To Chat with me click here

Friday, April 4, 2014

WANAMTANDAO WA CCM WAMEKULA NYAMA YA MTU




VITA ya urais mwaka 2015 ndani ya chama tawala – CCM, inatajwa kuwa ngumu na kutabiriwa kwamba inaweza kukiathiri kutokana na tabia ya uhasama inayojengeka siku hadi siku.

Inatabiriwa kwamba kuna kila dalili za CCM kupasuka vipande vipande kama tabia ya siasa za fitna na kupakana matope zitaachwa ziendelee kuimomonyoa.
Baadhi ya wanasiasa wanajiona kuwa na haki ya kucheza rafu na kuchafua wenzao kwa gharama zozote ili mradi waonekane hawafai kupitishwa na chama hicho kugombea urais wa mwaka 2015.

Mizizi ya siasa chafu za kupakana matope ina kina kirefu ndani ya CCM na haijaanza juzi, bali ni staili iliyotumiwa na kundi maarufu la mtandao lililomwingiza Rais Jakaya Kikwete madarakani mwaka 2005.

Wapo wanasiasa ambao hadi sasa wanaugulia majeraha yaliyosababishwa kwa makusudi na kundi la mtandao mwaka 2005 kwa lengo la kuhakikisha kwamba hawapati nafasi ya kuteuliwa kuwa wagombea wa nafasi ya urais kwenye mchuano huo uliokuwa na wagombea 11.

Walioumizwa na wanaodaiwa kuendelea kuwekewa macho mawili mawili hadi leo ni wale walioonekana kuwa na ushawishi na nafasi pana ambayo kwa njia moja au nyingine iliibua hofu kubwa kwa kundi hilo na mgombea wao kwa kuamini kwamba wangekuwa kikwazo kikubwa kwao kukidhi malengo yao.

Chini ya kundi hilo, tuliona kashfa mbalimbali zikiwaandama wanasiasa waliokuwa na majina makubwa kwa kuibuliwa mambo yasiyo na vichwa wala miguu.

Katika hili CCM imejiwekea ‘laana’ ambayo lazima itakuja kukigharimu chama hicho, kwani uchafu huo ulipokuwa ukifanyika, chama kilifumbia macho na kujifanya kwamba hakioni wakati wanachama wake wakiumizwa na kundi hilo na chama kukaa kimya bila kutoa tamko lolote.

Baadhi ya vyombo vya habari viligeuka kuwa wakala namba moja wa kundi la mtandao kwa kuhakikisha vinapeleka ujumbe hasi kwa wananchi dhidi ya wagombea walioonekana kuwa tishio kwa kundi hilo la mtandao.

Tuliona namna aliyewahi kuwa  Waziri Mkuu na Katibu wa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU, sasa AU), Dk. Salim Ahmed Salim alivyoandamwa kila kona kuanzia maisha yake binafsi  kwa kudaiwa kumdhulumu na kumnyima haki zake mmoja wa watu waliokuwa wasaidizi wake.

Haikuishia hapo Watanzania wakaaminishwa kwamba Dk. Salim, aliyeipatia nchi hii heshima kubwa kimataifa, si Mtanzania na ndugu zake wana vyeo vya juu huko Arabuni huku yeye akidaiwa kuwa mwanachama wa chama cha Hizbul, kilichouunga mkono utawala wa Sultani huko Zanzibar.

Hayakuishia kwa Dk. Salim, kundi hilo linaloonekana kutaka kutumia tena staili hiyo ya kupakana matope kwenye uchaguzi mkuu ujao lilimwandama aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo,  Frederick Sumaye, kwa kumpaka matope katika masuala mbalimbali likiwemo la kujilimbikizia utajiri wa matrilioni hadi kuwapora wanakijiji ardhi huko Mvomero na Kibaigwa.

Hata hivyo, muda na wakati ulibainisha ukweli wa hayo baada ya kundi hilo kupata walichotaka na ghafla  hatukusikia tena ‘uchafu’ wala  ‘wizi’ wa kina Sumaye.

Hofu na tabia za kundi hili zinatajwa kuanza kuchukua kasi tena wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu ujao. Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuonya kuwa: “Ukila nyama ya mtu huwezi kuacha tabia hiyo, itaendelea.”


