To Chat with me click here

Wednesday, May 30, 2012

HOTUBA YA NAIBU KATIBU MKUU CHADEMA Ndg. ZITTO KABWE KWA WANACHADEMA WANAOISHI MAREKANI – MARYLAND, VIRGINIA NA DC

 
Tumekutana leo wakati ambao Taifa letu lipo katika mpito wa mambo mengi sana. Kufuatia shinikizo kubwa kutoka chama chetu cha CHADEMA na asasi nyingine za kiraia ikiwemo viongozi wa dini, tupo katika mchakato wa kuandika upya katiba ya nchi yetu. Lakini pia kuna muamko mkubwa sana wa haki za kiraia na haki za kisiasa katika Taifa letu hivi sasa. Watanzania, kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya nchi yetu, wameamka na kutaka mabadiliko ya kisiasa na hasa kutaka kabisa uongozi mpya wa nchi kutoka chama kingine tofauti na chama kinachoongoza hivi sasa. Huu mpito pia, Mpito wa kutoka chama kimoja hodhi kwenda mfumo wa kweli wa vyama vingi vya siasa. Watanzania wameamka sana kujua rasilimali za nchi yao na kutaka kutokomeza rushwa na ufisadi na matumizi mabaya ya utajiri wa nchi. Huu ni mpito wa kutoka viongozi wanaojali maslahi yao binafsi na kwenda kwa viongozi wawajibikaji na wenye uchungu wa kuendeleza nchi yetu na watu wake.

Mpito wowote unapaswa kuongozwa vyema. Unapaswa kushirikisha wananchi wote bila kujali wapo sehemu gani ya Dunia. Chama chetu kipo mstari wa mbele kuongoza mpito tulionao Tanzania. Licha ya kuongoza juhudi za kuwa na Katiba mpya itakayohakikisha HAKI na Wajibu wa Watanzania, lakini pia tumekuwa tukiendelea kupambana na rushwa na ufisadi. Pia tumekuwa tukiendelea kuhakikisha utajiri wa nchi yetu unatumika kwa manufaa ya Watanzania. Hatujatetereka hata kidogo na hatutateterekea kuhakikisha Watanzania wanakuwa na Taifa lenye demokrasia iliyokomaa, lenye maendeleo na ustawi wa watu wake (Developmental Democratic State).

Licha ya kwamba tupo Upinzani, lakini hatua mbalimbali tulizochukua zimeleta mabadiliko makubwa katika nchi yetu. Kuanzia vuguvugu la Buzwagi mpaka kuibuliwa kwa maskandali ya EPA na mpaka kutajwa kwa orodha ya Mafisadi nchini pale MwembeYanga. Hata hivi karibuni juhudi za Bunge kutaka Uwajibikaji Serikalini zilizoongozwa na CHADEMA zimeleta mabadiliko. Inawezekana mabadiliko hayo sio kama tutakavyo, sio kamili, lakini ni hatua ambayo tumepiga. Tutaendelea kama chama cha siasa sio tu kusema na kupiga kelele kuhusu uoza uanaofanyika Serikalini (maana ndio kazi yetu kikanuni) lakini pia kutoa masuluhisho ya matatizo ya nchi yetu na kusukuma kupitia Bunge mabadiliko chanya yanayotakiwa ili kuleta mabadiliko nchini.
Ni matumaini yangu kwamba Watanzania wanaoishi nje ya nchi, kokote walipo watashiriki pamoja nasi katika vuguvugu (movement) hili la kuleta mabadiliko katika Taifa letu. Hampaswi kukaa na kutazama, bali mnapaswa kushiriki kikamilifu maana hii ni nchi yetu sote. Ni wajibu wa kila mmoja wetu kuhakikisha nchi yetu inakuwa na demokrasia na ustawi wa watu wake.

Hali ya Uchumi wa Nchi
Tumekuwa moja ya nchi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi zaidi duniani. Katika kipindi cha muongo mmoja uliopita uchumi wa Tanzania umekuwa ukikua kwa wastani wa asilimia 6. Kazi hii ya ukuaji ukilinganisha na kiwango cha ukuaji wa idadi ya watu (ambacho ni 2.8%) ingeweza kupunguza umasikini kwa zaidi ya 50% katika kipindi hicho. Hata hivyo Umasikini Tanzania umebakia ni mkubwa ambapo zaidi ya Watanzania 37 katika kila Watanzania 100 hawana uhakika wa mlo mmoja kwa siku. Idadi ya Watanzania masikini wa kutupwa (wenye kipato cha chini ya tshs 500 kwa siku) imeongezeka kutoka watu milioni 12 mwaka 2007 mpaka watu milioni 15 mwaka 2011. Ukitaka kujua wingi huu ni wa kiwango gani, chukua idadi ya watu wa Nchi ya Botwasana, Namibia, Swaziland na Lesotho haikaribii idadi ya Watanzania wenye mashaka ya mlo mmoja kwa siku. Idadi ya watu wa Denmark, Netherlands, Norway na Uholanzi kwa pamoja ndio sawa na idadi ya Watanzania masikini. Kwa nini?
Ni kitendawili. Ni nadra kukuta uchumi unaokua kwa kasi kama wetu ukizalisha masikini zaidi. It’s a paradox of a fast growing economy and increasing poverty. Kwa miaka kumi ambayo tumeiangalia (2000 – 2010) tumeshuhudia kwa dhahiri kabisa kushindwa kwa sera za kuondoa umasikini zinazotekelezwa na Serikali ya CCM.

Masikini wa Tanzania wapo vijijini zaidi. Uchumi wa vijijini kwa kipindi cha muongo mmoja umekua kwa wastani wa asilimia moja tu. Flat lining. Kwa hiyo uchumi unaokua hivi sasa sio uchumi wa Watanzania bali ni uchumi wa watu wachache kwenye sekta chache kama madini, mawasiliano na ujenzi. Watanzania walio wengi walioko vijijini wanaendelea kuandamwa na ufukara bila juhudi mahususi za kuwasaidia. Tumesema na tunarudia kusema kwamba ni lazima kubadili mwelekeo wa mipango yetu na kujikita kwenye maendeleo vijijini. Kama chama tunaendelea kusema jambo hili ndani ya Bunge na pia kuwaelimisha wananchi kwenye mikutano yetu ya hadhara.
Mfumuko wa Bei umefikia kiwango cha juu sana cha 19% na hivyo hata mikopo katika mabenki imekuwa ghali hadi kufikia riba ya 23% na zaidi. Mfumuko wa bei unaongozwa na bei ya vyakula. Katika hali ya kawaida, kupanda kwa bei za vyakula kungemnufaisha mkulima lakini hali sio hiyo Tanzania. Mkulima bado anauza mazao yake kwa bei za vijijini ambazo ni ndogo na zinaamuliwa na wachuuzi wa mijini. Lakini mkulima huyu anaponunua bidhaa za matumizi yake kama sukari, mafuta ya taa, nguo nk ananunua kwa bei za mijini ambazo zimeathiriwa vikali na mfumuko wa bei. Hivyo mfumuko wa Bei unamuathiri zaidi mwananchi masikini kabisa. Serikali imekuwa mlalamikaji kama wananchi wengine. Mfumuko wa Bei utapungua kwa kuongeza uzalishaji wa chakula, kuimarisha miundombinu ya vijijini na kupunguza gharama za Nishati kama hasa Umeme. CHADEMA inaendelea kuisukuma Serikali kuchukua hatua ili kupunguza makali ya maisha kwa wananchi. Hatua za muda mfupi zihusishe nafuu ya kodi kwenye bidhaa zinazotumiwa na wananchi kwa wingi.

