To Chat with me click here

Friday, April 4, 2014

JAJI WARIOBA AVUNJA UKIMYA!


Mwenyekiti wa Tume ya mabadiliko ya katiba Jaji Warioba.

SIKU moja baada ya Ikulu ya Rais Jakaya Kikwete kutoa taarifa ya kejeli na kumsuta Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, mwenyekiti huyo naye ameibuka kujibu mapigo.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Jaji Warioba alisema ameiona taarifa ya serikali kuhusu Tume ya Mabadiliko ya Katiba, lakini ameshangazwa na maudhui na lugha iliyotumiwa na Ikulu dhidi yake.

Majibu ya Jaji Warioba kwa Ikulu ya Rais Kikwete, yalitokana na taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, ambayo ilimwita Jaji Warioba  mnafiki kwa kujifanya hajui ukomo wa tume yake.

Ikulu ilitoa taarifa hiyo baada ya gazeti moja juzi kumkariri Jaji Warioba akidai kuwa tume yake ilifukuzwa kazi na kwamba haikupewa muda wa kuandaa na kuwasilisha nyaraka za kukabidhi ofisi na madaraka na kwamba wajumbe wa tume hiyo waliporwa magari ambayo yamewekwa Ikulu.

Akitoa ufafanuzi wa taarifa ya Ikulu ya juzi, katika taarifa hiyo, Warioba alifafanua hivi:

“Kwanza, tume iliwaheshimu sana waheshimiwa marais wetu. Mafanikio ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba yametokana na jinsi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar  walivyoiunga mkono na kuisaidia tume. Milango yao ilikuwa wazi wakati wote. Wakati wowote mimi kama mwenyekiti nilipoomba kuonana nao nilipata nafasi haraka na tume ilipoomba chochote, pamoja na kuongezewa muda hawakusita. Na wakati wote hawakutoa shinikizo la aina yoyote.  Makatibu wakuu viongozi nao waliisaidia tume kwa kiwango hicho. Heshima yangu na wenzangu kwa waheshimiwa marais na makatibu wakuu viongozi ni kubwa.

“Pili, tume ilikuwa haijamaliza kazi yake wakati inakabidhi ripoti kwa Mheshimiwa Rais. Tume iliendelea na kazi ya kuandaa Randama ya Rasimu, Bango Kitita la Rasimu na maelezo niliyotoa kwenye Bunge Maalumu. Serikali ilijua tulikuwa tunafanya kazi hiyo na nyaraka hizo zilikabidhiwa bungeni siku ya kuwasilisha Rasimu.

Tatu, wajumbe wa tume hawajatoa madai ya kulipwa shilingi milioni mia mbili. Hakuna mjumbe yeyote aliyetoa dai kama hilo na serikali inajua,” alisema Jaji Warioba.

Alisema alichozungumza ni muda wa kuandaa makabidhiano na kuandaa safari ya wajumbe kurudi makwao. Alisema aliwasilisha rasimu Machi 18, 2014, tume ilivunjwa Machi 19, 2014 wakati wajumbe wako Dodoma.


“Pamoja na lugha ya kejeli iliyotumiwa na serikali na kuniita mnafiki, busara ya kawaida ingeonyesha umuhimu wa serikali kujipa muda wa kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani.  Hata kama sheria ilitaja muda wa kuvunja tume bado ilikuwa ni wajibu serikali kufanya mipango ya safari ya wajumbe baada ya kumaliza kazi. Sheria haikuizuia serikali kufanya hilo. Huo ni wajibu wa serikali na utaratibu wa kawaida unaotumiwa na serikali kwa tume zote inazoziunda,” alisema.

Jaji Warioba alimalizia taarifa yake kwa kusema inaonekana Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliwekewa utaratibu tofauti na tume nyingine zilizopita na kuhoji kulikoni?

Katika taarifa yake juzi, Ikulu ilisema kuwa muda wa mwisho wa uhai wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ulijulikana, hivyo  mtu kujitia kwamba ameisahau siku hiyo ni mnafiki wa hali ya juu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, moja ya mijadala mikali ya awali kuhusiana na mchakato wa Katiba Mpya ulihusu lini Tume ya Mabadiliko ya Katiba imalize muda wake.

Ilisema wengine walitaka tume imalize muda wake baada ya kukabidhi Ripoti ya Tume na Rasimu ya Katiba, wengine wakitaka tume baada ya Mwenyekiti wake, Jaji Warioba, kuwasilisha rasimu yake bungeni na hata wengine wakitaka wajumbe wa tume wawe sehemu ya Bunge Maalumu la Katiba.

“Hatimaye, ilikubaliwa kuwa shughuli za tume zingefikia ukomo wake baada ya Mwenyekiti wake kuwasilisha Rasimu ya Katiba kwenye Bunge Maalumu la Katiba kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 31 (1) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.

