To Chat with me click here

Wednesday, March 13, 2013

WAZIRI MEMBE ATAJWA SAKATA LA KUTESWA KIBANDA


Waziri wa Mambo ya Nje, Mhe. Bernard Membe

JINA la Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimaitafa, Bernard Membe, limeanza kuhusishwa na tukio la kutekwa na kuteswa kikatili na watu wasiojulikana lililomkuta Mhariri Mtendaji Mkuu wa New Habari (2006) Ltd, Absalom Kibanda.

Madai ya kulihusisha jina la Waziri Membe na tukio hilo, yalianza kuzagaa miongoni mwa watu waliofika katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kumjulia hali Kibanda, muda mfupi baada ya kutendewa unyama huo.

Makundi ya watu waliokuwa hospitalini hapo walilioanisha tukio hilo na kauli iliyopata kutolewa na Waziri Membe katika mahojiano ya kipindi cha Dakika 45, kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV, alipoeleza kuwa anao maadui wakubwa 11, wakiwamo waandishi wa habari wawili ambao aliahidi kuwashughulikia.

Ingawa Membe alikutana na shinikizo la watu mbalimbali lililomtaka awataje maadui zake hao 11, wakiwamo waandishi wa habari wawili ambao alikuwa na mpango wa kuwashughulikia, hadi sasa hajapata kufanya hivyo, jambo ambalo linadaiwa na wadadisi wa mambo kuwa ni uamuzi wake wa kuchukua mkondo wa kutekeleza kile alichokisema kwa vitendo.

Tamko lake hilo katika kipindi hicho kilichorushwa hewani Julai 16, 2012, ambalo limeibua hali ya sintofahamu, sasa linaonekana kuchukuliwa kwa uzito zaidi na wanahabari na wamiliki wa vyombo vya habari, baada ya kuwa moja ya mambo mazito yaliyozungumzwa jana katika mkutano wa wamiliki wa vyombo vya habari.

Kwa takribani siku mbili, Membe amekuwa akitafutwa na gazeti hili kwa ajili ya kuzungumzia madai hayo, lakini hata hivyo jitihada za kuzungumza naye hazikufanikiwa, baada ya simu yake kuita wakati wote bila majibu.

Hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu yake ya kiganjani, hakujibu, licha ya kuonyesha umefika.

Jana katika mkutano huo wa wamiliki wa vyombo vya habari ulioketi Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, kujadili kuzorota kwa mazingira ya usalama ya waandishi na wanaharakati wengine, suala hilo la Membe pia lilijadiliwa.

Wakijibu maswali ya waandishi waliotaka kujua namna viongozi wa serikali na watendaji wa vyombo vya ulinzi na usalama wanavyohusishwa na matukio ya aina hii, wamiliki hao walieleza kuwa wapo baadhi ya watendaji waandamizi wa serikali waliokwishalitangazia taifa kuwa wanao maadui 11 hapa nchini, wawili kati ya hao ni waandishi wa habari walioahidi kuwashughulikia.

Akizungumza kwa niaba ya wamiliki wenzake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Hussein Bashe, alisema ni jambo la kushangaza kuona kauli kama hiyo iliyotolewa na kiongozi mwandamizi wa serikali haijafanyiwa kazi na vyombo vya ulinzi na usalama.

“Mfano, mwaka jana, alinukuliwa mwanasiasa na kiongozi wa Serikali kupitia kipindi cha Dakika 45, akisema kuwa ana maadui 11 ambao kati yao, wawili ni waandishi wa habari, hivi kauli hii ambayo ilikuwa ikiruka katika kituo cha luninga haikusikika au adui mwenyewe kati ya waliotajwa ndiyo Kibanda?

“Kama ni hivyo, mbona haitwi ili ahojiwe kuhusu hali hii na vyombo hivi vya ulinzi na usalama vya nchi yetu, tunahitaji kuona kuwa Serikali yetu inafanya kazi na hata kulinda maisha ya watu wake,” alidai Bashe.

Sehemu ya kauli ya Waziri Membe katika kipindi hicho kilichokuwa kikiongozwa na mtangazaji Selemani Semunyu, ambayo sasa inaonekana kuwa hatari kwake, alisema: “Lazima watu hao wajue kwamba ukikaa juu ya nyoka, ipo siku atakugonga tu. Hili nawaachia Watanzania waamue, lakini kuna watu 11, wakiwamo waandishi wawili wa habari, nitawatwanga kweupe.”

Kutokana na hali ya kuzorota huko kwa usalama, hususan wa wanahabari, wamiliki hao waliazimia kuundwa kwa kamati ya watu 16 ambayo itakutana na vyombo vya usalama nchini kuzungumzia kwa undani wa tukio hilo na usalama wa makundi yanayolengwa na vitendo vya kushambuliwa, kuumizwa na hata kuuawa kwa waandishi.

