To Chat with me click here

Thursday, October 16, 2014

KARDINALI PENGO: KUSTAAFU BAADA YA MIAKA MITANO IJAYO!



Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam,
Kardinali Polycarp Pengo
“Najua wengine wanashangaa kuona askofu wao akitembea namna hii, kwa mkongojo, hivi ndivyo ilivyo, nilikuwa mgonjwa, lakini nawashukuruni nyote kwa kuniombea, Mwenyezi Mungu awabariki,”

Alisema kiongozi huyo na kuibua vifijo kutoka kwa mamia ya waumini walioshiriki misa hiyo.

Dar Es Salaam. Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Kardinali Polycarp Pengo amesema waumini wa kanisa hilo hawana sababu ya kuingiwa wasiwasi kuhusu hali yake kiafya kwa kuwa anastaafu miaka mitano ijayo.

Akihubiri katika ibada maalumu ya misa iliyoandaliwa na Utume wa Wanaume Katoliki (Uwaka) jimboni humo juzi, Kardinali Pengo mwenye umri wa miaka 70 alieleza kuwa anajiandaa kustaafu kisheria, jambo ambalo halina sababu ya kuwaweka roho juu waumini.

Katika mahubiri yake ya muda mfupi kwenye misa hiyo iliyofanyika Kituo cha Kiroho Mbagala, Dar es Salaam juzi Kardinali Pengo alitumia muda huo kuzungumzia afya yake, akisema kwa muda sasa amekuwa haonekani hadharani kutokana na kuumwa.

Hata hivyo, bila kutaja aina ya ugonjwa uliokuwa ukimsumbua, Kardinali Pengo ambaye Machi mwaka huu aliadhimisha miaka 30 ya uaskofu na wakati ule ilielezwa kuwa alikuwa mgonjwa asiyetakiwa kusafiri umbali mrefu, alitumia muda huo juzi kuwashukuru waumini wa kanisa hilo na Watanzania kwa jumla kwa maombi yao wakati wote alipokuwa akiumwa.

“Wapo watu wengi walikuwa na wasiwasi kuhusu hali yangu, wengine si Wakristo, walinipigia simu wakinijulia hali. Nawashukuru wote kwa kuniombea, sasa nimepata nafuu.
 
“Najua wengine wanashangaa kuona askofu wao akitembea namna hii, kwa mkongojo, hivi ndivyo ilivyo, nilikuwa mgonjwa, lakini nawashukuruni nyote kwa kuniombea, Mwenyezi Mungu awabariki,” alisema kiongozi huyo na kuibua vifijo kutoka kwa mamia ya waumini walioshiriki misa hiyo.

Tofauti na kawaida yake ya kuzungumzia mambo mengi katika jamii kwa kujiamini, katika misa hiyo juzi, kiongozi huyo alitumia mahubiri yake kueleza kuwa kanisa hilo ni taasisi iliyo imara na ambayo hata akiondoka katika uongozi, atapatikana mwingine bila kuvuruga misingi iliyopo.

“Hata kama afya yangu isingetetereka, nimebakisha miaka mitano, nitastaafu, lakini hakuna sababu ya msingi ya waumini kuanza kuingiwa hofu yoyote kuhusu ni nani atarithi nafasi yangu. Sisi (kanisa) tunao mfumo imara wa kupata viongozi wetu.”

Pia, Kardinali Pengo alikemea migawanyiko ambayo alisema imeanza kujitokeza katika baadhi ya parokia za jimbo hilo, akisema haikubaliki.

“Nimesikia minong’ono kuwa baadhi ya parokia, zipo nyingine zinajitangaza kuwa ni za mashirika ya kitawa, sikubali, sitaki kuona hili likitokea, mwenye mamlaka kusimamia parokia zote ni askofu, ni mimi,”alisema.

No comments:

Post a Comment