To Chat with me click here

Tuesday, January 15, 2013

MAKINDA, JAJI MKUU WATEMA CHECHE


Spika wa Bunge, Anne Makinda akiongea katika mkutano na Tume ya Mabadiliko ya Katiba jana, ambapo mhimili huo wa dola uliwasilisha maoni yake kwa Tume kuhusu Katiba Mpya. Wengine ni watumishi wa Bunge walioongozana naye. Picha Omega Ngole

MIHIMILI miwili ya Dola; Bunge na Mahakama, jana ilitoa maoni yake kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba, huku Spika wa Bunge, Anne Makinda akitaka kuwe na mabunge mawili na kupendekeza kuwa Spika wa Bunge na mawaziri wasiwe wabunge.

Wakati Spika Makinda akitoa maoni hayo, Jaji Mkuu, Mohamed Chande Othman amesisitiza umuhimu wa Mahakama kutoingiliwa na wanasiasa na akapendekeza usawa katika upatikanaji wa haki kwa wananchi wote wa Tanzania.

Makinda akiwa na Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah na viongozi wengine wa mhimili huo, alisema ni muhimu kuwe na Bunge la kuchaguliwa na wananchi na jingine la Seneti litakalotokana na wataalamu mbalimbali na viongozi wa zamani wenye uzoefu na walioitumikia nchi.

Alisema ni muhimu kukawa na aina hiyo ya mabunge pamoja na utaratibu wa wabunge kutokuwa mawaziri ili kulinda demokrasia ya kweli nchini.

“Tunataka Spika wa Bunge asiwe mbunge na pia mawaziri wasiwe wabunge. Wakuu wa mikoa na wilaya nao wasiwe wabunge. Pia tunataka Ibara ya 67 ya Katiba ya sasa ifanyiwe marekebisho ili kulinda demokrasia,” alisema Spika Makinda na kuongeza;

“Ibara hiyo inasema ili mtu awe mbunge lazima atokane na chama cha siasa, sasa Katiba Mpya ikataze kuwavua uanachama wabunge ambao wamechaguliwa na wananchi hata kama wanatokana na vyama vya siasa.”

Spika Makinda alisisitiza kwamba Bunge la Seneti litasaidia kuondoa mambo ya itikadi za vyama bungeni kama ilivyo sasa na kujali maslahi ya taifa katika kila jambo.

Spika asiwe mbunge
Makinda alisema umefika wakati Spika wa Bunge asitokane na wabunge na kwamba kama atachaguliwa kuwa Spika akiwa mbunge, ajiuzulu nafasi moja ili kuweza kulitumikia Bunge kiukamilifu.

Alisema Spika wa Bunge ni mwenye kazi nyingi hivyo ni vyema akapunguziwa majukumu hayo ili kutoa nafasi za kuendesha na kusimamia vizuri shughuli za Bunge.

“Tumependekeza Katiba Mpya itamke kwamba nafasi ya Spika wa Bunge haitatokana na ubunge na kama nafasi hiyo akipewa mbunge, atalazimika kujiuzulu nafasi moja,” alisema na kuongeza:

“Tumependekeza hivyo kutoa nafasi ya maspika wa Bunge kufanya kazi zao kikamilifu kwani nafasi hiyo ina mambo mengi sasa, ni vyema mabadiliko hayo yakatokea ili kuwapa nafasi wananchi wanaowachagua wabunge wao kutumikiwa kikamilifu,” alisema.

Mawaziri wasiwe wabunge

Makinda alisema ili kuhakikisha mgawanyo wa madaraka unaonekana kikamilifu wamependekeza Katiba Mpya ikataze mawaziri kuwa wabunge.

“Tumetaka kuondoa mgongano wa kimadaraka. Sisi tumependekeza kwamba Katiba Mpya ikataze mawaziri kuwa wabunge,” alisema Makinda na kuongeza:

“Mfano ni kwamba mbunge ana shida ya kupata fedha za maendeleo na waziri naye ana shida hiyohiyo katika jimbo lake, lazima atajijali yeye kwanza kwa kuwa ndiye anayepanga bajeti.”

Pia alisema wamependekeza Katiba Mpya ikataze wakuu wa mikoa na wilaya kuwa wabunge na kwamba wabunge wachaguliwe na wananchi tu.