Haiyumkini kwamba kundi la mtandao ni kama mtu aliyeonja nyama ya mtu, hivyo ni vigumu kuacha tabia hiyo.

Watanzania watarajie kusikia kwa mara nyingine siasa chafu za kupakana matope kwa gharama ya urais tu, tabia ambayo enzi za Mwalimu Nyerere haikuwahi kujitokeza.

Sumaye anaweza kuwa mmoja wa wanasiasa wanaongoza kukaliwa kooni na wanamtandao kwa kila hatua ya mguu wake unapokanyaga kuanzia pale alipotangaza kugombea urais akiwa bado Waziri Mkuu hadi alipostaafu na wakati huu tunapoelekea uchaguzi mkuu mwaka 2015.

Hadithi ya Sumaye na kundi la mtandao inaweza kufananishwa na uhusiano uliopo kati ya paka na panya ambao hata siku moja hawawezi kupikika chungu kimoja.

Sumaye mwaka 2005 ndiye aliyejikuta akitengenezewa zengwe na kuachwa na ndege huko Tabora na kulazimika kupanda kiberenge kwenda Kigoma kuwahi muda wa kupata wadhamini wa fomu zake za kugombea uteuzi wa kugombea urais.

Sumaye huyu ndiye aliyejikuta akihujumiwa na kundi la mtandao kwenye mkutano mmoja wa hivi karibuni uliofanyika viwanja vya Mnazi Mmoja Dar es Salaam, wakati akiendelea kusubiri watu wajae alishitukia akiambiwa kwamba nafasi yake ya mgeni rasmi imepewa aliyewahi kuwa Waziri wa Viwanda, Nazir Karamagi.

Hilo halikuishia hapo, Sumaye alijikuta akifanyiwa hujuma  kwa kile kilichodaiwa mpango uliosukwa na wagombea urais, wafuasi wa kundi la mtandao wakati alipoalikwa kuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa Chama cha Kuweka na Kukopa (Saccos) huko mkoani Kagera na nafasi hiyo kupewa mtu mwingine katika dakika za mwisho.

Mbali ya hilo, ‘faulo’ aliyochezewa Sumaye na kundi la mtandao kumbariki Waziri Dk. Mary Nagu kwenye kinyang’anyiro cha mjumbe wa NEC Hanang’ na kumwangusha kiongozi huyo aliyemshika mkono na kumlea kisiasa, Dk. Nagu, ni mambo yanayoonyesha nguvu kubwa ya mtandao inayojipenyeza kwa gharama yoyote hata kwa watu wa karibu wa mwanasiasa huyo ili kuhakikisha safari yake kisiasa haifiki mbali.

Tukio la hivi karibuni pia la kukamatwa na meno ya tembo kwa dereva mmoja anayedaiwa kumwendesha kiongozi huyo, lilihusishwa na mikakati ya kumhujumu kiongozi huyo katika kinyang’anyiro cha urais mwaka 2015.

Dereva huyo anadaiwa kutumia gari hilo baada ya kumwacha kiongozi huyo na mkewe uwanja wa ndege waliposafiri kwenda nchini Marekani na yeye kwenda na gari hilo Morogoro.

Hata hivyo, Sumaye mwenyewe alipohojiwa na gazeti moja kutoka aliko safarini Marekani kuhusu tukio hilo alisema: “Sijazungumza chochote, siwezi kusema sasa ni njama za nani. Tukio hili limetokea nikiwa sipo nchini na sihusiki nalo kwa lolote na sina mtu wa kumlaumu, naachia vyombo vya dola  vifanye kazi yake na sheria ichukue mkondo wake…ni uhalifu uliotokea, nasisitiza  dola ifanye kazi yake kama inavyotakiwa.”

CCM inaweza tu kuondoka hapo ilipofikia kama italinda haki za wanachama wake wote na kuacha woga wa kukemea na hata kuwachukulia hatua kali makada wa chama hicho wanaotafuta uongozi kwa gharama za fitna na kuchafua wenzao kwa manufaa yao binafsi.

No comments:

Post a Comment