To Chat with me click here

Friday, April 4, 2014

MKUU WA MILA AMPA BARAKA MGOMBEA CHADEMA CHALINZE!




WAKATI kampeni za uchaguzi mdogo Chalinze zikikaribia ukingoni kwa wapiga kura kumchagua mbunge wao siku ya Jumapili ijayo, Mkuu wa Mila wa jamii ya Wamasai wa Tanga, Morogoro na Pwani, Chifu Tiku Moreto, amempa baraka za ushindi mgombea wa CHADEMA, Mathayo Torongey, akimtaka atimize wajibu wake kwa kutenda haki kwa wote.

Katika tendo hilo lililofanyika juzi asubuhi, kwa faragha katika makazi ya kiongozi huyo wa kijadi, maeneo ya Kibaha Vijijini, kijijini Gumba, Chifu Moreto, alimfanyia dua ya kimila, kisha kumtakia kila la heri mgombea huyo, ambapo alimpatia kitu mfano wa kalamu kama ishara ya uongozi unaosimamia haki.

Kabla ya tendo hilo la kimila, kiongozi huyo wa kimila alitoa nasaha zake kwa msafara wa viongozi wa CHADEMA waliofika kijijini hapo, wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Said Issa Mohamed, ambapo Chifu Moreto alisema pia anamtakia baraka za Mungu, Torongey.

“Mimi kama kiongozi wa kimila, wote mnaogombea ni wa kwangu…yule mwenzako wa CCM naye alikuja hapa…natambua kuwa wewe ni Mmasai mwenzangu, lakini mimi kama kiongozi sina CHADEMA wala CCM, wote ninyi ni wa kwangu. Sina cha chama tawala wala upinzani. Nakutakia mafanikio mema katika uchaguzi huu.

“Ni kweli kuwa CCM imekuwa na udhaifu mwingi, ona hata hapa kwangu wanataka kupauza. Ni kwa sababu tu mimi ningali hai hapa, lakini nasema kuwa mimi kama kiongozi wa mila sina cha chama tawala wala upinzani,” alisema Chifu Moreto kupitia kwa mtafsiri wake.

CHADEMA wazungumza

Mapema akitoa nasaha za msafara wao kwa niaba ya Makamu Mwenyekiti, Mohamed, mmoja wa makamanda wa chama hicho waliofika kwa chifu huyo,  Alphonce Mawazo, alisema kuwa migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa ikisababishwa na uongozi mbovu, unaoweka sera zinazosababisha makundi hayo mawili kukosa haki zao za msingi.

Alisema kuwa katika maeneo mengi, wafugaji wamekuwa kama wakimbizi kwenye maeneo yao, hivyo kujikuta wakigombania ardhi ya malisho ya mifugo yao na wakulima ambao nao wanahitaji maeneo hayo kwa ajili ya kilimo.

Baba yetu chifu…mimi natoka jamii ya wafugaji kama ninyi…ingawa sisi Usukumani tunafuga na kulima pia. Sisi watu wa jamii ya wafugaji mifugo yetu ndiyo benki yetu, mifugo yetu ndiyo M-Pesa zetu, mifugo yetu ndiyo inatupatia wake, mifugo yetu ndiyo kila kitu, sasa kwa sera za CCM, chama kilichoko madarakani sasa, wafugaji miaka michache ijayo tutakosa pa kukimbilia.

“Wakati ule wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, serikali ilijali watu wake, wafugaji tuliletewa mabwana mifugo, wakulima tuliletewa mabwana shamba, leo hakuna tena mambo hayo…badala yake sera wanazotuletea ni kupunguza mifugo, sasa wanataka kuvunja kabisa benki zetu, wachukue hata kilichobaki.

“Kabla ya sera hizi mbovu walianza kwa kupora ardhi…eti leo hii serikali yetu haiwezi kutenga maeneo kwa ajili ya wakulima na wafugaji, lakini inao uwezo wa kupora ardhi kwa ajili ya kumpatia mwekezaji aliyetoka China au Marekani maelfu ya ekari, huku watu wake wakitaabika kwa kukosa ardhi ya kilimo au kufugia, baba yetu nchi hii imekuwa ya hovyo, serikali haijali watu wake tena,” alisema Mawazo.

Naye mgombea Torongey alimshukuru kiongozi wake wa kimila kwa baraka na heri alizomtakia kwenye uchaguzi, akikubali maagizo aliyopewa ya kuwatumikia wananchi wote kwa haki, bila kuwabagua.

No comments:

Post a Comment