Hata hivyo bado matumizi ya Serikali ni makubwa mno kwenye masuala ambayo hayana uhusiano na kuendeleza watu. Bado bajeti ya posho mbalimbali, safari za nje na hata matumizi makubwa ya magari ya serikali ni kubwa mno kulinganisha na hali yetu ilivyo. Katika matumizi haya pia kuna ufisadi mkubwa sana. CHADEMA inaendelea kuanisha masuala haya na kukemea na kuchukua hatua pale inapobidi.
Uwezo wetu wa kukusanya mapato ni changamoto kubwa. Mapato mengi yanapotea kama misamaha ya kodi ambayo sasa imefikia tshs 1.3trn kwa mwaka. Mapato mengine hayakusanywi kwa sababu ya ukwepaji kodi uliokithiri. Kodi kwenye Sekta ya Madini imekuwa ni mjadala wa muda mrefu sana. Sheria ya madini ya mwaka 1998 na Sheria za Fedha ya mwaka 1997 ziliweka mfumo wa kinyonyaji kabisa ambao ulikuwa unafaidisha makampuni ya uchimbaji madini kuliko Taifa. Sheria mpya ya madini ya mwaka 2010 ambayo ilitokana na kazi kubwa tuliyofanya ndani ya Bunge pamoja na Mashirika yasiyo ya kiserikali imeweka mfumo bora zaidi. Hata hivyo makampuni ya Madini yaliweka mgomo kwenye sheria mpya kwa kukataa kuanzisha miradi mipya na hata kukataa kuhamia kwenye sharia mpya. Sheria mpya inataka Serikali kuwa na hisa kwenye kila mgodi, hisa za kampuni za madini kuorodheshwa katika Soko la hisa la Dar es Salaam na kulipwa kwa mrahaba mpya wa asilimia 4 kwa kanuni mpya ya kukokotoa mrahaba (from Netback Value to Gross value) ambayo ingeongeza mapato ya Serikali maradufu. Kwa miaka Serikali imekuwa inapoteza mapato kwa kutotekelezwa kwa sharia mpya. Nimesikia kuanzia mwezi huu kampuni ya Barrick imeanza kulipa mrahaba mpya. Tutataka maelezo ya Serikali kuhusu kampuni nyingine na pia mrahaba wa miaka ya nyuma. Ni lazima Serikali ihakikishe nchi inafaidika na rasilimali zake.
Tunaenda kwenye Uchumi wa Gesi Asilia. Makampuni mawili makubwa duniani yamegundua Gesi Asilia nchini kwa kiwango kikubwa sana. Hivi sasa Tanzania ina Utajiri wa Gesi ulitothibitishwa wa 20TCF na makadirio yanaonyesha kuwa tutafika 85TCF katika kipindi kifupi sana. Bado kuna meneo yanaendelea kufanyiwa utafutaji kutokanana vitalu vilivyogawiwa. Hata hivyo hatuna Sera na Sheria ya kusimamia vema sekta hii na hasa yenye kuhakikisha Uwazi na Uwajibikaji. Hatuna pia Sheria ya kusimamia mapato yanayotokana na Gesi Asilia (Petroleum Revenue Management Act). Hatutaki kurudia makosa yaliyofanyika kwenye sekta ya Madini. Tunataka Gesi Asilia itumike kwa maendeleo ya watu wetu.

Tumependekeza kwamba Vitalu vipya vya kutafuta mafuta visitolewe kwa sasa (moratorium) mpaka hapo Sera mpya, Sheria mpya na mfumo bora wa matumizi ya Fedha zitakazotokana na Mafuta na Gesi ziwepo. Pia shughuli za utafutaji katika vitalu vya sasa zitaongeza thamani ya vitalu vijavyo na hivyo nchi kufaidika zaidi. Tumependekeza pia kwamba ni lazima kuweka mfumo mzima wa uwazi na uwajibikaji katika sekta ili kujipanga vyema na kuepuka yaliyowakuta wenzetu wenye utajiri kama huu ambao uligeuka balaa. Tatu tumependekeza kusomesha Watanzania kwa ngazi zote. Mafundi mchundo kupitia VETA na Mafundi wa kati kupitia Vyuo vya Ufundi. Muhimu zaidi tunataka kijengwe Chuo Kikuu kikubwa Mtwara chenye Kampasi Lindi ambacho kitakuwa ni kituo cha kufundisha sio watanzania tu bali Waafrika wengine kuhusiana na masuala haya. Ujenzi wa Chuo Kikuu Mtwara unapaswa kuanza mara moja bila kuchelewa.
Kutokana na uzoefu tuliupata katika sekta ya Madini na kupitisha sharia mbaya Bungeni, tunaona kwamba suala la Gesi tukabe kila mahala ili kuhakikisha nchi inafaidika. Historia inatuonyesha kwamba Nchi nyingi za Kiafrika zenye utajiri wa Gesi na Mafuta hazina demokrasia, zimegubikwa na uvundo wa ufisadi na watu wake ni masikini. Tunataka kuonyesha Dunia kwamba inawezekana kuwa nan chi ya Kiafrika yenye utajiri mkubwa wa Mafuta na Gesi na ikawa ya kidemokrasia, isiyo na ufisadi na yenye watu wenye ustawi. Sio kazi rahisi lakini tumedhamiria. CHADEMA haitakaa tu kuona utajiri wan chi unatapanywa hovyo. Tumesema na kusimamia kwenye Madini, tunatoa mwongozo kwenye Mafuta na Gesi.

Katiba
Ninajua Watanzania mnaoishi nje mna shauku kubwa ya kujua ushiriki wenu na hatma yenu kwenye Katiba mpya. Kwa muda mrefu mmekuwa mkishawishi haki ya kupiga kura, haki ya kuwa na uraia zaidi ya mmoja (Dual Nationality) na hata namna gani mnashiriki katika kujenga uchumi wa nchi.
Kwanza nataka niwapongeze kwa kuchukua uamuzi mzito wa kuondoka nyumbani kuja ughaibuni kutafuta maisha au maarifa au vinginevyo. Nawapongeza zaidi kwa juhudi mnazofanya kusaidia familia zenu nyumbani, vijiji vyenu na hata Taifa kwa ujumla. Takwimu zilizotangazwa na Benki Kuu ya Tanzania zinaonyesha kwamba Watanzania mliopo nje ya Tanzania mlituma nyumbani fedha (remittances) zaidi ya Dola za kimarekani 350 milioni mwaka 2011. Hii ni sawa na asilimia 5 ya mapato yote ya Fedha za kigeni zilizoingia Tanzania mwaka huo na ni zaidi ya Fedha za kigeni zilizoingizwa na Chai, Kahawa, Pamba na Korosho kwa ujumla wake. Kwa hiyo ‘Diaspora’ ni sehemu muhimu sana ya Uchumi wa Taifa ni muhimu Dola iwawekee mazingira mazuri ya kuweza kufanikisha mambo yenu huku ili mshiriki vema maendeleo ya nchi yetu.

CHADEMA tunatambua umuhimu wenu hata kama msingekuwa mnatuma fedha nyumbani. Ninyi ni Watanzania na ni jukumu la Dola ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwalinda popote mlipo duniani. Mtakumbuka mwanzo mwa miaka ya 2000 kulikuwa kuna ‘petition’ ya kudai Uraia wan chi mbili kwa Watanzania. Dkt. Willibrod Slaa alikuwa ni mmoja wa Wabunge waliokuwa wanauliza maswali Bungeni kuhusu jambo hilo. Wengi tuliweka sahihi katika ‘petition’ ile ambayo ilianzishwa na Watanzania wanaoishi nje. CHADEMA inaunga mkono haki ya Watanzania kuwa na uraia wa nchi nyingine. CHADEMA inataka suala hili lifikie mwisho kwenye mjadala wa Katiba. Kuna watu wanasema sio uzalendo Mtanzania kuchukua uraia wa nchi nyingine. Ninasema sio uzalendo pia kuacha raia wako wanateseka nchi nyingine kwa sababu tu wamechukua uraia wa huko au wanashindwa kuchukua uraia wa huko. Sheri zetu za Uraia ni gandamizi hasa kwa wanawake wa Tanzania. Tumepoteza dada zetu wengi sana na watoto wao kwa sababu wakiolewa na wageni watoto wao hawana haki ya kuwa raia. Wakinyanyaswa na wageni na kutaka kurudi nyumbani wao na watoto wao wananyanyaswa pia kwao. Haikubaliki na tutakabili suala hili kwa nguvu zetu zote. Tunataka Watanzania walioko nje wapate kila aina ya msaada kutoka Dola yetu ili wafanikiwe.
CHADEMA inataka pia Watanzania waliopo nje waruhusiwe kupiga kura nyakati za uchaguzi. Ni suala la ushamba tu kuendelea kujadili jambo hili la uwazi kabisa. Kuna teknolojia za kisasa kabisa kuhakikisha watu wanapiga kura kokote walipo. Mwaka 2004 Chama rafiki cha CHADEMA kutokan Msumbiji RENAMO kiliniteua kuwa wakala wa kura katika kituo cha Ubalozi wa Tanzania Msumbiji uliopo Dar es Salaam. Raia wa Msumbiji wanaoishi Tanzania wanapiga kura nje, seuze Tanzania? CHADEMA inawahakikishia kulisimamia jambo hili.