Maazimio mengine yaliyofikiwa katika mkutano huo ni kuitaka serikali kuunda tume huru ya wapelelezi kuchunguza undani wa sakata hilo, kwa sababu kasi ya upelelezi wa vyombo vya usalama vya hapa nchini hairidhishi na kwamba baadhi ya watendaji ndani ya vyombo hivyo wanahusishwa na matukio haya ya utesaji na utekaji.

Aidha, katika kikao hicho, wanachama wa MOAT ambao walisoma tamko lao kwa waandishi wa habari baada ya kumaliza kikao chao, walisema pamoja na kuwepo kwa vitendo vya kuwatesa na kuwaua waandishi, bado ukweli utasimama katika jamii.

Wamiliki hao, ambao waliachiana zamu kusoma tamko lao, walisema vyombo vya usalama kudaiwa kuhusika na vitendo vichafu dhidi ya rais ni udhaifu.

Mmoja wa wajumbe hao, Reginald Mengi, akisoma moja ya maazimio ya mkutano huo, alisema kumekuwa na tishio dhidi ya wanahabari, huku akimtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kutaja maofisa wa vyombo vya ulinzi waliokwenda nyumbani kwa mwandishi wa habari, Eric Kabendera na kuwatisha wazazi wake.

“Tunajua wazi jambo hili lilipangwa na watu ambao wamekuwa wakitumia fedha hata za ufisadi ili kutishia uhai wa waandishi wa habari, kutokana na matukio haya yaliyojitokeza namuomba Waziri Nchimbi awataje maofisa hao, kama asipofanya hivyo tutawataja kwa majina mchana kweupe.

“Pamoja na hila na vitimbi vinavyofanywa na watumishi hao wa idara za ulinzi na usalama dhidi ya wanahabari, ni vema Serikali ichukue hatua za haraka ili kuondoa hali hii. Hivi sasa Watanzania wamekuwa wakiishi kwa woga na katu huwezi kusema nchi ina amani huku watu wake wakitishwa.

“Ninapenda kusema kuwa kwa matukio haya ya kupigwa na kuteswa kwa Kibanda na hili tukio la wazazi wa Kabendera kuhojiwa kule Bukoba, ni wazi hata wakituua watakaobaki watasema ukweli wa nini kilichopo sasa,” alisema Mengi.

Mengi ambaye ni Mwenyekiti wa MOAT, pia alitumia fursa hiyo kutangaza majina ya kamati itakayokutana na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama, kuwa ni pamoja na yeyé mwenyewe ambaye ni mwenyekiti wa kamati hiyo, wajumbe ni Hussein Bashe, Tido Mhando, Aga Mbuguni, Abdallah Mrisho, Ansbert Ngurumo, Mikidadi Mahamud, Pili Mtambalike, Godfrida Jola, Tumaini Mwilenge na Deodatus Balile.

Wengine ni Katibu Mkuu wa Jukwaa la Wahariri nchini, Neville Meena, Samson Kamalamo, Henry Muhanika, Japhet Sanga na Jesse Kwayu.

Alisema wadau hao, mbali na kukutana na Waziri Nchimbi, pia watakutana na Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi, Saidi Mwema, Mkuu wa Usalama wa Taifa, Othuman Rashid na Naibu wake, Jack Zoka pamoja na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Dk. Edward Hosea.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Hussein Bashe, alisema hatua ya kupigwa kwa Kibanda ilipangwa na watu ambao alidai ni watumishi wa vyombo vya ulinzi.

Alisema wiki tatu kabla ya tukio hilo, zilionekana kila dalili za baadhi ya watumishi wa vyombo vya ulinzi ambao wamekuwa wakitumiwa na baadhi ya watu kwa maslahi yao binafsi kuwafuatilia yeye na Kibanda.

Bashe alisema wiki tatu kabla ya Kibanda kufanyiwa unyama, wakiwa wameongozana kuelekea nyumbani, walifuatwa na gari la Polisi lenye namba PT 180, ambalo lilikuwa limeegeshwa nje ya lango la Ofisi ya New Habari, huku likiwa katika uelekeo wa kwenda Shekilango.

“Baada ya muda lile gari liligeuza na kuanza kutufuata kwa nyuma na tulipofika katika eneo la Sinza Makaburini, lilitupita na kutuzuia kwa mbele. Kutokana na hali hiyo, Kibanda akiwa katika gari lake nyuma yangu alinitaka nisishuke, ila nimuulize yule Polisi ana shida gani.

