To Chat with me click here

Friday, October 17, 2014

MANDELA, MKAPA WALIVYOMWANGUSHA NYERERE!




BABA wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alimaliza siku zake za mwisho katika hali ya masikitiko kutokana na vitendo vya mwisho vya watu aliowaamini sana.

Wakati Watanzania wakiadhimisha miaka 15 tangu kufariki kwa Mwalimu katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas jijini London, Uingereza mwaka 1999, taarifa mpya zimeibuka kuhusu namna alivyotumia siku zake za mwisho.

Katika mahojiano ambayo vyanzo vya habari hii vilifanya na watu waliokuwa karibu naye ikiwamo familia yake na watu aliokuwa akifanya nao kazi, mambo makubwa mawili yameelezwa kumuumiza Mwalimu.

Mambo hayo ni mchango mdogo wa serikali za Tanzania na Afrika Kusini kwa taasisi yake ya Mfuko wa Mwalimu Nyerere (MNF) na ubinafsishaji wa iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC).

Mmoja wa viongozi wa MNF aliyezungumza na vyanzo vyetu vya habari  kwa masharti ya kutotajwa jina, alisema Mwalimu alihuzunika sana wakati alipokwenda nchini Afrika Kusini kutafuta fedha za taasisi hiyo na kuambulia mchango kidogo sana.

“Wakati Nelson Mandela akiwa Rais wa Afrika Kusini, Mwalimu alikwenda kutafuta fedha kule akiwa na matumaini makubwa sana. Unajua Tanzania ilijitolea sana kwa ajili ya Uhuru wa Afrika Kusini.

“Afrika Kusini ina uwezo mkubwa wa kiuchumi. Mwalimu alitaraji makubwa sana kutokana na uhusiano baina ya nchi hizi mbili. Cha ajabu, alipokwenda kule serikali ilimpa kiasi cha dola 60,000 (takribani shilingi milioni 60 wakati huo).

“Hebu fikiria uwezo wa kiuchumi wa Afrika Kusini na mchango ambao Mwalimu na Tanzania kwa ujumla walikuwa nao kwa Taifa hilo na halafu Mwalimu anapewa dola 60,000. Nyerere returned a broken man (Nyerere alirudi akiwa amefadhaika sana),” alisema kiongozi huyo.


Kiongozi huyo alieleza pia kwamba kwa upande wa Serikali ya Tanzania, msaada pekee ambao MNF iliupata ni kiwanja kilichopo jirani na Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam kilichotolewa wakati wa Serikali ya Rais Ali Hassan Mwinyi, na hawakuwahi kupokea fedha yoyote kutoka serikalini hadi leo.

“Hebu fikiria, serikali yake mwenyewe ya Tanzania haikumpa hata senti moja kwa ajili ya MNF. Serikali ya Rais Benjamin Mkapa haikuwahi kumpa kitu na nafahamu serikali ya Jakaya Kikwete pia haijawahi kuchangia MNF. Hilo ndiyo tatizo,” alisema kiongozi huyo.

Kutokana na hali hiyo, kiongozi huyo alimnukuu Mwalimu Nyerere akisema mwaka mmoja kabla ya kifo chake; “Siku nikifariki dunia, kesho yake tu MNF itakufa”.

Vyanzo vyetu vya habari vimeelezwa pia namna wasaidizi wa karibu wa Mwalimu walivyoshangazwa na ukweli kuwa katika kitabu cha Mandela cha The Long Walk to Freedom, Mwalimu alitajwa mara moja tu kwenye kitabu hicho.

Katika kitabu hicho, Mandela alimtaja Mwalimu wakati akieleza kuhusu harakati zake za kutafuta kuungwa mkono na nchi za Afrika katika mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi, ambapo alitembelea Tanganyika huru kutafuta kuungwa mkono.

Wakati wa utawala wa Makaburu wa Afrika Kusini, ilikuwa marufuku kutaja hadharani jina la Nyerere au Tanzania kwa vile ilionekana kama ni uchochezi. Lakini pia Makaburu walitaka kuzuia ushawishi wa Nyerere kwa watu Weusi wa kule. Ndiyo maana Mwalimu alitaraji makubwa sana kutoka huko.

“Ni sawasawa na utawala wa Mkapa. Watanzania wote wanafahamu kuwa isingekuwa Mwalimu, Mkapa huenda asingeupata urais wa Tanzania. Alitaraji huyo ndiye angeisaidia MNF kuliko pengine rais yeyote. Cha ajabu, serikali ya Mkapa haikuchangia kitu. Afadhali hata Mzee Mwinyi ambaye alichangia kiwanja,” kilisema chanzo hicho cha habari hii.

Katika mahojiano mengine na aliyekuwa Katibu Myeka wa Mwalimu, Samwel Kassori, ilibainika pia namna Mwalimu alivyohuzunishwa na suala la kuuzwa kwa NBC kwa mojawapo ya makampuni kutoka nchini Afrika Kusini.

“Lakini moja kubwa ninalokumbuka ni kuhusu mchakato wa uuzwaji wa benki ya NBC mwaka 1997 mwezi Aprili  wakati wa utawala Mkapa ambapo Mwalimu aliwahi kulengwalengwa na machozi akipinga benki hiyo kuuzwa  kwa ABSA Group kutoka Afrika ya Kusini.

“Wakati huo nakumbuka  serikali ilipanga  kumwandalia Mwalimu sherehe ya kitaifa ya siku yake ya kuzaliwa (birthday) ya kutimiza miaka 75 ambazo zingefanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee wa Jijini Dar es Salaam, na jambo hilo lilimshtua kidogo akaniagiza nichunguze fedha hizo zingetoka wapi na kwanini afanyiwe sherehe kubwa kiasi hicho na pia tetesi zilikuwa zimezagaa kuwa NBC inauzwa.