Katika mkutano wa Bajeti ujao Bajeti Kivuli itazungumzia namna ya kuimarisha uwekezaji wa Watanzania wanaoishi nje katika uchumi wa nchi. Siku zote tunazungumzia mitaji kutoka nje kwa maana ya ‘Foreign Direct Investments’ peke yake na kwa kweli tunasahau kwamba kuna ‘Diaspora Direct Investments’. Tumetoa vivutio vingi sana kwa Wawekezaji kutoka nje. CHADEMA inakwenda kupendekeza kuwepo kwa vivutio vya kikodi na kirasimu kwa Watanzania wanaoishi nje wanaotaka kuwekeza nyumbani. Ninawashawishi muangalie namna ya kujikusanya na kuwa na ‘Investments Funds’ ili kununua ‘equties’ kwenye miradi mbalimbali. Uwekezaji Tanzania unalipa sana (Return on Investments goes up to 25%) kwenye baadhi ya maeneo. Huduma katika sekta zinazoinukia kama Mafuta na Gesi ni eneo ambalo mnapaswa kuliangalia tusiachie wageni tu. Mnakumbuka wakati wa mwanzo wa Sekta ya Madini hata huduma za kufua nilikuwa zinatolewa na kampuni kutoka Australia! Mtwara hakuna vyumba vya kutosha vya mahoteli na hata nyumba za kupanga, angalieni maeneo haya maana Mtwara is booming. Sisi kama wanasiasa jukumu letu ni kuwawekea mazingira mazuri. Ninyi mnapaswa kuzileta hizo Dola kidogo mpatazo nyumbani na kuwekeza kwenye maeneo yatakayozalisha ajira na hivyo kuondoa umasikini kwa ndugu zenu. Ninaamini mtachukua changamoto hii na kuangalia namna ya kuitekeleza. Wenzetu kutoka Ethiopia na Kenya wanafanya hivi.

Mjadala wa Katiba pia na hatimaye Katiba mpya itaamua hatma ya Muungano wetu. Muungano pekee katika Bara la Afrika ambao umedumu na umeonyesha nia ya Mwafrika kukataa mipaka ya kikoloni. Kuna Watu wanaona Muungano huu haina manufaa hivyo uvunjwe. Kuna watu wanaona ni bora kuurekebisha ili uweze kufaidisha Jamhuri mbili zilizoungana. Mchakato wa Katiba mpya kupitia Tume ya Katiba ambayo CHADEMA tumeshiriki, ni nafasi ya kuandaa mustakabali wa Tanzania ijayo. Tanzania tunayoitaka kwa miaka mingine hamsini, mia moja au hata alfu moja. Watanzania wawe huru kusema wanataka Muungano au hawautaki, wanataka Muungano wa namna gani na wanataka Tanzania ya namna gani.
Ni Haki ya Watanzania wanaoishi nje kutoa maoni yao kuhusu Katiba. CHADEMA inakusudia kwanza kukusanya maoni ya wanachama wake walioko nje kuhusu Katiba lakini pia kuitaka Tume ya Jaji Warioba kuja huku kukutana na Watanzania na kupata maoni yao. Ni Haki yenu kutoa maoni na ninawaomba mtumie haki yenu vizuri. Mtupe uzoefu wa nchi nyingine ambazo mmeishi na kuweza kuona ni vipi tutaimarisha Dola imara ya Kidemokrasia yenye kuleta ustawi wa watu wake.
Msimamo wa CHADEMA ni Muungano wa Serikali Tatu. Hata hivyo katika mchakato tulio nao sasa wanachama wa CHADEMA wana uhuru wa kutoa mawazo mapya na kuboresha sera hii ya CHADEMA kuhusu Muungano. Muwe huru kabisa kutoa maoni yenu.

Haki na Wajibu
Watanzania mnaoishi nje mna haki na lazima Dola ilinde haki hizo lakini pia kama Watanzania mna wajibu kwa nchi yenu. Ni wajibu wenu kushiriki kikamilifu katika kuimarisha demokrasia nchini. Sisi wenzenu tumejitoa muhanga katika eneo hili. Tumejenga taasisi zinazoitwa vyama vya siasa kwa zaidi ya miaka ishirini sasa. Hatuchoki lakini tunahitaji ushiriki wenu. Jambo hili sio kwa wanachama wa CHADEMA peke yake bali pia hata wanachama wa vyama vingine mnaoishi hapa Marekani.
Hutakuwa mwanachama bora wa CCM kwa kufanya kazi ya kuwachoma Watanzania wenzako ambao ni wana mageuzi kwa viongozi kila wanapokuja kwenye ziara nje ya nchi. Utakuwa mwanachama mzuri wa chama chako iwapo utawaambia viongozi ukweli wa mambo na namna bora ya kuongoza nchi yetu.
Hamuitendei haki Tanzania kwa kusemana, kusingiziana, kutetana na hata kugombana.  Wakati mwingine unapoona mijadala ya watu kwenye mitandao ya kijamii unasinyaa. Unajiuliza sasa kama hawa ndio wapo kwenye mwanga sisi tulio kwenye giza inakuwaje?
Fanya kazi. Furahia maisha. Lakini kumbuka kuna nchi yenye barabara za mashimo, yenye giza muda mwingi wa mwaka kuliko mwanga, yenye umasikini, yenye viongozi wasiwajibika na wala rushwa. Ni nchi yako. Usiseme hii ni kazi ya kina Zitto, Slaa, Mbowe, Nassari, Leticia na Msigwa. Kila mtu ana wajibu wa kufanya kuisogeza mbele nchi yetu. Timiza wajibu wako kwa namna unavyoona inafaa.
Nkrumah once said ‘organise, don’t agonise’ narudia hivyo kwa Watanzania mliopo Marekani. Organise for your motherland.

Tanzania yenye usawa wa fursa
Nimalizie kwa stori yangu. Nilizaliwa katika umasikini wa kutisha kama Watanzania wengi wa vijijini. Nimekwenda shuleni bila viatu na wakati mwingi tumbo likiwa tupu ama nimekunywa uji wa unga wa Yanga uliotiwa chumvi. Darasani nilikuwa ninasoma na watoto wa watu wote wenye mamlaka pale mjini Kigoma. Wote tulikuwa tunafundishwa na Mwalimu huyo huyo na tunakaa darasa hilo hilo, tunapata elimu hiyo hiyo. Leo mimi ni msomi mwenye shahada ya Uzamili na Mbunge nawakilisha watu wa kwetu. Wenzangu wengi pia wanaendesha maisha yao na wengine wapo hapa Marekani wakitafuta maisha.
Leo mtoto wa masikini Tanzania hapati elimu anayopata mtoto wa mwenye uwezo. Mtoto wa masikini hakutani na mtoto wa mwenye uwezo. Wanasoma shule tofauti. Wanafundishwa na walimu tofauti. Hawachezi pamoja. Wote wakimaliza kidato cha Sita, mtoto wa mwenye uwezo ana nafasi kubwa zaidi ya kupata mkopo kwenda Chuo Kikuu kwa sababu amesoma shule bora zaidi hivyo anapata daraja kubwa zaidi la kupewa mkopo na Bodi ya Mikopo.

Wakati nasoma, kikwazo kilikuwa uwezo wako tu kichwani. Hivi sasa kikwazo ni kipato pia. Tofauti ya kipato nchini ni kubwa lakini sisi wanasiasa hatuioni. Wakati wenzetu wanajiandaa kufaidika na ‘demographic dividend’ kwani watoto wao wanapata elimu bora, sisi hata hatujiandai na ‘demographic Bomb’ litakaloletwa na kundi kubwa la vijana wasio na elimu wala ujuzi.
Shiriki kurejesha Tanzania yenye kutoa fursa kwa kila raia bila kujali hali yake ya kipato. Shirika kurejesha Tanzania yenye Usawa kwenye fursa na yenye demokrasia. Jiunge na CHADEMA tuendeleze mapambano.
Nawashukuru kwa kunisikiliza

Zitto Kabwe, Mb
Naibu Katibu Mkuu CHADEMA

Thursday, May 24, 2012

JE WAIJUA TANZANIA YA KESHO?

Miaka michache iliyopita tumekuwa tukishuhudia jinsi Bunge letu tukufu lilivyokuwa likihoji na kutaka kujua juu ya mikataba mibovu ambayo baadhi ya viongozi wetu wa Serikali wamekuwa wakiingia na mashirika, makapuni ya kigeni ambayo kwa mtazamo, uchambuzi na uchunguzi ambao umekuwa ukifanya na kamati, taasisi, wanaharakati na vyombo mbalimbali vikiwemo vyombo vya dola, kama vile taasisi za kuzuia na kupamba na rushwa, ripoti mbalimbali za mkaguzi mkuu wa serikali na vingine vingi, vyote kwa pamoja vimethibitisha kuwa, mikataba hiyo haina manufaa kwa wananchi wa Taifa hili, hususani walalahoi, huku ikibaki kunufaisha watendaji hao wakuu wa Serikali (Walala Kheri) na mashirika au makampuni hayo ambayo wamekuwa wakiingia nayo mikataba hiyo ya kuiifirisi nchi na Watanzania kwa ujumla wao. 

