To Chat with me click here

Friday, July 11, 2014

TENDWA: KIKWETE AMETELEZA KUSEMEA MSIMAMO WA CCM BUNGENI


Aliyekuwa msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwakwe.


Dar es Salaam.  
Aliyekuwa msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa amesema Rais Jakaya Kikwete aliteleza kueleza msimamo wake na ambao baadaye ulibainika kuwa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wakati akizindua Bunge Maalumu la Katiba, Machi 21.

Tendwa, ambaye alistaafu Agosti mwaka jana na nafasi yake kuchukuliwa na Jaji Francis Mutungi, alitoa kauli hiyo jana katika mahojiano maalumu na Mwananchi ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

Tendwa, ambaye alikuwa Msajili kwa miaka 13, alisema akiwa kiongozi mkuu, Rais Kikwete alipaswa kutoa mwongozo wa uendeshaji wa Bunge Maalum la Katiba.

“Sikuwapo nchini, lakini kwa kadri ninavyoelezwa, kama hiyo ni kauli yake, basi alijisahau kusemea msimamo wa chama chake, (CCM) na sera yake ya serikali mbili katika bunge hilo,” alisema.

“Rais ni mtendaji, alipaswa kutoa guidelines (miongozo) ya jinsi ambavyo Bunge Maalum la Katiba linatakiwa kufanya. Alichokisema, aliteleza.

“Alijisahau na kurudi kwenye chama kwa sababu hiyo ndiyo sera ya chama chake, ” alisema Tendwa.

“Na siyo yeye tu (Kikwete) kwani nimemsikia hata Dk Shein (Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi), akisema kuwa msimamo wa CCM ni serikali mbili,” aliongeza Tendwa.

“Nimemsikia  Makamu wa Pili wa Rais (Balozi Seif Ali Iddi)  akisema hivyo na  Rais wangu (Kikwete) katika mikutano mbalimbali ya hadhara, naye amelisema hilo.”

Madai ya kuibeba CCM
Tendwa ambaye katika uongozi wake wa miaka 13 alikuwa akituhumiwa mara kwa mara na vyama vya upinzani kuwa anakibeba chama tawala, alisema: “Nadhani na yeye (Rais Kikwete) kasema. Nadhani alijisahau kuwa ni kiongozi wa taifa.”

“Rais ni mtendaji na mimi nasema aliteleza. Turudi katika hoja kwa kujadili rasimu iliyoko mezani.”

Kauli hiyo imekuja kipindi ambacho baadhi ya viongozi wakiwamo wa vyama vya siasa nchini, Dk Wilbroad Slaa (Chadema), Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Shariff Hamad na pia aliyekuwa mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, pia kumkosoa Rais Kikwete.

Kwa nyakati tofauti, wameeleza kuwa Kikwete ndiye mtu pekee anayeweza kutuliza mvutano ulioibuka katika mchakato huo unaoendelea kwenye Bunge la Katiba.

Ulikoanzia mzozo
Machi 21, wakati akifungua Bunge Maalum la Katiba,  Rais Kikwete aliipinga Rasimu ya Pili ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Jaji Warioba, akigusia mambo saba ya msingi yaliyomo katika rasimu hiyo na kutaka yatazamwe kwa kina, kubainisha kuwa mengine hayawezi kutekelezeka.

Miongoni mwa mambo hayo ni muundo wa Muungano kuwa wa serikali tatu uliopendekezwa katika rasimu hiyo.

Kikwete, ambaye alisema anatoa maoni yake binafsi, alipinga waziwazi pendekezo la serikali tatu na kuegemea katika muundo wa serikali mbili unaoungwa mkono na CCM, huku akifafanua kuwa idadi ya watu waliopendekeza muundo wa serikali tatu ilikuwa ndogo.

Walilosema wengine
Julai 7, wakati akizungumza katika kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na televisheni ya ITV,  Maalim Seif alimtupia lawama Rais Kikwete kuwa amechangia kuukoroga mchakato wa katiba kwa kufuata msimamo wa chama chake, badala ya maoni ya wananchi yaliyomo katika rasimu ya pili ya katiba.

Maalim Seif, ambaye alilenga kauli iliyotolewa na kiongozi huyo wa nchi wakati akifungua Bunge la Katiba, alisema kauli ya Rais Kikwete imeondoa imani ya wananchi kuhusu kupatikana kwa katiba inayotokana na maoni yao.

Alisema mchakato huo hivi sasa unamtegemea Rais pekee, huku akisisitiza kuwa hakuna binadamu aliyekamilika na kumshauri kutafuta uwezekano wa kuweka mambo sawa, ili kujenga tena imani kwa wadau wote.

Julai 4, Dk Slaa, wakati akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili jijini Dar es Salaam, alimtaka Rais Kikwete kujitokeza hadharani kutafuta suluhu ya kupata mwafaka wa mchakato wa Katiba Mpya kwa kuwa hakuna mamlaka nyingine zaidi inayoweza kuunusuru.

Naye Jaji Warioba kwa nyakati tofauti amemshauri  Rais Kikwete kuchukua hatua zitakazoondoa matatizo katika Bunge la Katiba ili kuwezesha mchakato huo kukamilika.

Alisema ni muhimu kiongozi huyo mkuu wa nchi kuweka kando tofauti za mawazo na mitazamo ili kupata Katiba Mpya kwa masilahi ya Taifa.

