To Chat with me click here

Wednesday, December 24, 2014

UTOUH: ZA EPA ZILIRUDI, ZA ESCROW ZIRUDI!


Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
(CAG) mstaafu,Ludovick Utouh

MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mstaafu, Ludovick Utouh, amesema serikali inatakiwa kuhakikisha fedha zake zilizokuwepo kwenye akaunti ya Tegeta Escrow zinarudi kama ilivyokuwa kwa zile za EPA.
Katika mahojiano yake na Raia Mwema yaliyofanyika jijini Dar es Salaam wiki hii, Utouh alisema kama angepewa fursa ya kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuhusu nini cha kufanya na suala la Escrow bila shaka angemwambia ahakikishe anapata kwanza fedha zilizopotea.
“Kwanza niseme kwamba aliyetoa pendekezo kwa serikali kwamba iwabane walioiba fedha za EPA wazirudishe kwanza kabla ya kufuata mikondo ya kisheria ni mimi. Hela kurudi ni jambo la muhimu sana.
“Ushauri wangu ni kwamba uchunguzi unatakiwa ufanyike na wale watakaobainika kufanya wizi basi warudishe fedha walizoiba na halafu wapelekwe mahakamani.
“Watu wanaolalamika kuhusu wezi wa EPA wanafanya hivyo kana kwamba watu walirudisha fedha na wakaachiwa jambo ambalo si la kweli. Hela zilirudi na bado kesi zikaendelea mahakamani na zinaendelea hadi hivi leo tunavyozungumza.
“Hivi kuna tatizo gani kama mtu atarejesha fedha aliyochukua? Huyu mtu unaweza kumkuta na hatia na ukampeleka jela lakini akifika kule atakula na kulala bure kwa gharama za walipa kodi. Kama atalipa fedha alizoiba, ndizo fedha hizohizo zitatumika kumhudumia.
“Ninachosema hapa, kitu kizuri ni kipi? Kuendelea na kesi kwa miaka mingi na huku ukitumia fedha za umma kuzihudumia au angalau kushinikiza kwanza hela zilizochukuliwa zirudishwe na kesi zikaendelea kama kawaida?
“Kutaka hela zirudishwe haina maana hata kidogo ya kusamehe watuhumiwa bali maana yake ni kuhakikisha kile kilichochukuliwa kinapatikana kwanza,” alisema Utouh.
Katika mahojiano hayo, Utouh alisema ni sahihi kwa ripoti ya CAG kuhusu suala la Escrow kusema fedha zilizokuwepo katika akaunti ya Escrow ni za umma na pia si umma kwa vile huo ndiyo ukweli.
“Kama ulifuatilia mjadala ule wa bungeni, kitu cha kwanza ambacho kilisemwa na kipo kweli ni suala la kodi. Ndani ya fedha zilizokuwepo kwenye akaunti ya Escrow kulikuwa na kodi. Kodi ni mali ya umma. Hivyo kwenye eneo hilo la kodi, fedha za umma zipo.
“Jambo la pili lipo kwenye historia ya kuanzishwa kwa akaunti hiyo. IPTL na Tanesco walikuwa na mzozo kuhusu malipo ya capacity charge. Mgogoro ulikuwa mkubwa na wakaamua kuweka fedha za malipo hayo kwenye akaunti ya Escrow huku wakisubiri shauri lao kutoka katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro.
“Sasa, nizungumze kama mfano tu, hypothetical, kwamba IPTL walikuwa wanaichaji Tanesco shilingi 30 kwa siku. Tanesco wakaona kwamba wanalaliwa kwa gharama hizo. Wanalipa zaidi ya wanavyotakiwa kulipa.
“Wakaenda mahakamani kushitaki. Uamuzi uliotoka ni kwamba, ni kweli Tanesco wamebambikiwa hizo gharama. Inabidi gharama za capacity charge zikokotolewe upya. Sasa ofisi ya CAG haina mamlaka ya kufanya ukokotoaji huo.
“Kwa hiyo, kama ukokotoaji ungefanyika, labda tuseme IPTL ingetakiwa kutoza shilingi 20 kwa siku, maana yake ile tofauti ya shilingi 30 inayotozwa na shilingi 20 inayotakiwa kutozwa, yaani shilingi 10, ingekuwa ya Tanesco.
“Hii maana yake ni kwamba, katika kila shilingi 30 iliyokuwepo katika Escrow, ukiondoa zile za kodi, shilingi 20 zilikuwa za IPTL kwa sababu ya umeme wake iliyouza na shilingi kumi zilikuwa za Tanesco ambayo ni taasisi ya umma,” alisema.

No comments:

Post a Comment