Uhuru wa Mahakama
Jaji Mkuu Othman alisema Mahakama imewasilisha mapendekezo yake 12 kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, moja likiwa ni Katiba yenyewe kuwa msingi wa kutawala nchi.

“Katiba iwe ndiyo kitu bora chenye hadhi ya juu na kinapaswa kuwa chombo pekee cha kuongoza nchi na kusiwepo na mwanya wowote wa mtu au mhimili fulani kuikiuka. Tunataka Katiba ibaki kama dira ya kuongoza nchi kwa kuzingatia utawala wa sheria,” alisema Jaji Mkuu.

Pia alisema Katiba ijayo inatakiwa kusimamia utoaji haki sawa kwa wananchi wote. Jaji Mkuu alisema Katiba haina budi kutambua haki ya wananchi kupata haki katika mambo mbalimbali ikiwamo kuabudu na kuishi.

Katika hoja hiyo ya upatikanaji wa haki, Jaji Mkuu alisema kuna mikoa 12 na wilaya 25 nchini ambako hakuna Mahakama Kuu na Mahakama za Wilaya.

Alisema wananchi wanalazimika kutafuta haki zao kwenye mikoa na wilaya nyingine, tatizo ambalo Katiba Mpya inapaswa kuliondoa ili kuwafanya wananchi wote kuwa na fursa sawa katika kupata haki.

“Pia tumependekeza Katiba Mpya ilinde kwa hali na mali mhimili wa Mahakama kwa kuwa siyo wa kisiasa. Mahakama ni mhimili huru na haufungamani na upande wowote na hiyo ndiyo nguvu ya Mahakama. Isiwe na mambo ya kisiasa, upendeleo au kufungamana na upande mmoja,” alisema Jaji Mkuu.

Aidha, Jaji Mkuu alisema wamependekeza Rais aendelee kuwa mteuzi wa majaji nchini kwa kuwa ndiye mkuu wa nchi. Alisema atafanya uteuzi huo kwa kufuata ushauri atakaopewa na Tume ya Utumishi wa Mahakama na si vinginevyo.

“Katiba ya sasa inasema kuwa Rais atafanya uteuzi kwa kushauriana na Mahakama, lakini sisi tumependekeza asishauriane na Mahakama, bali ateue kwa kufuata ushauri atakaopewa na Tume ya Utumishi ya Mahakama,” alisema.
Alisema haki za binadamu zinapaswa kupanuliwa na kulindwa katika Katiba ijayo. Alisema ilivyo sasa haki za kisiasa na kiraia ndizo zinazoonekana kupewa kipaumbele zaidi kuliko haki nyinginezo kama vile za uchumi na kijamii.

Tume ya Mipango
Kwa upande mwingine, Tume ya Mipango imependekeza Katiba Mpya iwe na ibara itakayoelezea uwajibishwaji na uwajibikaji wa viongozi wa Serikali.

Katibu wa Tume ya Mipango, Dk Philip Mpango alisema wametaka Katiba Mpya iwe na ibara itakayoelezea uwajibikaji wa viongozi wa Serikali pamoja na uwajibishwaji ili kuhakikisha wanawatumikia wananchi ipasavyo.

UNYAMA MKUBWA MBEYA, WAWILI WAZIKWA HAI





WAKAZI wawili wa Kijiji cha Karungu, Kata ya Ivuna, Wilaya ya Momba, mkoani Mbeya wamefariki dunia baada ya kufukiwa wakiwa hai katika kaburi moja na marehemu wanaodaiwa kumuua, tukio linalohusishwa na imani za kishirikina.


Watu hao, Ernest Molela anayekadiriwa kuwa na umri zaidi ya miaka 60 na Bibi Mizinala Nachela ambaye umri wake unakadiriwa kuwa zaidi ya miaka 50, walizikwa wakiwa hai pamoja na aliyekuwa mkazi wa kijiji hicho, marehemu Nongwa Hussein.

Kaimu Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ivuna, Joseph Silwimba aliliambia gazeti hili jana kwa simu kuwa, tukio hilo lilitokea juzi kati ya saa tano na sita mchana, muda mfupi kabla ya maziko ya Hussein.