Mwanzoni mwa wiki, mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mbeya na naibu waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Godfrey Zambi alifichua kuwa msimamo wa serikali mbili unaoonyeshwa na wabunge wa chama hicho ni maagizo ya Kikwete.

NEC YAKWAZA WAPINZANI, WAKATAA MFUMO MPYA WA KUANDIKISHA WAPIGA KURA!




VYAMA vya upinzani vimepinga teknolojia mpya ya Biometric Voter Registration (BVR), itakayotumiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kwa ajili ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga kura vikidai mfumo huo umetumika Zanzibar, lakini bado una changamoto nyingi.

Hatua hiyo ilijitokeza jijini Dar es Salaam jana, wakati NEC ilipokutana na viongozi wa vyama vyote vya siasa, kikiwemo CCM, ili kupeana taarifa kuhusu maandalizi ya uboreshaji huo utakaoanza Septemba.

Pia, mkutano huo ulikuwa kwa ajili ya NEC kuwaonyesha viongozi hao jinsi mtambo mpya utakavyofanya kazi. Lakini ulipofika wakati wa kuonyeshwa mtambo huo, viongozi wa NEC walidai wako nyuma ya muda.

Uamuzi huo ulionekana kumkera Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), na hivyo kuhoji kwanini waliahidi kuwaonyesha mtambo  halafu waseme wako nyuma na muda.

“Mmetuambia kuwa mtatuonyesha jinsi mtambo huo utakavyofanya kazi, lakini sasa hivi mnasema muda umeenda, hivyo mtatuonyesha ulivyo tu bila ya kuona utendaji wake wa kazi, haina maana yoyote, kama hilo limeshindikana ni bora tuendelee na ratiba zingine,” alisema Lissu na kuungwa mkono na viongozi wengine.

Akizungumza na waandishi wa habari, Lissu alisema kuwa bado anaona kuna tatizo na kwamba kuna maswali mengi ambayo wanajiuliza na hawajapata majibu, hivyo bado hawajaelewa jinsi mfumo huo utakavyoleta mabadiliko na kuondoa changamoto zilizopo.

“Wamesema kitambulisho kitakuwa kina mfano wa kadi ya benki, kama ukikipoteza haupigi kura? Tume inaandikisha wapiga kura wengi sana na utaratibu wa sasa kama una kadi unaenda kujiandikisha na ukijiandikisha kwa sababu una kadi, kumbukumbu zako wanazo.

“Je, kama ulijiandikisha huna kadi, unaenda kujiandikisha kama mpiga kura mpya ambaye kumbukumbu zako haziko kwenye tume au unaenda kujiandikisha kama mpiga kura ambaye kumbukumbu zako ziko kwenye tume, lakini huna ushahidi wa kuwa na kadi?” alihoji.

Aliongeza kuwa kitu muhimu kinachohitajika kwanza ni mabadiliko ya sheria, kwamba tatizo kubwa lililopo mtu hata kama alijiandikisha akapoteza kitambulisho haruhusiwi kupiga kura, hivyo utaratibu huo hauwezi kuondoa tatizo.

“Namna ya kuliondoa ni sheria iseme wazi kwamba kama umejiandikisha, picha yako iko kwenye tume na ipo siku ya uchaguzi kwenye orodha ya kupiga kura, una haki ya kupiga kura kwani watu wanakufahamu na picha yako ipo,” alisema.

Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba, alisema tume imeeleza kuhusu mashine hiyo, lakini hawajaambiwa kampuni ambayo imehusika na jinsi gani inaweza kusimamia ikiwa na uzoefu gani.

Alisema Zanzibar wanatumia mtambo kama huo, lakini bado kuna matatizo mengi, hivyo tatizo sio mtambo ila ni utendaji.

Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alisema bado nchi iko nyuma kiteknolojia, kwani mtambo huo unatumiwa na nchi za Afrika tu, na kama ungekuwa na ubora ungetumika pia katika nchi zilizoendelea.

“Bado sijaona kama matatizo yataisha, nenda nchi zote za Ulaya, mfumo ni mmoja tu, wanatumia kitambulisho kwa kila kitu, lakini nchi yetu kila kitu kina mfumo wake,” alisema.

Mapema katika hotuba yake ya ufunguzi, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva, alisema mfumo wa BVR ni wa kuchukua au kupima taarifa za mtu kibaiolojia au tabia ya mwanadamu na kuzihifadhi katika kanzi data (Database), kwa ajili ya utambuzi.

Alisema kwa kutumia mfumo huo, wananchi wote wenye sifa za kuwa wapiga kura na wale walio na kadi za mpiga kura, watatakiwa kuandikishwa upya.

“Mtakumbuka kuwa vituo vya uandikishwaji uliopita vimekuwa katika ngazi ya kata, kwa utaratibu huu vituo vya kujiandikisha vimeongezeka kutoka 24,919 hadi kufikia 40,015 ambavyo vimewekwa katika ngazi za vijiji, vitongoji na mitaa ili kuwezesha kuwa karibu zaidi na wananchi,” alisema.

Kwa mujibu wa Jaji Lubuva, uchaguzi mkuu wa mwakani kwa mujibu wa Sensa ya 2012, utakuwa na wapiga kura 23,917,467 baada ya kutoa watu watakaokadiriwa watakuwa wamefariki.