“Kifungu hicho kinasema kuwa baada ya kuwasilishwa kwa Rasimu ya Katiba kwenye Bunge Maalumu chini ya Kifungu cha 20(3) (cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba) Rais, kwa amri itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali, atavunja tume.

“Mheshimiwa Warioba aliwasilisha Rasimu ya Katiba katika Bunge Maalumu la Katiba Jumanne ya Machi 18, mwaka huu, 2014 na siku iliyofuata Jumatano, Machi 19, 2014 na kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Rais alitia saini tangazo la Serikali la Kuvunja Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

“Hivyo, tokea mwanzo wa mchakato mzima wa Katiba Mpya na utendaji kazi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba hapakupata kuwepo, hata wakati mmoja, shaka kuhusu siku ya tume hiyo kumaliza kazi zake.

“Mwenyekiti wa Tume, wajumbe wote wa Tume, Sekretarieti ya Tume na Watanzania wote waliijua fika siku ya mwisho ya Tume kukamilisha shughuli zake. Kwa mtu kujitia ameisahau siku hiyo leo ni kiwango cha juu sana cha unafiki,” alisema Salva Rweyemamu.

Kuhusu wajumbe kutakiwa kurudisha magari, Ikulu ilikiri kuwa kweli wajumbe wa tume walitakiwa kurudisha Ikulu magari ambayo walikuwa wanatumia kikazi kwa sababu kazi ya tume ilikuwa imemalizika.

Pili, alisema tume ilijua toka mwanzo kuwa baada ya kumaliza kazi yao, magari ambayo walikuwa wanatumia wajumbe na maofisa wa tume hiyo yalikuwa yanatakiwa kupelekwa Dodoma kwa matumizi ya shughuli za Bunge Maalumu la Katiba ambalo linakabiliwa na shida kubwa ya usafiri.

“Serikali ilichukua uamuzi kuwa magari hayo yapelekwe Dodoma kwa sababu lisingekuwa jambo la busara kwa serikali kutumia fedha za umma kununua magari mengine mapya wakati yale ya tume bado yanafaa kufanya kazi na wala hakuna bajeti ya kufanya manunuzi ya magari mapya.

“Hivyo, ni kweli magari hayo yako Ikulu, Dar es Salaam, yakisubiri kukamilika kwa taratibu za kuyapeleka Bunge Maalumu la Katiba mjini Dodoma,” ilisema Ikulu.

Kuhusu madai kwamba tume haikupata muda wa kukabidhi ofisi na nyaraka, Ikulu ilisema hili nalo ni jambo la kutunga na kuzusha tu.
Alisema Jaji Warioba alikabidhi rasmi Ripoti ya Tume na Rasimu ya Katiba kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa Zanzibar Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein, Desemba 30, 2014, mbele ya wananchi katika viwanja vya Ukumbi wa Karimjee, jijini Dar es Salaam.

“Hivyo, toka siku hiyo, Tume haikuwa tena na kazi ya kuandaa Ripoti ama Rasimu kwa sababu kazi hiyo ilikuwa imekwisha na wala isingeweza kuibadili tena Rasimu ya Katiba.

“Kwa maana hiyo, toka Desemba 30, mwaka jana, kupitia miezi ya Januari, Februari mpaka Machi 18, mwaka huu, Sekretariati ilikuwa na muda wa siku 77, zaidi ya miezi miwili na nusu, kufanya maandalizi ya kukabidhi nyaraka na ofisi kwa sababu ilijua kazi yake ilikuwa inamalizika siku ambayo Mwenyekiti wa Tume hiyo angewasilisha Rasimu ya Katiba katika Bunge Maalumu la Katiba.

“Sasa katika muda wote huo, Sekretarieti ya Tume ilikuwa inafanya nini badala ya kuandaa ripoti ya makabidhiano na wakati maofisa wake walikuwa wanaendelea kulipwa mshahara na serikali? Kwa nini walalamike hadharani leo kwa jambo ambalo lilikuwa ni la wajibu wao na wakashindwa kulifanya kwa wakati?” alihoji Salva.

Ikulu katika taarifa hiyo, pia ilijibu madai kwamba wajumbe wa tume walitakiwa  kulipwa kiinua mgongo cha sh milioni 200 kila mjumbe.

Alisema hakuna shaka kuwa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba wamefanya kazi nzuri sana na wanastahili pongezi nyingi za wananchi.

Lakini kama wanadhani kuwa serikali ina uwezo wa kumlipa kila mjumbe kiinua mgongo cha sh milioni 200, basi wanajidanganya kwani wananchi wa Tanzania hawawezi kuelewa maana kabisa ya malipo hayo makubwa kupindukia.

Chanzo: Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment