To Chat with me click here

Friday, January 24, 2014

ZIJUE AHADI ZA SERIKALI KWENYE SEKTA YA ELIMU 2012/2013



Kila mwaka, katika mikutano ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wabunge, ambao ni wawakilishi wa wananchi, huiuliza Serikali maswali mbalimbali kuhusu mipango iliyopo kwenye sekta mbalimbali, ikiwemo elimu.

Mawaziri husika au wawakilishi wao hutoa majibu ambayo mara nyingi huambatana na ahadi. Je, baada ya hapo, nani ana jukumu la kufuatilia utekelezaji wa hizi ahadi? Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano (1977), wananchi ndio msingi wa mamlaka yote na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi. Pia, lengo kuu la Serikali ni ustawi wa wananchi na itawajibika kwao. 

Hii ina maana mwananchi yuko ndani ya wajibu na mamlaka yake akihoji na kufuatilia ahadi za serikali, kwani zinatolewa na viongozi wanaopaswa kuwajibika kwake. Ndiyo maana, tangu January 2014, nimeamua kuwaelimisha na kuwashirikisha watanzania ili waweze kutimiza wajibu wao wa kufuatilia ahadi za serikali na kuhakikisha vipaumbele vyao vimefikiwa.

ELIMU KWA WASICHANA, UFUNDI STADI, VIFAA VYA SHULE N.K


Baadhi ya wanafunzi wa kike wakiwa darasani wakifuatilia kipindi.
Kwa mujibu wa taarifa za Bunge, ahadi zifuatazo zilizotolewa Bungeni na Ummy A. Mwalimu, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto (4 Februari 2013), Hawa Ghasia, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (10 Aprili 2013) na Aggrey Mwanri, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (10, 19 na 23 Aprili 2013):

Serikali itaanza rasmi kujenga shule ya wasichana Borega (Halmashauri ya Wilaya ya Tarime) mwezi June, 2013. Ujenzi huu utakamilika ifikapo Novemba, 2014. Halmashauri kupitia mapato ya ndani imechangia shilingi milioni 28 na eneo la ujenzi limeshapimwa. Kwa sasa utaratibu wa kutangaza zabuni unaendelea.

Serikali imepanga kuviboresha vyuo vya maendeleo ya wananchi (FDCs) kwa kuvikarabati, kuvipatia watumishi na vyombo vya usafiri.

Serikali itatumia fedha za malipo ya fidia ya rada kwa ununuzi wa vitabu na madawati katika shule za msingi Tanzania Bara. Fedha itakayotumika kwa ajili ya ununuzi wa vitabu ni karibia shilingi bilioni 59 na fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawati ni karibia shilingi bilioni 20. Mchakato wa ununuzi wa vitabu umekamilika ambapo Serikali imeingia mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 57 na wachapishaji wa vitabu. Kulingana na mikataba, kazi hii inategemewa kukamilika ndani ya miezi sita tangu tarehe ya kuweka saini mikataba tarehe 18 Machi, 2013. Kwa upande wa ununuzi wa madawati, mchakato umeanza ambapo katika Kikao cha Bunge la Bajeti ya mwaka wa fedha 2012/2013 iliazimiwa kuwa madawati yanunuliwe na kusambazwa katika halmashauri zote kwa usawa.

• Katika juhudi za kutatua tatizo la madawati nchini, Serikali imekuwa ikipeleka fedha katika halmashauri kwa ajili ya ununuzi na utengenezaji wa madawati. Mwaka 2010/2011 shilingi bilioni tatu zilipelekwa katika halmashauri zote kwa ajili ya madawati ambapo Mkoa wa Mara ulipata shilingi milioni 197 na mwaka 2012/2013 shilingi bilioni moja zilipelekwa katika halmashauri zote kwa ajili ya madawati na Mkoa wa Mara ukapata shilingi milioni 68.

• Kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi Serikali imekuwa ikitoa fedha za uendeshaji wa shule (ruzuku) kwa kiwango cha shilingi 10,000 kwa kila mwanafunzi. Hadi kufikia mwezi Machi, 2013 Serikali imeshatoa jumla ya shilingi bilioni 60 za ruzuku kwa shule za msingi nchini kote. Kiasi hiki ni sawa na shilingi 7,565 kwa mwanafunzi ambayo ni sawa na asilimia 75.


Je, ahadi hizi zimetekelezeka? wananchi husika wa maeneo ambako ahadi hizi zililengwa kwao wana wajibu wa kufuatilia na kuhakikishwa zimetekelezwa. Tafakari na chukua hatua kwa maendeleo ya Taifa lako sasa.

Unaweza kupata habari hizi kila wakati kwa ku-click “LIKE” au katika “facebook page” yangu: Maxmillian Kattikiro FB-Page

No comments:

Post a Comment