Dar/mikoani.
Kashfa ya uchotaji wa fedha katika Akaunti ya Tegeta Escrow inayoendelea
kulitingisha Taifa, jana ilitawala mahubiri ya Sikukuu ya Krismasi katika
makanisa mbalimbali nchini, viongozi wa dini wakionyesha kutoridhishwa na
maelezo na hatua zinazochukuliwa. Wakihutubia
waumini wao, viongozi hao walitumia siku hiyo kukemea vitendo vya ufisadi, wizi
na uzembe.
Hofu ya Escrow
Ujumbe
wa Askofu wa Dayosisi ya Central Tanganyika (DCT) wa Kanisa la Anglikana, Dk
Dickson Chilongani ulilenga kueleza hofu ya wananchi kutokana na sakata la
Akaunti ya Tegeta Escrow, ugumu wa maisha, ukosefu wa ajira, kukosa uhakika wa
huduma bora za matibabu na elimu pamoja na wimbi la viongozi waandamizi
wasiokuwa waaminifu na waadilifu.
Akihubiri
katika Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu mjini Dodoma, Askofu Chilongani alisema
mbali na maisha ya ufukara na ukosefu wa huduma, sakata la Escrow na hotuba ya
Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa Jumatatu vimezidi kuzidisha hofu kwa Watanzania
na kuwafanya waonekane kama hawana tumaini.
Akitumia
mtindo wa kuhoji, Askofu Chilongani alianza kwa kuhoji, “Kitu gani kinakutia
hofu unaposherekea sikukuu hii, watu wengi tunaishi katika ulimwengu wa hofu
kutokana na ufukara, ukosefu wa huduma, tunajiuliza tutawasomeshaje watoto
wetu, tutapataje huduma bora za matibabu, yaani kila mmoja wetu ana hofu,”
alisema.
Askofu
Dk Chilongani alisema ingawa kila mtu ana hofu yake lakini sakata la akaunti ya
Escrow limejenga hofu kwa mwananchi, kila mmoja akihoji na kutengeneza majibu
yake jambo linalotoa picha kuwa jibu sahihi halijatolewa au kupatikana.
“Mimi
siyo mwanasiasa wala mtaalamu wa masuala ya siasa lakini kuna hili sakata la
Escrow ambalo juzijuzi Rais amelitolea ufafanuzi, hili nalo linazidi kuwajengea
wananchi hofu, wengine wanakosoa maazimio ya Bunge, wengine wanataka Serikali
itoe maamuzi yenye tija kwa umma, yaani ni hofu tu,” alisema.
Escrow ni fedha za umma
Mchungaji
wa Kanisa la Maombezi, Anthony Lusekelo alisisitizia kuwa fedha zilizochotwa
katika Akaunti ya Tegeta Escrow ni mali ya umma kutokana na taarifa
iliyowasilishwa na PAC bungeni.
Kauli
hiyo inakuja baada ya Rais Kikwete kusema fedha hizo ni mali Kampuni ya IPTL na
zilikuwa Sh202 bilioni na si Sh306 bilioni kama inavyodaiwa.
Akihubiri
katika kanisa hilo jana, Lusekelo maarufu kama ‘Mzee wa Upako’ alisema:
“Niliisikiliza kwa makini mwanzo hadi mwisho (hotuba ya Rais) leo nimeona
niseme machache kwamba fedha hizo ni mali ya umma. Mimi siungani na hao
wanaodai fedha hizi siyo za umma lakini kwa hali hii hakuna jinsi inabidi
tumwachie Mungu maana yeye ndiye atakayeweza kutuvusha kutoka hapa tulipo,”
alisema.
Padri: Viongozi wa dini waliotajwa wajipime
Paroko
wa Parokia ya Mugumu, Serengeti, Padri Aloisi Magabe amesema viongozi wa dini
ambao wametajwa kuhusika na fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow wanatakiwa
kujipima kwa kuwa maadhimisho ya Krismasi yana maana kubwa, hivyo kuwa sehemu
ya watu wanaotuhumiwa si jambo jema.
Akihutubia
katika ibada ya Krismasi, Padri Magabe alisema vitendo hivyo vinazidi kushika
kasi lakini hatua hazichukuliwi.
Alisema
ufisadi ulijichomoza kwa nguvu kwenye Richmond, Epa na sasa Escrow, huku
viongozi wa dini wakihusika, hatua ambayo ni hatari huku akisema juhudi za
kuwashughulikia wahusika huchukua muda mrefu, chanzo kikiwa ni kulindana na
rushwa. “Sina hofu ya kusema waziwazi matukio kama hayo, nimefuatilia magazeti
jinsi wanavyojitetea, bado kuna haja ya kuwa wazi zaidi, maana nchi yetu ni ya
haki na usawa, tutaupataje usawa kwa ‘skendo’ kama hizi?”
Askofu Mkude: Nina imani kubwa na JK
Askofu
wa Jimbo la Morogoro, Telesphol Mkude amesema ana imani kubwa na Rais Kikwete
kwa namna anavyolishughulikia suala la kuwajibisha waliotajwa katika sakata la
Tegeta Escow na kuwaomba Watanzania kumpa muda wa kutosha ili aweze kuendelea
kutoa uamuzi ulio sahihi.
Akizungumza
na waandishi wa habari mjini hapa katika ofisi ndogo ya Kanisa Kuu la Mt
Patrick, Mkude alisema suala la Escrow limepita katika mchakato mrefu na baadhi
ya wameanza kuchukuliwa hatua, wakiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji
Frederick Werema aliyejiuzulu na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo Makazi,
Profesa Anna Tibaijuka aliyefukuzwa.
“Haya
mambo yanaenda na uchunguzi, sidhani kama Rais anaweza kutoa uamuzi pasipo
kujiridhisha, pamoja na kuwapo kamati iliyojiridhisha na uchunguzi na kubaini
uchotaji wa fedha za umma, lakini na yeye kwa nafasi yake anapaswa kujiridhisha
kupitia jopo lake,” alisema Askofu Mkude.
Hofu ya Mungu na ufisadi
Hofu
ya Mungu imeelezwa kuwa ndiyo pekee itakayoondoa wizi na ufisadi miongoni mwa
viongozi na watendaji badala ya kutegemea sheria pekee.
Hayo
yalisemwa jana na Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania
(KKKT), Dk Alex Malasusa wakati akihubiri katika ibada ya Krismasi katika
Kanisa la Azania Front, jijini Dar es Salaam.
Kauli
hiyo inafanana na ile iliyotolewa na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Gloryland
International la jijini Tanga, Manase Maganga. Malasusa
alisema kutokuwapo kwa hofu ya Mungu miongoni mwa Watanzania, ndiyo sababu ya
kuongezeka kwa vitendo vya ufisadi.
“Wakristo
tunahitaji kusimama kwa ujasiri na kukemea mabaya yote katika jamii yetu hata
kama yanafanywa na marafiki zetu kwa kuwa neno linatuagiza kufanya hivyo. Bwana
anasema ‘woga ni dhambi’, hivyo tuwe makini ili kuepuka dhambi hii yenye
madhara kwa watu wengi katika Taifa hili,” alisisitiza Dk Malasusa.