Baadhi ya mikataba kama ile ya Richmond, Kagoda, EPA, mkataba wa TRC na mingine mingi ambayo umma tumepata kuiisikia, yote imekuwa ikikwamisha kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa nchi na kuongeza kasi ya kukua kwa umasikini miongoni mwa Watanzania na kuongeza hali ngumu ya kimaisha hususani kwa wananchi wa Vijijini. Mbali na hayo tumeona na kupata kusikia juu ya uuzwaji wa mali za umma kama vile maeneo ya wazi, viwanja vya michezo na viwanja kama kile cha KIUTA na vinginevyo. Hayo vyote hufanyika kwa ajili ya manufaa ya wachache na familia zao. 

Pia Sera ya ubinafsishaji hutumika vibaya kwa ajili ya kutimiza azma hizo za kupokonya mali za Taifa kwa ajili ya kujinufaisha wenyewe. Tumesikia na kushuhudia jinsi baadhi ya wananchi wa maeneo mengi yanayochimbwa madini kulalamika kila kukicha jinsi wanavyonyanyasika kutokana na ubinafsishaji huo. Sera hiyo si mbaya na kama ikitumiwa vyema, huweza kuliletea Taifa hili maendeleo makubwa na ya kasi mno, lakini kutokana na ubinafsi wa viongozi wetu, wamekuwa wakiitumia vibaya kwa kujichumia wao wenyewe. Je kwa mwenendo huu Tanzania ambayo Mungu ameijalia karibu kila kitu mfano; Maziwa, Mito, Mbuga, Madini, Ardhi, Amani na mengi mengine itabaki kuwa kama ilivyo sasa kwa ajili ya vizazi vijavyo? Bila shaka jibu ni hapana, wakati unakuja ambapo Tanzania yetu itabaki kuwa mapango matupu na hapatakuwa tena na chochote ambacho vizazi vijavyo vitaweza kujivunia kama ilivyo kwa kizazi hiki au kama isifikavyo nje ya mipaka yake kwa sasa. 

Wataalamu na washauri wengi wa uchumi, wamekuwa wakitoa ushauri mbalimbali kwa serikali na watendaji wake kwa ujumla, juu ya ni namna gani rasilimali zetu zinafaa kutumika ili kuongeza mapato ya Taifa na hatimaye kuinua uchumi wa Taifa, lakini cha kusikitisha ni kuwa, viongozi hao na watendaji wakuu wa serikali wamekuwa wakipuuza ushauri huu na kuendeleza matendo yao ya KIFISADI. Jambo hili limezidi kurudisha nyuma maendeleo ya Mtanzania mmoja moja na Taifa kwa ujumla. 

Kulindana na kutochukuliwa hatua kwa viongozi au watendaji ambao wamekuwa wakithibitika kufanya vitendo hivyo vya hujuma na ubadhilifu kumekuwa ni jambo la kawaida kabisa, hivyo kuwafanya wananchi wengi kukosa imani na serikali yao pia na viongozi waliopo madarakani. Hili huweza kuliletea taifa madhara makubwa, hususani pale ambapo wananchi wataamua kulazimisha mabadiliko ya uongozi au utendaji kwa kutumia NGUVU YA UMMA ambayo ndiyo silaha pekee wananchi waliyobakia nayo, katika kutetea na kilinda mali za nchi yao. Kama hili likitokea tunaweza kujikuta (Watanzania) tunapoteza ili sifa ya AMANI na UTULIVYO ambayo tumekuwa nayo kwa miaka mingi sasa tangu uhuru wetu. Mbali na hilo tunaweza kusababisha kuzuka kwa wimbi kubwa la ukimbizi kwa nchi za jirani hata zaidi ya ilivyokuwa wakati ule ambapo tuliitia dosari sifa yetu ya amani pale tulipozalisha wakimbizi baada ya machafuko yale yaliyotokea kule Zanzibar wakatifulani kama mnakumbuka. Pia tutaongeza umaskini na kuyumbisha kabisa ukuaji wa uchumi ambao kwa sasa unakua kwa kusuasua kutokana na matatizo lukuki yanayolisonga Taifa letu. 

Hivyo basi, sisi wapenda maendeleo tungependa kuiasa serikali pamoja na watendaji wake wote kuwa, wakati umefika sasa kwa wao kubalisha namna ya utawala wao wa kidhalimu na kuwajibika zaidi kwa watanzania na si kwa ajili yao wenyewe. Vilevile ni vyema kuhakikisha wanalinda na kuzitekeleza sheria za nchi, ili kuepusha migongano na migogoro ambayo huweza kusababisha vurugu na machafuko ya amani yatokanayo na kutotiiwa kwa utawala wa sheria. Wale wote wanaothibitika kuvunja au kuhujumu uchumi wanapaswa kufikishwa katika vyombo vya sheria na kuhakikisha sheria inachukua mkondo wake, ili kuwapa imani tena wananchi. Unyonyaji na kutumia mabavu hata pale pasipo hitaji nguvu za kiasi hicho, paepukwe na badala yake majadiliano zaidi yatumike ili kufikia muafaka. Uhuru wa kila mtu, vyama vya siasa na vyombo mbalimbali vya dola uheshimiwe, na nchi iendeshwe kwa demokrasia zaidi huku tukizingatia haki na sheria. 

Mwisho kabisa, uhuru wa kujadili na kutoa mawazo juu ya utengenezwaji wa katiba mpya kwa kila mtanzania usiingiliwe kwani ni haki ya kila mmoja kikatiba. Mchakato wa kutengeza katiba uwekwe wazi na usiharakishwe ili kukipa chama, watu au kikundi fulani manufaa kutokana na zoezi zima la kutengeneza katiba mpya. Katiba kimsingi ni sheria mama ambayo hutoa tashwira na mustakabali mzima wa maendeleo ya nchi na maisha ya wananchi kwa ujumla, hivyo mchakato usifanywe kiujanja janja kwa ajili ya kujinufaisha kwa watu wachache pekee, ila pawe na dhamira ya dhati ya kuleta mabadiliko ya Kitaifa na maendeleo kwa Jamii nzima.

Elimu juu ya zoezi zima la kutengeneza katiba, itolewe kwa kina ili kila mtanzania apate kuelewa kiundani ni nini anachopaswa kufanya (Kama vile afanyavyo, Pro. Issa Shivji, kupitia vipindi vyake vya Television - ITV). Hili litasaidia kupunguza au kuondoa kabisa minong'ono na manunguniko ya baadaye kuwa Katiba haiakisi malengo na maendeleo kwa manufaa ya watanzania wote.  Hivyo ni muhimu kuendela kuelimisha wananchi wote katika nyanja zote.


MUNGU IBARIKI TANZANIA.
    
    

Wednesday, May 16, 2012

TODAY'S QUOTE !!

“If you are neutral in situations of injustice, you have chosen the side of the oppressor. If an elephant has its foot on the tail of a mouse, and you say that you are neutral, the mouse will not appreciate your neutrality.” - Kattikiro Jr.

Tuesday, May 15, 2012

DIWANI CCM ATISHIA KUMUUA MBUNGE.


Polisi wamdaka na watoto wake

SIKU moja baada ya kundi la vijana wanaoaminika kuwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwacharanga mapanga wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, sasa ametishiwa kuuawa.

Habari zinasema kuwa Diwani wa Kata ya Nduli, Idd Rashid Chonanga, jana asubuhi alimvamia Mchungaji Msigwa ofisini kwake na kumtaka ajue kuwa siku zake zinahesabika, hata kama juzi alinusurika, lakini atahakikisha ameuawa kwa njia zozote zile, hali iliyomfanya mbunge huyo kukimbilia polisi kuomba msaada.
Diwani huyo, ndiye anayetuhumiwa kusimamia kikamilifu tukio la kucharangwa mapanga kwa wafuasi watatu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakati wa mkutano wa mbunge huyo uliofanyika katika uwanja wa kata ya Nduli na kuwajeruhi vibaya.

