To Chat with me click here

Friday, June 20, 2014

MAJINA YA WANAFUNZI WA KIDATO CHA NNE WALIOCHAGULIWA KUJIUNGA KIDATO CHA TANO HAYA HAPA!



Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) imetangaza majina ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano kwa mwaka 2014 ambao waliomaliza kidato cha nne mwaka 2013

Wanafunzi waliochaguliwa wanatakiwa kuripoti kwenye shule walizopangiwa kuanzia tarehe 10 Julai 2014 na mwisho wa kuripoti ni tarehe 30 Julai 2014. 

Aidha, hakutakuwa na mabadiliko ya wanafunzi kubadilishiwa shule walizopangiwa, hivyo wanafunzi wote wanatakiwa kuripoti katika shule walizopangiwa kama inavyoonekana katika matokeo haya.



MAJINA YA WANAFUNZI WALIOCHAGULIWA KUJIUNGA KIDATO CHA TANO MWAKA 2014

 






Maxmillian Kattikiro Blog  inapenda kuwapongeza wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na sita kwa mwaka 2014. Pia tunapenda kuwatia moyo wale wote ambao hawakuchaguliwa kuwa, wasikate tama, bado wanayo nafasi nzuri ya kurekebisha pale ambapo walitereza, na vilevile watambue kuwa elimu haina mwisho.
 

Wednesday, June 18, 2014

POLISI AFANYA SIASA ZA CCM




ASKARI Polisi, Mwashibanda Shibanda wa Wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma, anadaiwa kujihusisha na siasa za Chama Cha Mapinduzi (CCM), suala ambalo ni kinyume na taratibu za jeshi.

Kwa sasa Mwashibanda anasoma katika Chuo Kikuu cha Mzumbe, mkoani Morogoro, na katika kipindi chote anadaiwa kufanya shughuli za kisiasa za wazi.
Mwashibanda amepata kuwa mwenyekiti wa tawi maalumu la CCM Mzumbe, na mwenyekiti wa shirikisho la matawi ya CCM mkoani Morogoro mwaka 2012 – 2013.

Mtoa taarifa wetu amedokeza kuwa akiwa chuoni, anadaiwa kuwakamata wanachuo wenzake kwa kushirikiana na polisi wa kituo cha Mzumbe, hasa wale wenye mirengo tofauti na CCM.

Kwa mujibu wa kumbukumbu mbalimbali za picha ambazo gazeti hili limeziona, askari huyo anaonekana akiwa amevalia sare za CCM zenye rangi za njano na kijani akiwa na makada na viongozi tofauti wa kitaifa.

Askari huyo amewahi kuwa mkimbiza mwenge wa uhuru mwaka 2010 na akiwa mkoani Shinyanga, alikaririwa akimpigia kampeni aliyekuwa mgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete.  Mwashibanda anatajwa kuzitia dosari mbio za mwenge baada ya kuonyesha wazi kuipigia kampeni CCM wakati huo.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu, askari huyo alifanya kituko hicho katika Kijiji cha Wigelekelo, Shinyanga Vijijini wakati wa makabidhiano ya mwenge huo ukitokea Manispaa ya Shinyanga.

Alisema wilaya hiyo ni ya kihistoria, lakini imekuwa ikichanganywa na wanasiasa wanaotangatanga kama kumbikumbi wasiokuwa na makazi.

“Watu wa Maswa mtaonekana kuwa mmepotoka iwapo itaonekana mnampatia uongozi mtu aliyejiunga na kanisa jipya, kwani huyo ana tamaa ya uongozi, hakuna aliyezaliwa duniani kuwa kiongozi hadi kufa bali ni kuachiana zamu, sasa ni zamu ya mwingine,” alisema.

Kauli hiyo, ilionyesha wazi kumlenga Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda, aliyejiondoa CCM na kuhamia CHADEMA baada ya kushindwa katika kura za maoni.

Hili sio tukio la kwanza kwa askari kufanya siasa za wazi za CCM kwani katika mkutano mkuu wa nane wa uchaguzi wa Umoja wa Vijana (UVCCM) Oktoba mwaka 2012 , mmoja wa wagombea wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Stanley Mdoe, alitiwa mbaroni na polisi akibainika kuwa askari wa jeshi hilo.

Askari huyo mwenye namba F 7961 wa cheo cha konstebo, alitoka Kituo cha Polisi Mvomero, Morogoro.

Sunday, June 1, 2014

KASHFA SABA NZITO NCHINI!




Dar es Salaam.
Serikali imepoteza zaidi ya Sh362.9 bilioni kutokana na baadhi ya kashfa kubwa za ufisadi na operesheni mbalimbali zilizoligharimu taifa tangu uhuru.

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini taifa kukumbwa na kashfa mbalimbali za upotevu wa fedha au kuanzisha mipango ambayo utekelezaji wake ulisababisha maumivu kwa wananchi na hakuna awamu ya uongozi wa Serikali iliyokwepa hali hiyo.

