To Chat with me click here

Thursday, August 29, 2013

WATOTO WA KITANZANIA WAKABILIWA NA 'HATARI KUBWA' KWENYE MIGODI YA DHAHABU, YASEMA HUMAN RIGHTS WATCH




Maelfu ya watoto wakiwa na umri wa hadi miaka minane wanafanya kazi kwenye migodi midogo midogo nchini Tanzania wakiwa wanakabiliwa na kitisho kikubwa kwa afya na maisha yao, lilisema shirika la Human Rights Watch (HRW) katika ripoti yake iliyotolewa siku ya Jumatano (tarehe 28 Agosti).

"[Watoto hao] wanachimba na kutoboa chini kabisa, wanabanja mawe, wanafanya kazi chini ya ardhi kwa zamu ya hadi masaa 24, na wanasafirisha na kubeba mifuko mizito ya dhahabu ghafi," ilisema HRW. "Watoto wanakabiliwa na hatari ya kujeruhiwa kwa miamba inapopasuka na ajali za vifaa, na pia madhara ya muda mrefu ya kiafya kutokana na kutumia madini ya zebaki, kuvuta vumbi na kubeba mizigo mizito."

Kundi hilo la haki za binadamu linasema watoto wengi wanaofanya kazi kwenye migodi ama ni mayatima au watoto wengine walio kwenye mazingira hatari ambao wanakosa mahitaji ya lazima na msaada. Wasichana wanaoishi karibu na maeneo ya machimbo pia wanakabiliwa na unyanyasaji wa kingono na shinikizo la kuwa makahaba, HRW iligundua.

"Wavulana na wasichana wa Kitanzania wanamiminika kwenye migodi ya dhahabu kwa matumaini ya maisha bora, lakini wanajikuta wamenaswa kwenye mduara mbaya wa hatari na fadhaa," alisema Janine Morna, mtafiti mwenza wa haki za watoto kwenye HRW. "Tanzania na wafadhili wanapaswa kuwaondoa watoto hawa kwenye migodi na kuwapeleka skuli au vyuo vya mafunzo ya amali."

"Kuwaandikisha watoto kazi hatari za uchimbaji madini ni moja ya aina mbaya kabisa za ajira za watoto chini ya makubaliano ya kimataifa, ambayo Tanzania ni sehemu yake," ilisema HRW.

Tanzania ni ya tatu barani Afrika kwa uzalishaji wa dhahabu na madini hayo ya thamani ni chanzo kikuu cha fedha za kigeni kwa nchi hiyo, ambapo usafirishaji wake nje ya nchi kwa miezi sita ya kwanza ya mwaka 2013 ulifikia dola bilioni 1.8, kwa mujibu wa benki kuu.

Human Rights Watch yenye makao yake makuu nchini Marekani ilifanya utafiti wake ndani ya mwezi Oktoba na Disemba 2012 kwenye maeneo ya migodi kaskazini magharibi na kusini mwa Tanzania, na katika miji ya Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya. Watafiti walitembelea maeneo 11 ya uchimbaji madini kwa ajili ya ripoti hii.

No comments:

Post a Comment