To Chat with me click here

Thursday, March 14, 2013

POLISI WATANO KIZIMBANI WIZI WA SH. MILIONI 150

Baadhi ya askari polisi wanaotuhumiwa kuiba Sh. milioni 150 baada ya kuziokoa katika tukio la ujambazi eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam wakifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
Askari watano wa Jeshi la Polisi wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, wakikabiliwa na shtaka la wizi wa Sh. milioni 150.

Washtakiwa hao walikwenda kuzuia tukuo la ujambazi wa kupora katika duka moja eneo la Kariakoo, lakini wakatuhumiwa kuiba fedha zilizoporwa na majambazi hao kisha kuzidondosha.

Washitakiwa hao walisomewa mashtaka yao jana mbele ya Hakimu Mkazi,  Emmilius Mchauru.

Washtakiwa hao ni Stafu sajenti D. 8845 Dancan Mwasabila (43),  Koplo E.9288  Geofrey (39), Koplo E. 5585  Rajabu Nkumkwa (46), Koplo E.29249 Kawanani  Humphrey (34)  na Koplo E. 5548 Kelvin Mohamed(44).

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Bernad Kongola, alidai kuwa Desemba 18, 2012 katika eneo la Kariakoo Wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam, washtakiwa hao kwa pamoja waliiba fedha taslimu Sh. milioni 150, mali ya Mire Artan Ismail.

Washtakiwa wote walikana shtaka hilo na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi bado haujakamilika na haukuwa na pingamizi ya dhamana dhidi yao.

Hakimu Mchauru alisema washtakiwa wanatakiwa kusaini hati ya dhamana ya  Sh. milioni tano, kuwasilisha fedha taslimu Sh. miloin 15 au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo ya fedha.

Mbali na masharti hayo ya dhamana, pia kila mshtakiwa alitakiwa  kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika  ambao kila mmoja wao angesaini bondi ya Sh. milioni tano.

Hata hivyo, mshtakiwa wa kwanza hadi wane walitimiza masharti hayo na mshtakiwa wa tano amekwenda mahabusu hadi Machi 27, mwaka huu itakapotajwa tena.

No comments:

Post a Comment