Katika mkutano huo ambao ulifanywa na mbunge huyo, mwenyekiti, katibu, wajumbe sita wa CCM wa kata ya Nduli na wanachama wengine takriban 90 walihamia CHADEMA, huku ikidaiwa kuwa wengine zaidi ya 150 wangelikihama chama tawala wiki hii.

Akizungumza akiwa polisi, Mchungaji Msigwa alisema kuwa kauli ya diwani huyo imemtisha kwa kuwa anajua ina baraka za viongozi wake wa ngazi ya juu.

Mchungaji Msigwa alilitaka Jeshi la Polisi lisifanye mzaha katika jambo hilo, kwa kile alichodai kuwa ni jambo la hatari na lenye lengo mahsusi la kuwatisha viongozi wa vyama vya upinzani na wananchi baada ya kuona kuwa CCM inazidi kupoteza maelfu ya wanachama wake kila kukicha.
Kamanda wa polisi mkoa wa Iringa, Evarist Mangalla, alisema hadi muda huo alikuwa hajapokea taarifa hizo, lakini akaahidi kulishughulikia jambo hilo kikamilifu, ili kulinda amani na usalama wa kiongozi huyo na raia wengine.

Hata hivyo, Vyanzo vyetu vya habari vimethibitishiwa kukamatwa kwa diwani huyo na vijana wa CCM waliohusika kuwakata mapanga watu watatu waliokuwa katika mkutano wa mbunge huyo juzi.
Mmoja wa maafisa wa polisi alidai kuwa miongoni mwa vijana waliokamatwa, wawili ni watoto wa diwani huyo na kwamba watu wengine wanne, akiwemo mfanyakazi wa diwani huyo, bado wanasakwa na jeshi hilo kwa kuhusina na tukio la juzi.

Akizungumzia kutishwa kwa maisha kwa mbunge Msigwa, aliyekuwa mwenyekiti wa CCM kata ya Nduli, Ayub Mwenda, alisema tangu jana amekuwa akipokea vitisho na kudai kuwa hali hiyo haitakisadia chama tawala, badala yake kinasababisha kichukiwe na hata na wale waliokuwa wakikipenda.

“Wananchi wengi wamechukizwa sana na tukio la juzi, na wakisikia tena na hili alilofanya huyu diwani leo, ndio itakuwa imezidi kujipalia mkaa. Hii ni nchi ya demokrasia ya vyama vingi, na kila mtu anayo haki ya kujiunga na chama chochote, sasa inashangaza kuona inakuwa nongwa kwao,” alisema Mwenda alipohojiwa na vyanzo vyetu vya habari hili.

Wakati huohuo, mmoja wa watu waliojeruhiwa vibaya katika shambulizi la mapanga juzi, Osca Sanga bado amelazwa katika hospitali ya mkoa, wakati wengine wawili waliruhusiwa jana.

Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, George Kabona, amesema Sanga anaendelea na matibabu, ingawa alikiri kuwa hali yake bado haijawa ya kuridhisha.

Monday, May 14, 2012

Uchaguzi wa Arumeru kuitikisa Kamati Kuu ya CCM

 Hali ya kisiasa nchini ambayo inajumuisha chaguzi mbalimbali zilizofanyika ukiwemo ule wa Arumeru Mashariki ambao Chama cha Mapinduzi (CCM) kilipoteza jimbo, ni miongoni mwa mambo ambayo yanatarajiwa kuvitikisa vikao vya Kamati Kuu, (CC) na Halmashauri Kuu ya chama hicho.
Katika uchaguzi huo ambao ulifanyika baada ya mbunge wake Jeremia Sumari kufariki dunia, mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Joshua Nassari aliibuka kidedea.
Kwa mujibu wa Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, jumla ya agenda 14 zitajadiliwa katika kikao hicho ambacho kilianza jioni jana.
Alisema hali ya kisiasa nchini ni miongoni mwa agenda ambazo zitakazojadiliwa katika kikao hicho.
Hata hivyo, alisema wanakusudia kuifanya agenda ya pekee ya hali ya uchumi ambayo kwa sasa huingizwa katika hali ya kisiasa. “Si mnafahamu kwamba hapa katikati kumefanyika chaguzi nyingi, zikiwemo za ndani ya chama ni miongoni mwa mambo tutakayojadili,”alisema Nape.
Alisema uchaguzi katika mashina na baadhi ya matawi umeshafanyika na kwamba watapokea taarifa ya maendeleo ya chaguzi hizo ili kama kuna jambo la kushauri wafanye hivyo.
Nape alisema agenda nyingine itakuwa itokanayo na vikao vilivyopita, taarifa mbalimbali na uchaguzi wa kujaza nafasi za makatibu wa mikoa.
Aliitaja baadhi ya mikoa hiyo kuwa ni Iringa na Dodoma.
Hadi tunakwenda mtamboni kikao cha Kamati Kuu kilikuwa kikiendelea baada ya kikao cha kamati ya maadili kilichokuwa kianze saa 4.00 asubuhi kuanza saa 7.30 na kumalizika saa 11.00 jioni.

Saturday, May 12, 2012

JE MISAADA YA KIGENI INATUSAIDIA AU HUNUFAISHA WACHACHE TU?


Inadaiwa kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinapokea misaada mingi zaidi ya kigeni duniani; tena wapo wanaodai kuwa tuko katika 'top 3'. Swali ambalo ninalo hasa baada ya wajomba zetu kuahidi kutoa mabilioni mengine ni kuwa wakati upande mmoja tunapoteza fedha kwenye ufisadi tena nyingi sana inakuwaje wajomba zetu wanaendelea kumimina mabilioni? Hivi hayo mabilioni yao hayawaumi kuona yanaliwa na wachache tuu na kutotumika kwa malengo husika? au misaada hiyo imelegwa makusudi kwa ajili yao ikiwa na malengo ya "nipe nikupe", kama ndivyo je watawala wetu wanamalengo gani na vizazi vya watanzania vijavyo?

Hivi wakiamua kusitisha misaada hii nini kitatokea kwenye uchumi na utendaji wa serikali yetu? Watanzania inabidi kujiuliza maswali haya sana na mwisho wa siku tufanye maamumzi makini ili kujinasua kwenye kitanzi tulichopo kwa sasa, kama si hivyo tuwe tayari kufa masikini na kumilikisha rasilimali zetu za nchi kwenye mikono ya wachache ambao wataendelea kuvuna na kuchumia matumbo yao na vizazi vyao vijavyo huku Watanzania wengine tukibaki tukilialia tu pasipo na pa kukimbilia.  Hebu angalia jinsi grafu hii ioneshavyo;

Watafiti wengi wa mambo, wamekuwa wakisema kuwa Watanzania wengi wamechoshwa na haya yanayoendelea nchini lakini wamekuwa ni waoga wa kufanya mabadiliko, wakihofia je nini kitatokea baada ya mabadiliko? Lakini wapenda maendeleo na wanaharakati wengi wamekuwa wakiwaasa Watanzania kutokuwa waoga wa kufaya mabadiliko kwani "udhubutu" unaweza kuwakomboa toka katika kitanzi cha umasikini walichovikwa na watawala wetu wa sasa.

Ushauri wangu;
Mabadiliko ni lazima, hofu ya madiliko ni sawa na kuendelea kuukumbatia umasikini, kwani siku zote watu husema kuwa "The risk takers are the very successful ones". Hivyo Watanzania wasiwe na hofu ya mabadiliko bali wawe na uthubutu wa kufanya maamumzi, lakini kwa uangalifu na umakini mkubwa.

Wednesday, May 2, 2012

KANUNI ZA MSINGI KUELEKEA KATIBA MPYA


Ili kuweza kufikia Katiba Mpya itakayokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye ya vizazi vya Watanzania ni lazima kuhakikisha kuwa mchakato wa kufikia katiba hiyo unakuwa huru, wa wazi na ambao una uhalali wa kutosha kuweza kufikia kusema kuwa Katiba itakayopatikana kweli imetokana na watu.  Ni muhimu basi kuweka bayana mambo ya msingi ambayo yanaendana na mchakato mzima utakaosababisha Watanzania wafikie katiba Mpya. Ni mambo haya ndio yanahitajika kuonekana kwenye sheria itakayosimamia mchakato wa kufikia Katiba Mpya.

LENGO:  
Kupatikana kwa Katiba Mpya ya Taifa la Tanzania itakayokidhi mahitaji mbalimbali ya kisiasa na kiutawala na ambayo itatokana na utashi, nia, matamanio, kiu, njozi na matarajio ya Watanzania. Katiba hiyo inatakiwa ipatikane kabla ya kufika mwaka 2015 ili kuhakikisha kuwa chaguzi za serikali za Mitaa za Mwaka 2014 na uchaguzi mkuu wa 2015 vyote vinafanyika chini ya Katiba Mpya.