Kabla ya kufukiwa katika kaburi moja na marehemu, Molela na Nachela kwa nyakati tofauti walipigwa hadi kuzirai na watu wanaodaiwa kushiriki kuchimba kaburi kwa ajili ya kumzika marehemu Hussein.

Silwimba alisema Hussein alifariki dunia Jumamosi saa 10 jioni baada ya kuugua kwa muda mrefu, lakini inaonekana kuwa baadhi ya wakazi wa kijiji hicho walihusisha ugonjwa huo ambao ulisababisha kifo chake na ushirikina.

Jana mchana, Mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD), Momba aliyefahamika kwa jina la Wendo aliongoza operesheni ya kufukua kaburi walimozikwa watu hao, ambao walikutwa wakiwa wameshafariki dunia.

Silwimba alisema miili ya Molela na Nachela ilifanyiwa uchunguzi, kisha kukabidhiwa kwa ndugu na jamaa zao ambao waliifanyia mazishi jana mchana.

Mkasa wenyewe

Kundi la vijana tisa ambao wanadaiwa kuwa ndiyo waliokuwa wakichimba kaburi la marehemu Hussein walianza msako katika Kijiji cha Karungu wakiwatafuta wale waliowatuhumu kwamba ni wachawi na kwamba walihusika na kifo chake.

Silwimba alisema katika harakati zao, walikwenda nyumbani kwa George Hussein ambaye ni kaka wa marehemu lakini hawakumkuta, hivyo kuamua kuchoma moto nyumba yake kwa kuwa walikuwa wakimtuhumu kuhusika na kifo hicho.

“Baada ya kufanya uharibifu huo, walikwenda hadi nyumbani kwa Mzee Molela kisha wakamkamata na kumpiga sana hadi hali yake ikawa mbaya kisha wakambeba hadi eneo la maziko,” alisema na kuongeza:

“Waliporejea kwenye msiba walimkuta Mama Nachela naye wakamkamata na kuanza kumpiga hadi akazimia na yeye pamoja na Molela waliwavuta hadi kwenye kaburi ambako mazishi ya Nongwa (Hussein) yalifanyika.”

Alisema baada ya jeneza kushushwa kaburini, vijana hao wanaodaiwa kwamba walikuwa na hasira walimvuta Molela na kumwamuru kuweka udongo kaburini, lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na hali yake kuwa mbaya.

“Baada ya kushindwa walimsukumiza kaburini na baadaye walimvuta yule mama (Nachela) ambaye naye alikuwa hajitambui na kumtupa ndani ya kaburi halafu wakawafukia wote, kisha wakaondoka,” alisema Kaimu Ofisa Mtendaji huyo.

Alisema mwingine aliyekuwa akisakwa na vijana hao ni Fotino Sichilongwa na kwamba kabla ya kufanya vitendo hivyo, vijana hao walimkamata Mwenyekiti wa Kitongoji, Alfred Kukwe na kumfunga miguu na mikono kwa kutumia kamba, wakamlaza kifudifudi, kisha kumnyang’anya simu yake ya kiganjani ili asiweze kutoa taarifa kokote.

Alisema Kukwe alifunguliwa kamba hizo saa saba na nusu mchana na ndipo alipopiga simu sehemu mbalimbali kutoa taarifa za tukio hilo.

Silwimba alisema baada ya taarifa hizo kusambaa kijijini Karungu, mwenyekiti wa kijiji hicho na ofisa mtendaji wake, walikimbia na kwenda kujificha kusikojulikana wakihofia kudhuriwa na vijana hao.

“Polisi walipofika jana (juzi) jioni walikuta vijana wote waliohusika wamekimbia na hawajulikani walipo maana nyumba zao zimefungwa, hili ni tatizo kubwa maana limesababisha taharuki kubwa hapa kijijini,” alisema.

Wawili mbaroni
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Diwani Athumani alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kulikuwa na taarifa kuwa Molela na Nachela wana undugu. Hata hivyo, habari kutoka kijijini Karungu zimesema hawana undugu wowote.

Kamanda Diwani ambaye aliwashutumu wananchi kwa kujichukulia sheria mkononi, alisema hadi sasa watu wawili wamekamatwa kuhusiana na mauaji hayo.“Tunawashikilia watu wawili ambao tunaamini walikuwa vinara wa tukio hili la mauaji,” alisema Diwani.