“Wakati huo Waziri wa Fedha alikuwa Daniel Yona, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo alikuwa Peter Ngumbulu na Gavana wa Benki Kuu (BoT) alikuwa Dk. Idris Rashid.

“Baada ya kupata taarifa za kwamba benki hiyo iko mbioni kupigwa bei, Mwalimu aliomba maelezo kutoka kwa wahusika ambao ni Waziri wa Fedha, Katibu Mkuu na Gavana wa BoT.

“Majibu ya serikali yalikuwa kwamba NBC inauzwa kwa sababu taasisi za fedha za Kimataifa za Fedha (IMF) na Benki ya Dunia (WB) ziliagiza Benki hiyo kuuzwa.

“Baada ya kupata maelezo hayo Mwalimu alikasirika kweli kweli, akaniita na tukiwa nyumbani kwake Msasani aliniagiza kumpigia simu Rais wa (WB) wakati ili azungume naye.

“Baada ya kumpata Rais huyo wa (WB) ambaye bado alikuwa akimwita Mwalimu Mr. President (Mheshimiwa Rais), alikana IFM pamoja na Benki ya Dunia kushinikiza au kutoa masharti kuuzwa kwa NBC.

“Namnukuu Rais huyo wa WB aliniambia:”Mr Kasori do me a favour could you request President Nyerere to come to our  headquarters  in Washington and read the documents from Tanzania government, they are too voluminous but will try to make executive summary of the same”

“Maana yake ni kwamba walitaka Mwalimu akajioonee mwenyewe nyaraka zilizotumwa katika taasisi hizo za kimataifa kuhusu uuzaji wa NBC na walisema wangelipa gharama zote muhimu za safari hiyo.

“Baada ya mazungumzo ya simu siku mbili baadaye tulifunga safari na Mwalimu hadi Washington nchini Marekani ambapo tulikutana na Rais wa WB kwa kikao cha siku nzima na kupitia nyaraka muhimu zilizowasilishwa kwao na serikali ya Tanzania.

“Tulirudi nyumbani baada ya wiki moja na Mwalimu aliniagiza kwanza  niwatafute Yona, Ngumbulu na Dk. Rashid ili azungumze nao kabla ya kukutana na Rais Mkapa.

“Basi baada ya mimi kufanya mawasiliano nao wote hakuna aliyeitikia wito wa Mwalimu “walimpuuza” na badala yake walimtuma Donald Kamori ambaye alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC.

“Nakumbuka vizuri kikao na Kamori kilifanyika Msasani nyumbani kwa Mwalimu Nyerere, Aprili 13 mwaka huo 1997, na Kamori alikuwa mtaalamu aliyebobea katika masuala ya fedha na ndiye kati ya wataalamu wazawa walioanzisha BoT.

“Kamori akiwa na nyaraka na takwimu za kitaalamu. Alimweleza Mwalimu bila ya kuficha kuwa kuiuza NBC serikali ilikuwa inafanya makosa makubwa katika sekta ya fedha kwa kuwa Benki hiyo ilikuwa inaendeshwa kwa faida kubwa. Uuzwaji wake ungeleta athari ya moja kwa serikali pamoja na taasisi zake nyeti.

“Mwalimu alitikisa kichwa kwa masikitiko makubwa, akasema ‘ooooh kweli nimesomesha Watanzania’ alikuwa amevutiwa sana na maelezo ya kitaalamu ya Donald Kamori.

“Baada ya kupata maelezo ya kutosha kutoka kwa Kamori, Mwalimu aliomba kukutana na Rais Mkapa na kikao kilifanyika Ikulu ambapo alitetea NBC isiuzwe kwani ndiyo ilikuwa nguzo ya serikali hasa wakati inapoishiwa fedha  katika mambo “nyeti yanayohusiana na usalama wa nchi”  ilikuwa inakopa fedha NBC.

“Majadiliano na Mkapa yalichukua muda mrefu sana kuhusu suala hilo na itoshe kusema kwamba baada ya majadiliano hayo marefu likazaliwa wazo la kugawanywa  kwa hiyo  na kuanzishwa kwa Benki ya NMB ambayo serikali  ina hisa hadi leo.

“Kilichomsikitisha zaidi Mwalimu ni kwamba baada ya juhudi zote hizo Kamori alifukuzwa kazi  kama Mkurugenzi Mtendaji wa NBC  na kurudishwa BoT bila kupangiwa kazi yoyote. Hakuwa na ofisi pale akifika anasoma magazeti aliyojinunulia na kurudi zake nyumbani.

“Alitishwa sana na kuhojiwa ni kwanini alikwenda kumweleza Mwalimu na kumwonyesha nyaraka za uuzwaji wa NBC kwa Benki ya ABSA ya Afrika ya Kusini?

“Kamori alinipigia simu akanieleza masahibu yaliyomkuta na mimi nikaufikisha ujumbe wake kwa Mwalimu, baada ujumbe huo Mwalimu alisikitika sana, akahoji ni kwanini wanafanya mambo hayo “kumfedhehesha” akiwa hai?

“Huyo Kamori alikuwa mzalendo kweli kweli ni kati ya Watanzania walioipenda nchi yao. Siku hiyo hiyo aliacha kazi akasema hawezi kupokea mshahara asioufanyia kazi na akaenda kufanya kazi zake sijui kwa sasa atakuwa wapi.

“Sakata la kuuzwa kwa NBC kwa kweli ni kati ya mambo yaliyowahi kumchanganya akili Mwalimu na kwa upande wangu uuzwaji wa benki ile ulifungua milango ya ufisadi mwingine uliokuja kufanyika miaka ya baadaye,” alisema.

No comments:

Post a Comment