UTOFAUTI WA MCHAKATO WA TANZANIA KUJIANDIKIA KATIBA MPYA
Jambo la kwanza la msingi ambalo tunahitaji kulitambua ni kuwa kwa Tanzania kuamua kuandika Katiba Mpya wakati huu ni jambo ambalo ni tofauti sana na nchi au jamii nyingine za watu ambazo zimewahi kufanya hivyo. Nchi nyingi zimelazimika kuandika Katiba Mpya kutokana na sababu ambazo kwa Tanzania hazipo kwa kiasi kikubwa. Kimsingi baadhi ya mabadiliko tunayoyataka yangeweza kabisa kufanyika kwa kufanya mabadiliko ya Katiba kama tulivyowahi kufanya huko nyuma lakini tumeamua kuandika Katiba mpya kwa namna ambayo naweza kusema ni ya kipekee sana duniani.

Hatuanzii kutoka kwenye sifuri.
Taifa letu linapoamua kuandika Katiba Mpya hatuanzii kwenye sifuri. Si kwamba hatujawahi kuwa na Katiba au hata kuwa na Katiba yetu. Kwa miaka karibu hamsini serikali zote mbili zimekuwa zikiongozwa na Katiba na hivyo suala la “katiba” siyo jambo geni. Jambo hili ni muhimu kulizamisha moyoni kwa sababu kwa vile hatuanzii kwenye sifuri ina maana ya kuwa mchakato wenyewe kimsingi hauitaji muda mrefu sana.

Ndio maana kinyume na watu wengine wanaotaka elimu ya muda mrefu ya “katiba” wanachukulia kana kwamba Watanzania hawajawahi kabisa kusikia Katiba au hawajui umuhimu wa Katiba. Wanafunzi wetu katika ngazi mbalimbali wamejifunza kuhusu Katiba na wanajua umuhimu wake. Kufikiria kwamba tunaenda kwa Watanzania wakiwa hawaelewi lolote ni dharau kwa Watanzania.

Watu ambao wamekuwa wakipiga kura, wakishiriki nafasi za uongozi na wakiandika katiba za taasisi zao mbalimbali hadi vijijini kuchukuliwa kuwa hawaelewi maana ya “katiba” au “umuhimu wa Katiba” ni kejeli dhidi ya uelewa wa Watanzania na tunaweza kuona kama ni dharau ya wazi. Watanznaia wanafahamu maana ya Katiba na wamekuwa tayari kwa miaka karibu ishirini kuanza mchakato huu.


Hatuanzii kutoka kwenye vurugu
Nchi nyingi ambazo zimelazimika kuandika Katiba Mpya zimejikuta zikifanya hivyo zikiwa zinatoka kwenye vurugu za kisiasa na hasa vita na udhalimu. Nchi kama Eritrea na nchi kama Marekani zilijikuta zinaandika Katiba zao zikiwa zinatoka katika vurugu na vita. Hili ni kweli pia kwa baadhi ya nchi ambazo zimekuwa katika mazingira hayo.

Hatuanzii kama tunaotoka katika ukoloni au utawala usio halali
Nchi kama Afrika ya Kusini au nchi nyingi ambazo zimetoka kwenye utawala usio halali zimejikuta zikilazimika kuandika Katiba Mpya ili kuakisi ukweli mpya wa kihistoria katika nchi hizo.

Kwa msingi huo ni wazi kutambua kuwa tunapotaka kuandika Katiba Hii mpya tunakuja kama Taifa ambalo limefikia mahali pa kukomaa. Kama nikichukulia mfano wa familia ni kuwa katiba zetu za awali za tangu baada ya Uhuru na Muungano ni katiba ambazo zilikuwa za kutusaidia kuweza kupita katika maisha ya utoto na ujana.

Sasa hivi taifa letu limefikia ujana na sasa liko tayari kutoka nyumbani kwa wazazi na kuwa taifa huru zaidi na lenye kuwajibika zaidi na ambalo liko tayari kushika majukumu makubwa zaidi. Hivyo, Katiba yetu mpya tunayotaka kuiandika ni sehemu ya kujieleza kwetu (self expression) kama taifa miaka ya kuelekea utu uzima. Hivyo, basi ni lazima mfumo mzima wa kuelekea uandishi huo wa Katiba Mpya uwe unaakisi ukweli huu kuwa Watanzania wanataka Katiba Mpya ambayo itawakilisha maisha ya Taifa kuelekea mbele zaidi na kuweza kuacha urithi mzuri wa kizazi kijacho.

Kutokana na hilo basi mchakato wa kufikia Katiba Mpya unapaswa kuongozwa na
  • Kanuni za Msingi za Kuandika Katiba Mpya
  • Mgawanyo wa Mchakato ili kuhakikisha mawazo na mipango inatekelezwa ipasavyo.
  • Vyombo huru vitakavyosimamia mchakato huo

KANUNI ZA MSINGI ZA KUANDIKA KATIBA MPYA
Ili kuweza kufikia Katiba Mpya ni muhimu kuongozwa na kanuni za msingi ambazo zitaainishwa na kuonekana vizuri katika sheria itakayosimamia mchakato huo wa kuandika Katiba Mpya. Pasipo kuwa na kanuni za msingi ambazo zitaongoza mchakato mzima ni vigumu kuwa na sheria itakayosimamia mchakato huo vizuri.

KANUNI YA KWANZA MCHAKATO UHUSISHE WOTE
Mchakato wa kufikia Katiba Mpya usipoweka msingi ambao utahakikisha wananchi wote wana nafasi sawa ya kuchangia mawazo yao juu ya yale wanayoyataka kwenye Katiba Mpya basi utakuwa ni mchakato mbovu. Utaona sijasema “kukusanya maoni”. Ninachozungumzia ni kuwa ni jambo moja kutoa maoni na ni jambo jingine kufanya mawazo yako yasikike. Kwa wale tunaokumbuka mchakato wa kurudisha vyama vingi tunakumbuka jinsi kina Marmo walivyopita na “kukusanya maoni”.

Japo wenyewe walijivunia kuwa walifanya kazi nzuri ukweli ni kwamba mfumo uliotumiwa ulihakikisha wenye kutoa maoni ni wasomi, wenye sauti na zaidi watu ambao katika maisha yao walikuwa na nafasi fulani za kuweza kusikika. Hata katika maeneo ambayo wananchi wa kawaida walitoa maoni hakukuwa na mjadala wa kutosha kati ya watu na watu kabla ya kufika kwenye tume ya maoni.

Yaani, kwa masaa machache watu walitakiwa kutoa maoni yao kwenye kikao cha masaa machache kabla hawajaondoka hao wanakamati kwenda mji mwingine “kukusanya maoni”. Kama vipepeo tume ya kukusanya maoni iliruka ruka na kupokea mshiko wa nguvu toka serikali ikikusanya maoni na baadaye kutoa ripoti yake. Matokeo yake asilimia 80 ya waliohojiwa walitaka tuendelee kuwa na mfumo wa chama kimoja. Wao wenyewe waliamini ni kwa sababu “CCM inapendwa” lakini hawakutaka kuangalia kuwa wananchi hawakuwa na muda wa kugonganisha mawazo yao ya kutosha.

Mbinu hii ya kukusanya “maoni” kwa mtindo ambao umewekwa kwenye mswada (ambao hauna tofauti na ule wa kina Marmo chini ya Tume ya Nyalali). Mbinu ya kukusanya maoni hairuhusu mjadala huru wa watu kuweza kushawishiana badala ya kukusanya maoni tu. Sasa tukikubali tume ya “maoni” kama ilivyo tujue mapema kabisa kuwa hawa watu watapita, wanakijiji wataitwa, kutakuwa na maelezo ya hapa na pale, maswali yataruhusiwa na wajumbe wataonekana wanaandika andika kwenye makaratasi yao na baadaye kikao kitaisha na watu watarudi makwao wakiwa “wametoa maoni”yao.

Lakini mfumo bora ni ule wa kuhakikisha kuwa watu wote wanahusishwa siyo tu watu wachache wanatoa maoni lakini watu wote wanahusishwa katika Mjadala wa Katiba Mpya. Kwa hiyo sheria itakayosimamia mchakato wa kufikia katiba Mpya ni lazima iweke mfumo mzuri wa kuendesha mjadala kwa watu wengi zaidi KABLA ya kuanza kukusanya Maoni. Maana yake ni kwamba kabla wananchi hawajaanza kuulizwa kutoa maoni yao ni lazima yawepo mazingira ya kiasi cha juu kabisa (optimal environment) ambapo wananchi watashiriki mjadala wa katiba katika mashule, makanisa, misikiti, maofisini, mitaani, kwenye vyama vya siasa n.k. Kabla ya kuanza kuratibu maoni tufanye mjadala kwanza ambao utahusisha Watanzania katika ngazi zao zote.