“Jibu lake lilikuwa eti anazishuku gari zetu kuwa kuna kitu, baada muda na kumpa maelezo ya kujitosheleza, yule Polisi aliondoka, nasi tukaendelea na safari yetu ya kuelekea nyumbani Mbezi Beach. Hata hivyo pamoja na kazi kubwa inayofanywa na Waziri Nchimbi ya kusafisha Wizara ya Mambo ya Ndani, lakini bado tunaona kuna maofisa wake wanakwenda kinyume na maadili ya kazi yao.”

Mkurugenzi huyo Mtendaji wa New Habari (2006) Ltd, aliitaka Serikali iunde tume huru ya wapelelezi ili kuweza kuchunguza kwa undani masuala haya, kwa kuwa kasi ya uchunguzi wa nyombo vya usalama nchini hairidhishi na pia baadhi ya watendaji wa vyombo hivyo kuhusishwa na kadhia hizi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Hussein Bashe, alisema hatua ya kupigwa kwa Kibanda ilipangwa na watu ambao alidai ni watumishi wa vyombo vya ulinzi.

Alisema wiki tatu kabla ya tukio hilo, zilionekana kila dalili za baadhi ya watumishi wa vyombo vya ulinzi ambao wamekuwa wakitumiwa na baadhi ya watu kwa maslahi yao binafsi kuwafuatilia yeye na Kibanda.

Bashe alisema wiki tatu kabla ya Kibanda kufanyiwa unyama, wakiwa wameongozana kuelekea nyumbani, walifuatwa na gari la Polisi lenye namba PT 180, ambalo lilikuwa limeegeshwa nje ya lango la Ofisi ya New Habari, huku likiwa katika uelekeo wa kwenda Shekilango.

“Baada ya muda lile gari liligeuza na kuanza kutufuata kwa nyuma na tulipofika katika eneo la Sinza Makaburini, lilitupita na kutuzuia kwa mbele. Kutokana na hali hiyo, Kibanda akiwa katika gari lake nyuma yangu alinitaka nisishuke, ila nimuulize yule Polisi ana shida gani.

“Jibu lake lilikuwa eti anazishuku gari zetu kuwa kuna kitu, baada muda na kumpa maelezo ya kujitosheleza, yule Polisi aliondoka, nasi tukaendelea na safari yetu ya kuelekea nyumbani Mbezi Beach. Hata hivyo pamoja na kazi kubwa inayofanywa na Waziri Nchimbi ya kusafisha Wizara ya Mambo ya Ndani, lakini bado tunaona kuna maofisa wake wanakwenda kinyume na maadili ya kazi yao.”

Mkurugenzi huyo Mtendaji wa New Habari (2006) Ltd, aliitaka Serikali iunde tume huru ya wapelelezi ili kuweza kuchunguza kwa undani masuala haya, kwa kuwa kasi ya uchunguzi wa nyombo vya usalama nchini hairidhishi na pia baadhi ya watendaji wa vyombo hivyo kuhusishwa na kadhia hizi.
Mbuguni na uvamizi
Katika kikao hicho, wadau hao walitoa maazimio matano ambapo mwakilishi kutoka Kampuni ya Business Times, Aga Mbuguni, alisema katika kikao hicho kilichokuwa kinaongozwa na Chama Cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari nchini (MOAT), wanaamini kuwa kutekwa na kuteswa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini, Absalom Kibanda, kumetokana na msimamo wa kalamu yake.

Alisema shambulio hilo halikutokana na kitu kingine ambapo wadau hao wamelichukulia shambulio hilo dhidi ya uhuru wa vyombo vya habari nchini na kuwajengea hofu wahariri, waandishi na wanaharakati wote ili wasitekeleze wajibu wao kwa umma.

Jesse na maofisa usalama
Kwa upande wake, Mhariri Mtendaji wa Nipashe, Jesse Kwayu, alisema kuwa wadau wa vyombo vya habari wamesikitishwa na hatua ya baadhi ya maofisa na watumishi wa vyombo vya usalama, kutumiwa na kutekeleza vitendo vya uhalifu ambavyo vinatishia usalama wa waandishi wa habari na wananchi kwa ujumla.

“Kutokana na hali hii na mfano halisi, ni usumbufu alioupata mwandishi wa habari, Eric Kabendera na familia yake, ambapo wazazi wake walihojiwa na watu waliojiita watumishi wa Idara ya Uhamiaji, waliotumwa kutekeleza azma ya watu fulani wenye lengo la kuleta hali ya kuzorota kwa usalama wa waandishi wa habari,” alisema Kwayu.

No comments:

Post a Comment