Kamanda huyo aliitaka jamii kuacha kujichukulia sheria mkononi na badala yake waheshimu na kutii sheria bila shuruti na kuachana na imani za kishirikina.

“Kila mmoja afanye mambo yake kwa kujiamini. Hii ya kuendekeza imani za kishirikina ina madhara na zaidi ni kurudisha nyuma maendeleo. Jamii inatakiwa kutafuta njia halali kufikisha kero na malalamiko badala ya kutumia vurugu na fujo na kusababisha mauaji.”

NDEGE ATCL YAPASUKA KIOO IKIWA ANGANI



ABIRIA  25 waliokuwa wakisafiri na ndege ya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutoka Kigoma kwenda Dar es Salaam wamenusurika kufa baada ya ndege waliyokuwa wakisafiria kupata ufa katika kioo cha mbele, hivyo kumfanya rubani abadili mwelekeo na kutua kwa dharura uwanja wa  ndege wa Kigoma.

Tukio hilo lilitokea juzi jioni muda mfupi baada ya ndege hiyo aina ya Bombadia Dash 8 kuruka katika uwanja wa ndege wa Kigoma, ikiwa katika safari zake za kwanza, baada ya kusitishwa takriban miezi tisa iliyopita.

ATCL ilisitisha safari zake April 9, 2012 baada ya ndege yake aina ya Dash 8 kupata ajali katika kiwanja cha Kigoma, hivyo Shirika hilo kukosa ndege nyingine. Miezi miwili iliyopita shirika hilo lilinunua ndege mpya.

Kaimu Mkurugenzi wa ATCL, Kapteni Milton Lazaro alisema ilipata hitilafu hiyo dakika 15 tangu iliporuka, baada ya kioo cha mbele kupata ufa.“Ufa ule uliwatisha marubani na waliamua kutua kwa dharura kwa sababu kioo kingeweza kupasuka na kusababisha ajali mbaya na ndege kuanguka,” alisema Lazaro na kuongeza;

“Kawaida vioo vya ndege hupashwa moto ndege inapoondoka na endapo utatokea ufa wowote ni lazima irudi kiwanjani na kama ipo mbali na kiwanja inambidi rubani ateremke chini na kupunguza mwendo.”

Alisema kutokana na hali hiyo, wapo kwenye harakati ya kuifanyia matengenezo ndege hiyo na wakati wowote itarudi kwenye safari zake za kawaida.

Wednesday, January 9, 2013

NGONO INASABABISHA SARATANI YA KIZAZI




UTAFITI mpya wa kitabibu umebaini kuwa saratani ya shingo ya kizazi, inasababishwa pamoja na mambo mengine na ngono kama ilivyo kwa ugonjwa wa Ukimwi, madaktari bingwa wa magonjwa ya maradhi hayo wamesema.

Hayo yalielezwa na daktari bingwa wa uchunguzi wa magonjwa katika Kitengo cha Patholojia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk Henry Mwakyoma na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Dk Crispin Kahesa.

Madaktari hao wametaja mambo mengine yanayoweza kusababisha saratani ya shingo ya kizazi kuwa ni kujiingiza kwenye mapenzi katika umri mdogo, kuolewa mara nyingi, kuwa na wapenzi wengi, kusafisha sehemu za siri kwa bidhaa zenye kemikali na kuzaa mara nyingi.

Katika kiwango cha kimataifa, wastani wa mwanamke kuzaa bila kuwa katika hatari ya kupata ugonjwa wa saratani, ni watoto wanne.

Dk Mwakyoma alisema saratani ya shingo ya kizazi inatokana na aina 40 ya virusi, aina mbili ikiwa ni virusi vinavyosambaa kwa njia ya ngono... “Human papilloma virus (HPV) Squamos cell carcinoma kirusi namba 16 na Adenocarcinoma namba 18, ni kati ya virusi 40 vinavyosababisha saratani ya kizazi na vyenyewe vinachangia tatizo hilo kwa asilimia 70.”

Alisema saratani ya uzazi ndiyo inayoongoza ikilinganishwa na nyingine nchini na asilimia 80 ya wagonjwa, wameambukizwa kwa ngono.