KANUNI YA PILI: MJADALA URUHUSU YOTE KUZUNGUMZIKA
Hatuwezi kufikia Katiba Mpya inayotokana na wananchi wenyewe na inayowastahili wananchi wenyewe kama hatuwezi kujadili na kuzungumza yote yanayotuhusu kama raia na kama binadamu. Ibara ya 9:2 ya mswada huu ambao umependekezwa kusimamia mchakato unatuambia kuwa tunaweza kuzungumza mambo mengine yote lakini tusije kugusa mambo 10 ya msingi. Mambo hayo wataalamu wetu waliotuandikia mswada (sijui walikuwa watu wangapi) wametuambia kuwa mambo hayo kumi hatayakiwi kuguswa au kubadilishwa.

Sasa hawa watu sijui nani kawapa uwezo wa kuwaambia wananchi milioni 43 na ushee kuwa wasizungumzia mambo fulani fulani au hata kuyafuta. Ndugu zangu tunapotaka kuandika Katiba Mpya ni LAZIMA mambo yote yaletwe mezani hakuna “mambo matakatifu yasiyogusika”. Katika mjadala wa Katiba Mpya hata mambo ambayo hayako mezani na yamewekwa pembeni ni lazima tuyatafuta na kuyaleta pembeni hata yale ambayo labda tulishayatupa inabidi tukayachukue huko na kuyaleta mezani.

Huu ni mjadala wa Katiba Mpya yaani nyaraka kuu itakayosimamia maisha ya Watanzania. Ndio maana kwenye nchi nyingine Katiba ina nguvu kuliko maandiko matakatifu na hii si kufuru. Kama Maandiko Matakatifu tuliletewa na watu na kuambiwa kuwa ni neno la Mungu kwa sababu kuna watu walitokewa na Mungu, malaika au walivuviwa na wakatupatia neno la Mungu na wengi wetu tumejikuta tukiamini. Hata leo utaona watu wanapigana na kuumizana kwa sababu ya maandiko hayo. Lakini Katiba (kwa maoni ya baadhi ya watu) ni juu ya vitabu hivyo vitukufu! Kwa sababu katiba ni sauti ya watu ambayo ina nguvu kama sauti ya Mungu. Yaani, kama kungekuwa hakuna vitabu vitakatifu vya kutuamulia maisha yetu ya kiroho basi binadamu tungetakiwa kuwa na mfumo fulani wa kujiongoza na mfumo huo ungekuwa ni mtakatifu kwa sababu unatokana na sisi wenyewe.

Vivyo hivyo Katiba. Kuna msemo wa Kilatini kuwa Vox Populi, Vox Dei yaani sauti ya watu (ni) Sauti ya Mungu. Katiba basi inatakiwa kuwa ni nyaraka ambayo inaakisi sauti ya watu kuhusu maisha yao na mfumo wanaotaka uwaongoze na watu hao wakiwa na taarifa sahihi, wakibadilishana mawazo na kushawishiana kwa hoja mbalimbali huweza kufikia kitu kilicho bora zaidi. Sisi binadamu tumepewa uwezo na Mwenyezi Mungu kufikiria na kutambua kitu ambacho hatukitaki hata kama hatuna uhakika wa kile tunachokitaka. Kwa mfano hakuna mwanadamu anayependa kudhulumiwa na mtu mwingine, au anayependa kufanya mtumwa na mtu mwingine. Hii hata hivyo haituzuii kuwadhulumu wengine! Kumbe Katiba ikiruhusu kuzungumzwa kwa yote inatusaidia kuona ni kitu gani hatukitaki na ni kitu gani tunaelekea kukitaka au tunajua tunakitaka.

Ni kwa sababu hiyo basi YOTE LAZIMA yaruhusiwe kuzungumzwa na kujadiliwa. Kusiwe na mada ambazo ni MWIKO. Hivyo sheria yoyote itakayosimamia mchakato wa Katiba ihakikishe kuwa wananchi wanashiriki kutoa mawazo yao kwa kila jambo. Ili hili lifanikiwe ni lazima kwanza kabisa kufanyia mabadiliko sheria ya Usalama wa Taifa ya 1970 pamoja na Sheria ya Magazeti ya 1976 kwani sheria hizo mbili ni kizuizi kikubwa cha uhuru wa mawazo na maoni kuliko kitu kingine chochote.

Hivyo, katika mjadala huu ni lazima wanaotaka Muungano uvunjwe waruhusiwe kuzungumza mawazo yao bila ya kuogopa kutiwa pingu; wanaotaka muda wa kikomo cha Urais uondolewe ili Rais aweza kugombea bila kikomo kama wabunge waruhusiwe bila ya kuonekana “si wana demokrasia”, wanaotaka Tanzania iwe Ufalme wa Kikwete na tuondokane na mfumo wa Urais waruhusiwe kutoa mawazo hayo. Naam, hata kama kuna watu wanataka kuzungumzia kuwa Tanzania iwe na Sharia za Kiislamu au iongozwe kwa Sheria za Kanisa watoe maoni yao vile vile. Tunapozungumzia Katiba Mpya ni lazima tuweke utaratibu utakaoruhusu mawao YOTE kutolewa hata yale ambayo hatuyapendi au yale ambayo yanatugusa vibaya.

Ninaposema YOTE nina maana kusiwepo na watu ambao watasema “hilo halizungumziki”. Kwa mfano wakati wapo wanaoweza kutaka tusema kwenye Katiba kuwa Tanzania inamuamini Mungu tujue wapo ambao pia wangependa tutambue haki za mashoga na wapo ambao wanaweza wakataka tutambue kuwa wanawake nao wanahaki ya kuolewa na mume zaidi ya mmoja!

Kwa hiyo, tunaporuhusu mjadala wa mambo yote maana yake ni kuwa tutakapofika wakati hasa wa kuanza kukusanya maoni na hatimaye kuanza mchakato wa kuandika Katiba tutakuwa tumesikia hoja karibu zote zenye kugusa wananchi karibu wote na hasa zile hoja ambazo pasipo mjadala kama huu zisingeweza kutolewa. Matokeo yake ni kuwa baada ya mjadala huru wenye kuhusisha watu wote na wenye kuzungumzia mambo yote basi mawazo yaliyo BORA ZAIDI na yenye kuvutia WATU WENGI ZAIDI ndio yatakuwa msingi wa Katiba.

KANUNI YA NNE: MCHAKATO UONESHE KUWA NI WANANCHI WANATUNGA KATIBA YAO

Demokrasia ni utawala wa watu. Neno Demokrasia linatoka kwenye Kigiriki likiunganisha maneno mawili 'demo' yaani watu na 'kratia' yaani madaraka au nguvu au utawala. Kimsingi demokrasia ni madaraka au utawala wa watu. Ni kinyume na Theokrasia (utawala wa Mungu) au utawala wa watu mashuhuri yaani Aristokrasia. Kwenye demokrasia wananchi ndio hutawala.

Hakuna wakati ambao wananchi wanaweza kuonesha nguvu yao ya kutawala kama katika kuandika katiba wanayoitaka. Kwa vile tunataka kuishi katika demokrasia basi hatuna budi kuhakikisha kuwa mchakato wa kuandika Katiba Mpya unawapa wananchi wetu nafasi ya kuandika Katiba yao – siyo nafasi ya kutoa maoni tu kuhusu Katiba yao.


Kanuni hii ya tatu inatokana moja kwa moja na hizo mbili za kwanza. Ukisoma mswada ulioandaliwa na “wataalam” wetu utaona ni jinsi gani kama nilivyosema awali waandishi wetu hawajapata ujumbe wa kwanini tunataka Katiba Mpya. Ushahidi ni matumizi ya neno Rais na Wananchi. Neno “Rais” linatokea mara 12 katika mswada huo, neno “mwananchi” linatoka mara mbili na moja kati ya hizo ni “asiye-mwananchi) na neno “watu” linatokea mara nne tu. Kwa maneno mengine, hawa watu walioandika mswada huu walikuwa wakiongozwa na fikra za kutekeleza na kulinda maslahi ya Rais.