Kuanzia awamu ya kwanza ya Mwalimu Julius Nyerere aliyeiongoza nchi toka mwaka 1961 ilipopata uhuru hadi 1986, Rais Ali Hassan Mwinyi (1986-1995), Rais Benjamin Mkapa (1995-2005) na Rais Jakaya Kikwete (2005-hadi sasa), kumeibuka kashfa mbalimbali, saba zikiwa kubwa na kulitikisa taifa.

Kashfa na operesheni saba kubwa zilizotikisa taifa ni pamoja na Operesheni Uhujumu Uchumi, ufisadi katika Mfuko wa Kuwezesha Uagizaji Bidhaa kutoka Nje ya Nchi (Commodity Import Support – CIS) na Kashfa ya Rada.

Nyingine ni ufisadi Akaunti ya EPA, kashfa ya Richmond, Operesheni Tokomeza Ujangili na ile ya uchotaji mabilioni katika akaunti ya Escrow.

Operesheni Uhujumu Uchumi
Mwaka 1984 Serikali ilianzisha Operesheni Uhujumu Uchumi, iliyoongozwa na Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Sokoine ili kutaifisha mali ambazo baadhi ya watu walidaiwa kujipatia kwa njia isiyo halali.

Operesheni hiyo ilishuhudia baadhi ya watuhumiwa wakimwaga fedha mitaani na majalalani, huku wengine wakitupa mali kuhofia kutiwa kwenye mkono wa sheria.

Hata hivyo, katika operesheni hiyo baadhi ya watendaji wa Serikali ambao hawakuwa waaminifu, waliitumia nafasi hiyo vibaya kutaifisha mali za baadhi ya watu, ambao hawakuwa wahujumu uchumi.

Zoezi hilo lilisababisha wananchi kadhaa hasa vijijini kuwekwa ndani na wengine kuachwa maskini baada ya kunyang’anywa mali zao ikiwamo mifugo na mashine za kusaga nafaka, kwa kudaiwa kuwa walizipata kwa njia isiyo halali.

Mfuko wa Commodity Import Support (CIS)
Miaka 24 baadaye yaani mwaka 2008, liliibuka sakata jingine lililokuwa na harufu kubwa ya ufisadi wa mabilioni katika Mfuko wa Kuwezesha Uagizaji Bidhaa kutoka Nje ya Nchi (Commodity Import Support – CIS).

Sakata hilo liliwahusisha baadhi ya wanasiasa, wafanyabiashara maarufu nchini na wizara kadhaa za Serikali ya Muungano na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ). Kupitia mfuko huo, vigogo hao walichota zaidi ya Sh200 bilioni kwa kivuli cha uagizaji bidhaa kutoka nje ya nchi.

Mfuko huo wa CIS, ulianzishwa katika miaka ya 1980, ambapo baadhi ya nchi wafadhili ikiwamo Japan, zililenga kuipatia Tanzania fedha za kigeni za kununulia malighafi, vyombo vya usafiri wa barabara, vifaa vya kilimo, ujenzi na vingine mbalimbali. Mpango huo ulioanzishwa na Serikali uliendelea hadi mwanzoni mwa miaka 2000, ambapo nchi hizo wahisani ikiwamo Japan, Uingereza, Uholanzi, Saudi Arabia, Norway, Uswisi, Ubelgiji, Sweden na Denmark zilikuwa zikiipatia Serikali fedha za kigeni ili kuimarisha sekta za biashara.

Wizara zilizotajwa katika orodha ya wadeni wa CIS ni pamoja na iliyokuwa ya Mawasiliano na Uchukuzi, Wizara ya Kazi, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa Tanzania Bara, wakati Zanzibar zinatajwa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi na Wizara ya Maji.

Rada
Mwaka 2011 Serikali ilikumbwa na jinamizi la ufisadi kwa mara nyingine. Safari hii uliibuka ufisadi wa mabilioni ya shilingi kupitia ununuzi wa rada kuukuu kutoka Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza. Ununuzi wa rada hiyo unatajwa kutofuata taratibu sahihi, uliligharimu taifa Sh29.5 bilioni, wakati gharama halisi ilikuwa Sh21 bilioni.

Serikali ya Uingereza iliamua kurudisha fedha hizo kama chenji, huku ikisisitiza kuwa watuhumiwa wote wa hapa nchini waliohusika na ununuzi wa rada hiyo mtumba, washitakiwe Tanzania au Uingereza kutokana na kubainika dosari kwenye ununuzi huo.

Wakati Uingereza ikitaka watuhumiwa hao wafikishwe mahakamani, mtandao wa Wikileaks unaosifika kwa kufichua siri za ndani ya mataifa mbalimbali duniani, ulibaini kuwepo kwa harakati nchini za kutowafikisha mahakamani wahusika wa ufisadi huo.

