazi wa Kijiji cha Nyangahe, Wilaya ya Uyui, mkoani Tabora, kutokana na tukio la kuuawa kinyama kwa Mwenyekiti wao wa Serikali ya kijiji, Mussa Chotta na mkewe Mariam Mhoja ambao walikatwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili na watu wasiofahamika.

Mwenyekiti huyo alichaguliwa katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Desemba 14 mwaka huu kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na waliuawa usiku wa kuamkia jana wakiwa nyumbani kwao katika Kitongoji cha Bukili.

Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Katibu wa CCM wilayani humo, Bagaile Lumolla, alisema tukio hilo limetokea katika Kijiji Cha Nyangahe, Kata ya Bukumbi.

Alisema chanzo cha tukio hilo bado hakijajulikana ambapo baadhi ya wananchi waliohojiwa, walilihusisha tukio hilo na itikadi za kisiasa.

Mtoto wa marehemu, Masumbuko Chotta, alisema watu waliofanya unyama huo walikuwa watatu na baada ya kufanya mauaji hayo walitokomea porini.

Alisema siku ya tukio, yeye na wadogo zake walikuwa wamelala ambapo ghafla wakasikia kishindo kikipigwa mlangoni na baada ya kuingia ndani walifanya mauaji ya wazazi wao wakiwa wamefunika nyuso zao.

"Baada ya kuingia ndani walikwenda moja kwa moja chumbani kwa baba na mama wakaanza kuwashambulia kwa kuwakata na mapanga na kusababisha vifo vyao.

"Wakati wakiendelea kufanya unyama huo, nilijaribu kupiga kelele kuomba msaada kwa majirani lakini mmoja wa watu hao alinitandika kofi na kuanguka chini na kapoteza fahamu," alisema Chotta.

Jeshi la Polisi wilayani humo lilithibitisha kutokea kwa tukio hilo, lakini alipotafutwa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo, Juma Bwire ili aweze kulitolea maelezo hakupatikana baada ya msaidizi wake kusema alikuwa kwenye kikao.

No comments:

Post a Comment