Katiba Mpya siyo zao la Rais aliyeko madarakani. Kutokana na hilo mchakato wowote ambao unampa nguvu kubwa Rais (kana kwamba ni mfalme wa Tanzania) ni mchakato mbovu unaohitaji kukataliwa. Walioandika inaonekana ni watu walioamua kufuata njia yenye vikwazo vidogo zaidi (a path of least resistance). Kwa maneno mengine hawakutaka kufikiria zaidi ya namna nyingine ya kufanya kitu hata kama ni bora zaidi na hivyo wakaamua tu kumrundikia Rais majukumu mengi na yasiyo na sababu. Kimsingi wanachopendekeza hawa walioandika ni TUME YA RAIS YA KUPITIA KATIBA.

Sasa kama watu wangetaka Rais aunde tume tungeomba Rais aunde tume! Hakuna aliyemuomba Rais aunde tume na wala hakikuhitajika kibali chake kwenye suala la Katiba Mpya. Katiba Mpya ni zao la Watanzania na hasa ni zao la WANAMAGEUZI nchini. Sasa kuandaa mswada wa kusimamia mchakato huo bila kuwashirikisha wanamageuzi siyo kutendea haki kwa sababu baada ya kuiteka hoja ya “katiba mpya” sasa wameenda mbele zaidi na wameamua kuteka mchakato wa kufikia Katiba Mpya na tukiwakubalia watateka na katiba mpya.

Ninachosema kwa maoni yangu ni kuwa sheria itakayosimamia mchakato wa kufikia Katiba Mpya ni lazima itambue kuwa katiba ni lazima itokane na wananchi, kufikiwa kwake ni lazima kuoneshe kuwa ni Katiba ya Wananchi na hivyo hata muundo wa mfumo wa kuifikia uwe ni ule wenye kuheshimu hilo. Bila ya Wananchi kushiriki katika kuandika Katiba hiyo basi Katiba itakayopatikana haiwezi kuwa halali.

Pamona na ukweli wa kanuni hizo hapo juu nina uhakika kuwa mswada huu unaweza kupita ukiwa na mabadiliko machache tu. Ninachojua ni kuwa endapo mswada utapita jinsi ulivyo au ukiwa na mabadiliko machache tu tutakuwa tumerasimisha mchakato wa Katiba Mpya mikononi mwa CCM. Hivyo, huu utakuwa ni utaratibu wa CCM kufikia Katiba Mpya. Yaani, wao ndio wataamua Katiba Iweje na kwa maoni yangu itakuwa ni dhambi kwa dhamira zetu kutoa ushirikiano wowote kwa tume hiyo ya Rais.

Kutokana na hilo ninaamini ni wajibu wa kila anayoengozwa na dhamira ambayo inamsuta kutoa ushirikiano kutofanya hivyo. CCM na serikali yake waendeshe mchakato wao na wafikie kwenye Katiba Mpya wanayoitaka wao. Sisi wengine tutaanza mchakato huru na wa wazi zaidi baadaye wa kuweza kuhakikisha kuwa wananchi wanatumia madaraka yao (kratia) ya kuweza kuandika Katiba wanayoitaka.

KANUNI YA TANO: KUTAMBUA UZITO NA UNYETI WA ZOEZI ZIMA
Tukitoka kwenye kanuni hizo tatu za juu ni wazi kuwa suala hili ni suala zito na nyeti. Ni suala ambalo matokeo yake yatabakia miaka mingi ijayo wakati sisi sote (tunaibishana leo) tukiwa tumeshageuka mifupa iliyosagika mavumbini. Ni lazima tujiulize TUNATAKA KUWAACHIA WATOTO WETU KITU GANI CHEMA KATIKA UTAWALA?

Tukifikiria kuwa tunataka kuandika Katiba Mpya kwa ajili ya kushinda uchaguzi ujao au kwa ajili ya kuiondoa CCM madarakani tutakuwa tumekosea. Tukifikiria kuwa tunaandika Katiba Mpya ili kumpunguzia Rais madaraka au kwa ajili ya kuimarisha Muungano tutakuwa tumekosea. Tunataka kuandika Katiba Mpya ili kuweza kukiachia kizazi kijacho mfumo mzuri wa utawala ambao utawapa nafasi ya kufanikiwa katika maisha na mipango yao na ambao utawahakikishia mtiririko mzuri wa mahusiano na kuwajibishana kati yao na watawala wao.

Hivyo, ni lazima tutambue “utakatifu” wa mpango mzima wa kuandika Katiba Mpya. Tunachotaka kukifanya ni sawasawa na kujaribu kuandika kitabu kitakatifu kutoka katika mioyo yetu na ambacho tutaapa kukilinda kwa maisha yetu. Tujue kuwa tunaposema “Katiba Mpya” maana yake kama kuna watu watakuja kuivunja au kuichezea wajue kabisa kuwa watapata hasira ya Watanzania wote.

Hivyo mchakato mzima ni lazima utambue ukuu, utukufu na upekee wa zoezi zima. Hili litaonekana katika mfumo na utaratibu utakaoewekwa. Hadi hivi sasa inasikitisha kuona kuwa watu wanafikiria zoezi la kuandika Katiba Mpya ni kama zoezi jingine lolote nchini; la hasha. Haliwezi kufuata taratibu tulizozizoea na kamwe halipaswi kuchukuliwa kama jambo la kawaida.

Ni kwa sababu hiyo naamini kuwa kikao cha sasa kifupishwe ili mambo mengine tu yajadiliwe lakini Bunge liurudishe mswada huu kwa serikali na kukusanya maoni bora zaidi (nami nitakuwa tayari kutoa maoni ya mchakato bora ambao utaakisi kanuni hizo hapo juu). Ila kifanyike kikao maalum cha Bunge ambacho kwa kuitwa kwake kitakuwa kinaonesha watawala wetu wanatambua uzito wa tukio lililo mbele yetu.

Badala ya kufanya haya mazingaombwe ya “vikao vya Kamati ya Katiba” ambavyo vitakutana na wananchi Dodoma, Dar, na Zanzibar kama wawakilishi tu wa mawazo ili waweze kusema “tulikusanya maoni” ni bora tuvute pumzi na tujipange vizuri ili kuweza kuonesha kuwa tunaelewa uzito wa kitu ambacho kama taifa tunataka kukifanya.

Binafsi ninaamini watawala wetu bado hawajelewa uzito wa jambo hili. Yaani kuliweka kama sehemu ya kikao cha kawaida ni kutolipa jambo hili uzito wake. Ninaamini suala la Katiba Mpya ni sawasawa na Musa alipopanda mlimani ili apewe Amri Kumi za Mungu – Katiba ya Wanaizraeli wa enzi hizo. Ilikuwa ni jambo la kuogofya. Sisi hatuendi milimani bali tunaenda kwa wananchi ambao ndio asili ya madaraka yote. Ni lazima tutetemeke na kuogopa kwa sababu watakuja na amri gani hatujui.


Ninaamini
Kikao Maalum cha Bunge cha kujadili Mswada wa Sheria ya Kuongoza Mchakato wa Katiba Mpya kiitwe hata kama kitakuwa ni cha siku tatu tu. Kikao hicho kisiwe sehemu, ya kikao cha kawaida (kama cha sasa au vikao vilivyotangulia tayari) au kile cha Bunge la Bajeti. Kiwe ni kikao maalum. Ni kwa namna hii tutaweka heshima ya jambo ambalo tunataka kulifanya.

Na tukifanya hivyo tutatoa muda kwa pande nyingine kutolea maoni sheria hizo na hata kwa upinzani kuja na mapendekezo ya mswada wao ili hatimaye miswada hiyo miwili (au zaidi) iweze kujadiliwa na hatimaye upatikane mswada ulio mzuri zaidi. Kama tulivyokosoa mswada wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi na watu walidhani tunawaonea wivu lakini tulikuwa sahihi nina uhakika tuko sahihi wakati huu tena.

Mswada huu ukipitisha kama ulivyo utachangia ujio wa sheria nyingine mbovu zaidi ambao katika dhamira safi baadhi yetu tutashindwa kuitii. Sasa kama tunataka kweli kufikia katiba Mpya ni lazima kwanza tubadili fikra. Watawala wasidhani wanatutendea hisani na wananchi tusifikirie tunabembeleza watawala wetu. Ni bora tusubiri miaka mitano tuweze kuleta timu itakayotuongoza kufikia katiba mpya kuliko tuharakishwe ndani ya miaka hii mitano kuongozwa kuelekea kwenye machozi. Katiba mpya itokane na fikra mpya.

Mungu ibariki Tanzania.