EPA
Mwaka 2008 iliibuka kashfa nyingine ya wizi wa mabilioni katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu (BoT), ambapo vigogo kadhaa walitumia mbinu chafu kuchota zaidi ya Sh133 bilioni katika akaunti hiyo.

Katika wizi huo ulioitikisa nchi, wahusika walitajwa kutumia vivuli vya siasa katika kupitisha nyaraka bila kufanyiwa uhakiki wa nyaraka hizo.

TANZIA: MAMA MZAZI WA ZITTO KABWE AFARIKI DUNIA!


Mhe. Zitto akiwa na mama yake mzazi B. Shida Salum enzi za uhai wake,kabla mauti kumkuta leo asubuhi katika hospitali ya AMI iliyopo Masaki,, jijini Dar Es Salaam.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Tanzania (CHAWATA), Bi Shida Salum, na Mjumbe wa kamati Kuu ya chama cha CHADEMA, aliyekuwa amelazwa chumba cha Wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU), katika Hospitali ya AMI, Masaki jijini Dar, ameaga Dunia.



Kwa habari zilizotufikia katika vyombo vyetu vya habari, vimesema kuwa, mama wa Zitto alifariki leo asubuhi katika hospitali hiyo ya AMI baada ya kulazwa hapo kwa muda ambapo alikuwa akisumbuliwa na ungonjwa wa KANSA mpaka mauti ilipomkuta asubuhi ya leo. Bi. Shida Salum, mbali na kuwa amekuwa akitibiwa AMI  mpaka umauti ulipomkuta, lakini vilevile amneshawahi kwenda kutibiwa ng’ambo ya nchi kama vile India bila mafaniko. 


Habari hizi za kufariki kwa mama yake Zitto zilielezwa na Zitto Kabwe mwenyewe kupitia mtandao wake wa twitter, akiripoti kuondokewa na mzazi wake huyo.

Watu na baathi ya viongozi mbalimbali wametoa salamu zao za rambi rambi kwa Mhe. Zitto kama ifuatavyo:-


Bernard Membe:
Zitto Kabwe pole sana kwako na ndugu kwa msiba huu mzito. Tunawaombea subira na Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi, Amina. 

William Ngereja:           
Nimepokea taarifa za msiba wa Bi. Shida Salum (mama mzazi wa Zitto Zuberi Kabwe) kwa masiitiko makubwa. Nawapa pole familia nzima ya ndugu yetu Zitto katika kipindi hiki cha majonzi, Mwenyezi Mungu awape wepesi na pia, natoa pole kwa wote walioguswa na msiba wa George Otieno aliyefariki jana, tuendelee kuziombea familia hizi na nyingine zenye misiba ili wapate faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu ambaye ndiye mfariji mkuu. 

Maxmillian Kattikiro (TEDA):
Napenda kuungana na wengine wote walionitangulia kutoa salamu za pole kwa ndugu, rafiki, jamaa, kamanda na mpambanaji mwenzutu, Mhe. Zitto Ruyagwa Kabwe pamoja na CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA), kwa kuondokewa na Mama yake mzazi Bi. Shida Salum, na mjumbe wa Kamati Kuu CHADEMA. Katika wakati huu mgumu na majonzi, tunakuombea ili Mungu aendelee kukutia nguvu na kukuongoza vyema. Tunaungana nawe katika kuomboleza msiba huu na Mwenyezi Mungu ampumzishe kwa amani mama yetu, Amina.

David Kafulila:
Nimepokea kwa huzuni kubwa msiba wa mama yetu Bi Shida Salum. Ni mama mzazi wa zitto. Alinipenda sana na nilikuwa karibu nae sana wakati wa uhai wake. Aliugua kwa muda kansa. Akapata matibabu india kwa muda bila mafanikio sana na akaendelea kupata matibabu akiwa Dar kupitia hospitali bora kabisa ya AMI. Nitambuka kwa ukaribu wangu kwake. Alipenda kuwa karibu na mimi. Alikaa namimi mpaka usiku mwingi wa sanane tunazungumza.alikuwa mama mcheshi, mwenye upeo na mwenye kufikiri kimkakati siku zote. Alipenda kufunga na kusali. Nimepoteza kitu kikubwa kwa mama yetu huyu. Mapenzi alokuwa nayo kwa watu wote. Naamini ametangulia kwa Mungu wa upendo. Na hakika tutamkuta tufurahi nae pamoja siku moja.

Halima Mdee:
Pole sana mh. Zitto kabwe, kwa kufiwa na mama yako mzazi Shida Salum,
Najua hilo ni pigo kubwa katika maisha yako , lakini mungu amempenda zaidi, nakuomba uwe na moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu, yote ni mipango ya Mungu, cha msingi ni kumuombea ili Mungu, aweze kumpokea mahari pema peponi amin. R.I.P Shida Salum.