To Chat with me click here

Monday, October 13, 2014

WAFADHILI: SERIKALI ICHAGUE, BILIONI 900 AU IPTL!



Waziri Mkuu - Mizengo Pinda
NCHI wahisani zimeitaka Serikali kuchagua kati ya kupata fedha za kusaidia bajeti ya mwaka huu au kulinda watuhumiwa wa uchotwaji wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow zilizokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), vyanzo vyetu vya habari vimeelezwa.

Kiasi cha dola za Marekani milioni 125 (shilingi bilioni 200) zinadaiwa kuchotwa kutoka katika akaunti hiyo na kulipwa kwa kampuni ya Pan African Power (PAP) katika mazingira ambayo duru za kibunge pamoja na zile za kibalozi zinaona kwamba yana harufu ya ufisadi.

Vyanzo vya habari hii vimeambiwa kwamba tayari serikali imepelekewa taarifa rasmi kwa maandishi kutoka kwa nchi wahisani zikieleza kwamba hazitatoa fedha hizo za msaada, kiasi cha dola za Marekani milioni 559 (shilingi bilioni 900) hadi pale matokeo ya uchunguzi wa suala hilo kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) yatakapofahamika.

Mmoja wa mabalozi wanaounda kundi la wahisani hao aliyezungumza na vyanzo vyetu vya habari  kwa masharti ya kutotajwa jina, alilithibitishia kwamba tayari wamepeleka taarifa Hazina kuhusu maamuzi yao hayo.

“Ni kweli kwamba tumewapa serikali taarifa rasmi kuhusu uamuzi wetu. Hili jambo kwanza lilikuwa katika hatua ya mazungumzo tu lakini sasa tumeamua kuliweka katika maandishi. Ni matumaini yetu kwamba serikali itatuelewa,” alisema.

Alipotakiwa na mwandishi wa habari hizi kueleza nini hasa kimeandikwa ndani ya taarifa hiyo, Balozi huyo alisema hataweza kusema chochote kuhusu kilicho ndani.
“Mimi ni mwanadiplomasia. Nina haki zangu zinazonilinda. Kilichomo ndani ya taarifa yetu kwa serikali yenu ni kwa ajili ya wana diplomasia pekee. Siwezi kukwambia wewe kilichomo,” alisema.

Juhudi zetu kumpata Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na Naibu wake, Adam Malima, ziligonga mwamba juzi usiku na hadi tunakwenda mitamboni, hawakupatikana. Katika mkutano baina ya wahisani na serikali uliofanyika Novemba mwaka jana katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam, nchi wahisani ziliahidi kuchangia kiasi hicho cha fedha kwa mwaka huu wa fedha.
 
Fedha hizo zilitakiwa kuchangia katika maeneo anuai kama vile upunguzaji wa umasikini, ukuzaji wa ajira na pia katika kusaidia mapambano dhidi ya rushwa. Kundi la wahisani wanaosaidia bajeti ya Tanzania linaundwa na nchi na taasisi 12 tofauti ambazo ni Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), Canada, Denmark, Umoja wa Ulaya, Finland, Ujerumani, Ireland, Japan, Norway, Sweden, Uingereza na Benki ya Dunia (WB).
 
Mtandao huu unafahamu kwamba nchi wahisani hazijafurahishwa na suala la mgao wa fedha hizo zilizowekwa BoT kutokana na ugomvi baina ya kampuni ya kufua umeme ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

Wiki iliyopita, vyombo vya habari viliripoti namna mmiliki wa PAP, Harbinder Sethi Singh, ambaye ni mfanyabiashara mwenye historia ya utata, alivyojipatia mabilioni hayo ya shilingi katika mazingira yenye utata.

Kwa mfano, Singh alimlipa mmoja wa waliokuwa wabia wa IPTL, James Burchard Rugemalira, malipo ya hisa zake alizouza siku chache baada ya serikali kuruhusu alipwe na BoT.

No comments:

Post a Comment