“Saratani hiyo husambaa kwa ngono kutoka mwanamke mmoja kwenda kwa mwingine. Mwanamke mwenye saratani ya kizazi akifanya ngono, mwanamume huchukua virusi na kumwambukiza mwingine atakayefanya naye ngono,” alisema na kuongeza:

“Wagonjwa wengi na wale ambao tayari wana maambukizi, wamekuwa wakikutwa na virusi hawa wa aina mbili ambao wamekuwa wakienezwa zaidi kwa njia ya zinaa. Inawezekana mwanamume akawa ametoa kirusi kwa mwanamke mmoja kwenda kwa mwingine.”

“Hata hivyo, kuna wanaume ambao tayari wameshakuwa na maambukizi ya HPV wanatembea na virusi, hawa tunawaita (high risk sexual male patner) wanaume hawa utakuta kila akioa mke anakufa kwa saratani ya shingo ya uzazi, lakini kamwe virusi hao hawawezi kumwathiri yeye.”

Alisema kuanza ngono mapema nako kunachangia kwa kiasi kikubwa maambukizi ya saratani hiyo, kwani binti anakuwa katika hatari zaidi ya kupata maambukizi mapema na hivyo kuweza kumwathiri mapema zaidi, tofauti na yule aliyeanza baadaye.

“Idadi kubwa ya wanawake wamekutwa na saratani mapema sana, ukilinganisha na umri wao, lakini wengi wao wamekuwa wakikutwa na ugonjwa huu kuanzia umri wa miaka 35 kwenda juu. Hii inamaanisha kuwa walipata maambukizi hayo walipokuwa na miaka 20-25.”

Dk Mwakyoma alisema licha ya hivyo mgonjwa anaweza asitambue tatizo hilo mpaka miaka 10 hadi 15 baadaye ambapo tatizo linajitokeza hadharani.

TENDWA AZUNGUMZIA UCHAGUZI MKUU 2015


Msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa

Msajili wa Vyama Vya Siasa Nchini, John Tendwa amekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM), kusimamisha mgombea wa Urais mwaka 2015 anayekubalika na Watanzania ili kukabiliana na changamoto za kisiasa zinazozidi kuongezeka hapa nchini.

Kadhalika, Tendwa amesema kuanzia sasa ofisi yake itaanza kuvifanyia uchunguzi vyama vyote vya siasa ili kubaini vile ambavyo havifanyi kazi za kisiasa na kuviweka katika madaraja.

Aliyasema hayo jana ofisini kwake jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi wa habari na kuongeza kuwa kwa sasa changamoto za kisiasa hapa nchini zimezidi kuwa kubwa.
Alisema CCM ili kiweze kuvuka katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ni lazima kisimamishe mgombea ambaye anakubalika na wananchi wengi.

Alitoa mfano kuwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimezidi kuwa na nguvu Bara na Visiwani na kwamba hiyo ni changamoto katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Alisema mwaka 2012 vyama vya siasa vilikabiliwa na changamoto nyingi na kwamba sasa ni wakati wa kujiangalia na kujiandaa kwa ajili ya kushiriki uchaguzi mkuu ujao.

Alipendekeza kwamba vyama vinavyokuwa kisiasa na kufanikiwa kupata wabunge vinapaswa kupewa ruzuku ili kuviwezesha kufanya vizuri zaidi.

Akizungumzia siasa za Zanzibar, Tendwa alisema kwa sasa zimebadilika kutokana na muafaka uliofikiwa kati ya vyama vya CUF na CCM na hatimaye kuunda serikali ya umoja  wa kitaifa.

Kuhusu vyama vinavyoibuka katika uchaguzi na kufa baada ya uchaguzi kumalizika, Tendwa alisema mwisho wao umefika na kwamba vitajifuta vyenyewe. Aliongeza kuwa ofisi yake itaviweka vyama katika daraja la 1-3 na vile vitakavyoangukia daraja la nne na sifuri havitakuwa vinaalikwa na kutambulika kama vyama vya siasa.

Aidha, Tendwa aliwaambia wanadishi wa habari kuwa kuanzia sasa mfumo wa chama kupata wadhamini ili kisajiliwe utabadilika na badala ya kupata wanachama 200 kila mkoa katika mikoa 10 sasa watatakiwa watu 1,000 kila mkoa.